AN-NUUR 
Na.170 Jamadul Akhir 1419, Oktoba 9 - 15, 1998 
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita
 
 
MAKALA 

Demokrasia ya rushwa ! 

Na Mwapwani Mohamed 

WAZIRI wa Mambo ya Nje wa Marekani Bibi Madeleine Albright alinukuliwa akitamba mbele ya vyombo vya habari vya kimataifa "We want to build a new democratic Sudan". Na hizo ndizo siasa za leo za Marekani za "kuleta haki za binadamu na kujenga demokrasia ya kweli duniani.  

Siasa hizo zilianzishwa na Bw. Jimmy Carter aliyepata kuwa Rais wa taifa hilo. Bw. Carter alipopata uongozi tu alianza kunadi siasa za "haki za binadamu", siasa hizo zinaendelezwa kwa kutumia Umoja wa Mataifa (UN) na hasa Baraza lake la Usalama ambalo limetekwa nyara na Marekani. 

Hali hii ilijionyesha wazi pale baa la njaa lilipoikumba Somalia, Marekani ikawa ya kwanza kupeleka majeshi yake huko kwa kofia ya Baraza la Usalama na kisingizio cha kwenda "kutoa misaada ya kibinadamu na kusaidia wanaokufa njaa", kumbe iligundulika kuwa lengo la Marekani lilikuwa kuivamia kijeshi Somalia, kuwatupia risasi wananchi wake na kumsaka aliyekuwa kiongozi wao Mohammed Farah Aideed. 

Ni haki hizo hizo za binadamu zilizowateketeza Wairaq wakati wa vita vya Ghuba kisingizio kilikuwa kumlazimisha Saddam atoke Kuwait, na hata sasa Wairaq wanaendelea kuteseka kufuatia vikwazo ilivyowekewa nchi Hiyo, kisingizio kikiwa "ukaguzi wa silaha za maangamizi alizonazo Saddam". 

Ulimwengu wote unaaminishwa kuwa katika Mashariki ya Kati silaha za sumu anazo Saddam peke yake na gaidi ni Usama bin Laden na wala hatuambiwi kitu chochote kuhusu silaha ilizonazo Israel inayowachinja ovyo Wapalestina na Walebanon na kukalia ardhi yao. Na leo Jerusalem ambapo ni mahali pa kwanza pa Kiblah imetwaliwa na Israel. 

Na hii inapelekea, amani huko Mashariki ya Kati kuwa kitu cha kufikirika tu, na hata huo unaoitwa mpango wa amani kati ya Israel na Palestine kuwa ndoto. 

Tuchukue kifungu kimoja cha mpango huo ambacho ni kuikubali Israel. Ina maana kuwa Israel ni lazima itambuliwe. Mpango unataka kuihakikishia amani Israel ambayo kwa miaka mingi inawaua watu wa Palestine na Lebanon na kukalia nchi zao. Na mpango huo ni kama kuipa zawadi Israel kwa yote iliyoyafanya mpaka sasa zawadi ya kuhakikishiwa amani. 

Mpango huu ukikubaliwa huenda kesho Israel ikafika mbali ikaamua kuzitwaa Makkah na Maddina. Kifupi tu "Mpango wa amani" ni agenda ya Israel kuitawala Mashariki ya Kati. 

Katika Afrika, "watengenezaji silaha za sumu na magaidi" ni Sudan, Libya, Algeria (FIS) ni nchi za Kaskazini mwa Afrika na hasa hizo tatu zilizotajwa, tukiiacha Misri ambayo serikali yake ilikuwa ikiwafanyia mateso makubwa wananchi wake. 

Afrika yote iliyobaki (tukiondoa Afrika Kusini chini ya Nelson Mandela) imebaki kuzitegemea Amerika na Ulaya kisiasa, kiuchumi, kijeshi na sasa kitamaduni. Afrika imepoteza fahari na heshima yake. 

Rais Yoweri Museveni wa Uganda alidiriki hata kushangilia kitendo cha Marekani kuzilipua Sudan na Afghanistan kwa tuhuma za kuhusika na ulipuaji wa mabomu katika ofisi zake za Dar es Salaam na Nairobi uliotokea Agosti 7, mwaka huu. 

Ni heri Museven angetueleza alichokuwa akikifurahia ili "tufurahie wote". Wapi tunakwenda, tunafikia kiasi cha kushangilia misiba ya jirani yako. 

Hizo ndizo demokrasia za kweli tunazoletewa na Marekani leo na zinazojengwa kwa mtazamo wa Amerika. 

Matokeo yake Wasudan wanakwisha leo kwa njaa na "kibri" cha Garang. Ulimwengu haujasikia Marekani ikitetea haki za binadamu wa Palestine, Lebanon, Vietman, Kosovo, Bosnia na kwingineko katika dhana kwamba Waislamu ndio viumbe pekee duniani wasio na haki. 

Na hii inawapa kichwa akina Madeleine kutaka kuzisaidia nchi nyingine kujenga demokrasia na hivi karibuni Bibi Hilary Clinton alinukuliwa na vyombo vya habari akimuelezea Clinton (mumewe) katika kampeni ya uchaguzi wa nchi hiyo kama mtu muhimu katika kuanzisha na kuendeleza "mazuri" ya Amerika ambayo wote "tunayafurahia" leo. Hatuelewi hiyo "wote" inawawakilisha akina nani. 

Ukiwaacha Waislamu, adui mwingine wa Amerika ni Fidel Castro wa Cuba ambayo mpaka leo inafuata siasa za kijamaa 

Ni muhimu tuonyeshe kuwa Uislamu ni dini kubwa ya umoja na kwamba Uislamu haukuja kwa Waarabu tu bali kwa ulimwengu wote. Ni vema Madeleine Albright na washirika wake wakaelewa maneno yaliyosemwa na mwanamapinduzi mmoja kuwa, "Demokrasi ya Magharibi na demokrasi ya Mashariki ni demokrasi ya rushwa, demokrasia ya Uislamu ni demokrasi ya kweli". 


Tujikwamue na janga la utwaghuti 

Na I. Kikong’ona 

KATIKA hija ya kuaga, Mtume (saw) ametuusia Waislamu kuwa tutakaposhikamana na Qur’an na mwenendo wake, ambao ndiyo ufafanuzi wa mwongozo aliotuletea Allah (sw) hakutokuwa na wakutupoteza. 

Ameyasema haya ili kututhibitishia kwamba kutokuwapo kwake siyo sababu ya sisi kupotezwa na matwaghuti endapo tutavikamata barabara vitu viwili hivi. 

Matatizo yanayotukabili hivi sasa yanaonyesha athari za kutoutafakari na kuutafsiri kwa vitendo usia huu wa Mtume, jambo ambalo limetupelekea kuingia kichwa kichwa katika kufuata sera za matwaghuti. 

Twaghuti ni yeyote yule anayeendesha maisha yake bila kuzingatia mipaka ya Muumba; kuishi na kufanya "sherehe" kabla ya kufa ndiyo dhana iliyojikita katika akili na kuongoza maisha ya matwaghuti. 

Kwa twaghuti haki haitokuwa machoni pake endapo itaonekana kuhatarisha kulifikia lengo lake, na batili itaendelea kuwa haki ikiwa ndiyo sababu inayomfanya aendelee kulitekeleza na kulifikia lengo lake. 

Kuua, kuonea, kudhuru, kusema uongo, kumpa haki asiyestahiki, kuendesha kampeni za kuiharibu jamii, kuwaingiza watu ugaidi, ubalakala n.k. Vyote vitafanywa na twaghuti ili kufikia lengo lake. 

Hakuna ukweli wenye kudumu katika kinywa cha twaghuti, kweli huwa kweli mbele yake endapo haitahatarisha maslahi na matakwa yake. Wala katiba haitakuwa na thamani na maana kwake endapo utekelezwaji wake utampa haki anayeitetea haki iliyo kinyume na malengo yake. 

Twaghuti hana rafiki wala jamaa wa kudumu, bali anachojali yeye ni kuangalia kwamba, kwa kiwango gani rafiki atamfanya afikie au kutofikia lengo. Ikiwa lengo litafikiwa kwa kumtoa kafara, ndugu, jamaa au rafiki hatosita wala halitokuwa jambo gumu kwake. 

Kwa kifupi, twaghuti hana aibu, utu, uadilifu, ukweli, huruma ni sifa iliyoko mbali kabisa katika maisha yake, sheria mkononi na ana vigezo vingi vya kuhukumia jambo (jambo.). 

Utwaghuti ni utaratibu wa maisha ambao kanuni na sheria za Muumba hazina nafasi. Katika mfumo wa kitwaghuti ni kawaida kuwaona "waheshimiwa" wanagombania kondomu na kuwashawishi wazazi wasione aibu kuwagawia watoto wao "Salama". 

Ni kawaida kabisa katika utwaghuti kuona mwanamke anajihifadhi kunyanyaswa, kudhalilishwa na kunyimwa haki zake za kiraia, lakini changudoa atatetewa na kutungiwa sheria ya kumlinda "haki za wanawake zinazotetewa ni zile za mabinti kunengua mbele ya waheshimiwa, U-miss na kutumiwa katika matangazo ya biashara. 

Badala ya kunufaika kutokana na maendeleo ya sayansi na teknolojia, utwaghuti humfanya binadamu awe duni zaidi ya mnyama na kuishi maisha ya khofu. Utawaona watu wakiwa kichele katika "mabidu" na Makasino wakifanya ngono waziwazi na kurushwa katika TV. 

Watu wanahamasishwa kuharibu akili zao na afya zao kwa kutumia ulevi, silaha kali za kumwangamiza binadamu zinasambawa na visingizio vya ugaidi vinatumika kuharakisha umwagaji wa damu. Kuuana, kubakana, kuporana n.k. vyote ni matunda ya utwaghuti. 

Asiyeona haya atakuwa bado amefunikwa na kuburuzwa na giza la utwaghuti, itamchukua muda mrefu kutoka huko ikiwa hana tabia ya kukutana na AN-NUUR. 

Haki, usawa, demokrasia, uwazi na ukweli ni nyimbo tu za kuwaliwaza Waislamu katika utwaghuti. Kinyume chake tunashuhudia Waislamu wakisakwa, kupigwa, kudhalilishwa, kuwekwa rumande na kuuawa hadharani kwa kulengwa shabaha. Kana kwamba hakuna katiba, serikali wala mahakama. 

Waislamu tuna mwongozo madhubuti, turejee katika Qur’an ili tuepukane na janga hili la utwaghuti. Tumekuwa tukitumika sana kupitisha na kutekeleza sera nyingi za kuuimarisha utwaghuti hata ikafikia kuwakana na kuwaangamiza ndugu zetu (49:6). 

Tuisome, tuitafakari, tuzingatie na kuitafsiri Qur’an kwa vitendo. Tuondokane na tabia ya "Qaala Sheikh". Tukumbuke kuwa twaghuti kazi yake ni kuwatoa watu katika nuru na kuwapeleka gizani. 

 
Juu 
 

YALIYOMO 
 
 

TAHARIRI 
Tutaendelea kudhalilishwa mpaka lini ? 

Waislamu wasisitiza: Nyumba ya Waziri Mkuu ni ya Waislamu 
Na Mwandishi Wetu 

Kuchomwa nyumba za wananchi 
Na Mwandishi wetu 

Maoni Yetu: 
Maisha ya Mtanzania yanapokosa thamani 

Nguruwe marufuku Kinondoni – Tume 
Na Kassim Juma 

Watanzania waanzisha Baraza la Waislamu Marekani 
Na Mwandishi Wetu 

Wanawake Hai wamtaka Rais azungumzie mauaji ya Mwembechai 
Na Mwandishi Wetu 

‘Serikali haiwezi kuzuia rushwa’ 
Na Kassim Msuya 

Makala ya Kimataifa 
Nani gaidi: Slobodan Milosovic au Usama bin Laden 
Na Mwandishi Wetu 

Afghanistan washindi dhidi ya uvamizi karne zote 
Na Faiza bint Abubaka 

MAKALA: 
Demokrasia ya rushwa ! 
Na Mwapwani Mohamed 

Tujikwamue na janga la utwaghuti 
Na I. Kikong’ona 

MAONI: 
Nini Jihad na nani Mujahidina ? 

MAKALA: 
Marekani ni magaidi wa haki za binadamu 
Na MUSSA ALLY 

Tufuate Uislamu kwa vitendo na siyo kwa maneno -2 
Mwandishi: Maalim Ali Bassaleh 

Tusihalalishe mauaji ya raia kwa kisingizio cha ‘wananchi wenye hasira’ 
Na Mwandishi Wetu 

Historia ya sayansi na tiba 
Na Dk. Amur A.A. 

Msiwageuze watoto ombaomba 
Na H.E. Omar 

MAKALA YA JAMII: 
Profesa Malise Kaisi acha uzushi dhidi ya Mtume Muhammad 

Sensa ya majaribio: Wananchi watofautiana na serikali 
Na Rajab Rajab - Morogoro 

Uislamu ulivyoingia Zanzibar -3 

Mwembechai wageuka Hame, Bado walindwa na polisi 
Na Badru Kimwaga 

Waislamu Moro waendelea kusaidia wagonjwa 
Na Rajab Rajab - Morogoro 

Mjadala wa Katiba ya Shirikisho kuzinduliwa Dar Jumapili 
Na Mohamed Othman 

Walimu wa dini Tanga wapokea Baiskeli 
Na Abu Said 

Mafundisho ya Quran 
Kutoa katika njia ya Allah: Al-Baqarah aya  264 

Barua za wasomaji 

Masomo ya dini ya Kiislam 

Chakula na Lishe 
Vitu vinavyoweza kuwemo katika vyakula 

  

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtz.org
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita