AN-NUUR 
Na.171 Jamadul Akhir 1419, Oktoba 16 - 22, 1998 
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita
 
 
TAHARIRI: 

Serikali iwahurumie wananchi wake 

  
NI MASAA 336 usiku na mchana wananchi wa Nzasa wake kwa waume, watoto kwa vikongwe, walio wazima na wagonjwa wapo nje, jua lao na baridi ya usiku sawiya. 

Awali, walikuwa chini ya miembe angalau wakipoa jua la mchana,wakisubiri kupigwa baridi ya usiku maana hata shuka hawana baada ya kuunguzwa pamoja na nyumba zao, lakini sasa hata kwenye kivuli cha miembe wamefukuzwa wapo ‘jangwani’. 

Serikali imedai kwamba watu hawa waliochomewa nyumba ni wavamizi wa msitu na hivyo wanafukuzwa. 

Lakini wananchi hawa wanasisitiza kwamba wao hawana tatizo na suala la kuhifadhi msitu, wala kuwahamisha kwa nguvu waliovamia kama wapo. Wao wanasema hawajavamia msitu na eneo lao lipo mbali sana na mpaka wenyewe wa msitu. 

Lau serikali inadai kwamba wao wamo ndani, basi ziletwe ramani za eneo hilo pamoja na msitu wenyewe, watalaamu waonyeshe mipaka ya msitu ulipokomea. 

Katika baadhi ya matamshi ya viongozi wa serikali, imeelezwa kwamba zilizochomwa moto si nyumba bali vibanda vya muda vya wachoma mkaa, wapasua mbao na wakulima. Yawezekana kulikuwa na vibanda vya aina hiyo katika jumla ya nyumba zilizochomwa. 

Lakini tutasema nini juu ya wananchi ambao kwa siku 14 wapo nje wakishinda juani na kulala chini wakipigwa na baridi usiku kucha huku wakiwa hawana chakula cha uhakika. Haiwezi kuwa wananchi hawa kwamba walichomewa ni kibanda cha kuamia ndege. Ingekuwa hivyo wangesharudi makwao. Kubaki kwao hapo siku zote hizi ni kwamba hawana pa kwenda. 

Watakwenda wapi wakati hapo ndio kwao ? Hayo ndiyo makazi na mashamba waliyorithishwa na babu zao ! Waende wapi wakati sehemu zote zinazowazunguka ni makazi na mashamba ya watu wengine ! 

Yawezekana serikali ikawa imeona kwamba eneo hilo ni muhimu liwe sehemu ya hifadhi, au hata kama toka awali lilikuwa hivyo. Lakini angalau basi ubinadamu ufanyike katika kuweka mradi mwingine utakaoiongezea serikali mapato. Izingatiwe kwamba japo hawa wanaoondolewa hawana uwezo sawa na na muhisani mhifadhi mazingira, lakini ni binadamu hawa sawa na wale wanaodai kwamba nyumba zao ni "viota" vya ndege. Wana roho sawa na binadamu wengine na hawana manyoya ya kuwakinga na jua au baridi. 

Serikali ina maguvu ya kufanya operesheni yoyote itakayo lakini na iwaonee huruma wananchi hawa. 

Hata kama wanaharibu msitu, tusiongeze janga kwa kuwaua kwa njaa, baridi na jua. 

Hawa hawahitaji ramani wala mhandisi, waonyeshwe eneo watapigilia fito na kuzungusha nyasi, waishi na watoto wao. Lakini kabla viazi havijachipua watakavyopanda katika maeneo hayo mapya waruhusiwe kuvuna mihogo yao. 

Hii ikiwa ni wiki ya kupunguza majanga kama azimio la Umoja wa Mataifa linavyosema, tuanze na Nzasa. 

Mpaka serikali itakapotoa ushahidi wake ukawawekwa kwenye mizani wananchi hawa wana haki ya kulipwa fidia kama sheria ya Misitu (Cap. 389 K.f. 6(1) ( c ) inavyoelekeza lau imeona eneo lao la Nzasa linafaa kuwa Msitu. 

 
Juu 
 

YALIYOMO 
 
 
TAHARIRI 
Serikali iwahurumie wananchi wake 

KUCHOMWA MOTO NYUMBA ZA WANANCHI: Nzasa wamtaka Mkapa awaonyeshe pa kwenda 
Na Mwandishi Wetu, Nzasa 

Mishikaki ya nguruwe Moshi yachomwa mbele ya Msikiti 
Na Mwandishi Wetu 

MAONI YETU: 
Je; ni halali kuchoma Kidungu cha mtu? 

Upimaji huu mpya ni wa nini 
Na Mwandishi Wetu 

TANGAZO LA HIFADHI YA MSITU WA KAZIMZUMBWI 

Ndoa si lengo, ni wasila wa kufikia lengo 
Na Bi. Zuhura Tajiri, Shinyanga 
 
Teknologia:
Jifunze kuunganisha Kompyuta
Na Hassan Omar

Makala:
Nani atakayewahoji Waheshimiwa hawa

Goda Muslim School, Manzese
Na Mwandishi Wetu

Utabiri sahihi wa kuibuka kwa Uislamu
Na Sheikh Bernard P. Nyangasa

Historia ya mgogoro wa Nzasa
Na Mwandishi Wetu

DUMT watoa msaada kwa walioathirika Nzasa
Na Mwandishi Wetu

UCHOMAJI NYUMBA NZASA: Wafadhili wana mchango gani?
Na Mwandishi Wetu

Mafundisho ya Quran 
Kutoa pasipo masimango 

Barua za wasomaji 

Masomo ya dini ya Kiislam 

Chakula na Lishe  

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtz.org
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita