AN-NUUR 
Na.172 Rajab 1419, Oktoba 23 - 29, 1998 
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita
 
 
Fitna ya Bakwata   

IMEELEZWA kwamba Ijumaa Oktoba 16, askari Polisi wapatao kumi na nne waliovaa sare waliuzingira msikiti mkuu wa Ijumaa mjini Same kwa kile kilichodaiwa kutuliza fujo na kulinda amani. 

Pamoja nao walikuwepo askari wengine wanne wasio na sare pamoja na mkuu wa Kituo, Bw. Shomari ambao waliswali pamoja na waumini. 

Waumini ambao walifurika katika msikiti huo tayari kwa swala ya Ijumaa walishangaa kuona askari wakiwasili katika eneo hilo na kujibana katika sehemu tofauti tofauti. 

Pamoja na hali hiyo Ibada iliendelea kama kawaida na hatimaye Polisi hao kutawanyika bila kusema wala kufanya lolote. 

Uchunguzi wa gazeti hili umebaini kwamba askari hao walifika msikitini hapo kutokana na taarifa waliyopelekewa na Ofisi ya Bakwata kwamba pangetokea vurugu kutokana na maswala ya uchaguzi wa uongozi wa Msikiti. 

Uchunguzi zaidi umebaini kwamba mtu ambaye alijitaja kama Mwenyekiti wa Bakwata, Wilaya ya Same Oktoba 12, 1998 alimuandikia barua Mkuu wa Wilaya akidai kwamba kungekuwa na tukio la kuvunjika kwa amani ambalo lingesababishwa na baadhi ya waumini. 

Mwenyekiti huyo akiinakili barua hiyo No. BWS/ML/F.7/9/7 kwa Mkuu wa Polisi wa Wilaya alidai kwamba baadhi ya waumini walikuwa wamepanga kufanya uchaguzi wa msikiti kinyume cha katiba ya Bakwata. 

Kufuatia tukio hili la aina yake msikitini hapo, waumini wamekuwa na hisia na maoni tofuati. Hata hivyo takriban waumini wote walioongea na Mwandishi wa Habari hizi walisema kwamba kwa lolote ambalo lingetokea Polisi wasingekuwa wakulaumiwa kwani wao walikuwa wakitekeleza wajibu wao kwa mujibu wa taratibu zao za kazi. 

Kwa upande mwingine lawama kubwa imekuwa ikielekezwa kwa uongozi wa Bakwata kwa madai kwamba badala ya kujishughulisha na mambo ya kuwaletea maendeleo Waislamu pamoja na kujenga umoja na upendo miongoni mwao imekuwa ikiwafitinisha Waislamu na Serikali na kuleta faraka miongoni mwa Waislamu. 

Hata hivyo mama mmoja mtu mzima ambaye hakupenda jina lake litajwe gazetini, aliongea kwa uchungu akidai kwamba wa kulaumiwa ni Waislamu wa Same wenyewe na wala si viongozi wa Bakwata. 

Akifafanua mama huyo alisema, miaka nenda miaka rudi, Waislamu wamekuwa na viongozi ambao ni mahiri sana kwa farka na fitna, halikadhalika weledi wa kuvunja hata zile juhudi ndogo wanazofanya Waislamu kujiletea maendeleo. 

Mama huyo aliyeonekana kuwa na majonzi alidai kwamba toka miaka ya 1970s wamekuwa wakiletwa waalimu na masheikh ili kuwa maimamu na kuwasomesha waumini waijue dini yao, lakini hakuna anayedumu. 

Alidai kuwa wamekuwa wakijengewa fitna na kufukuzwa huku maendeleo waliyoyaanzisha yakiachwa yaporomoke. 

Alisema kwamba pamoja na kwamba ni wengi wameshafukuzwa kwa fitna za viongozi lakini yeye binafsi waliomgusa sana kufukuzwa kwao ni watatu. 

Amewataja Masheikh hao kwa majina ya Sheikh Ramadhani Saiboko, Ustadh Thabit Othman na Ustaadh Atwaa Abdallah. 

Akifafanua alisema kwamba hawa ni Masheikh ambao lau si kwa fitna za viongozi wangeleta maendeleo makubwa sana. 

Alipotakiwa kufafanua juu ya dai la fitna ya viongozi mama huyo alitoa mfano wa Ustadh Thabit Othman ambaye alidai kwamba alifukuzwa kwa madai kwamba si ‘Rijali". 

Akitoa maelezo zaidi alisema kwamba Ustadh Othman alikuwa ndiye Khatibu wa kwanza kusoma khutba ya Ijumaa kwa Kiswahili Msikitini kwao. Hata hivyo akadai kwamba siku moja wakastukia wanatangaziwa na kiongozi mmoja wa Bakwata ambaye alimtaja kwa jina la Mwedadi Kiluvia; kwamba Imamu huyo anafukuzwa kwa vile si rijali jambo ambalo halikuwa kweli. 

"Viongozi wa namna hiyo ndio hao hao viongozi wa Waislamu wa Same toka miaka hiyo ya 1970 hadi leo. Sasa wa kulaumiwa nani kama sio Waislamu wenyewe wanaowafuga"; alihoji mama huyo kwa uchungu. 

Utafiti wa gazeti hili umebaini kwamba kwa vile Ustadh Thabit alikuwa hajaoa na kwa mujibu wa Uislamu alikuwa ametulizana.; baadhi ya viongozi wa Bakwata walimjengea dhana kwamba ana upungufu. 

Utafiti zaidi umebaini kwamba alipewa pesa msichana mmoja, Muuza Bar, ili amtie mtihanini Ustadh huyo. Alichofanya binti huyo ni kuingia ndani ya chumba cha Ustadh bila hodi na kufanya vitimbwi ambavyo vilimfanya Ustadh akikimbie chumba amwache binti huyo ndani. 

Binti huyo ambaye imeelezwa bado anaishi mjini Same akiwa mtu mzima na heshima zake sasa aliporejesha salamu kwa waliomtuma, ndipo likatolewa tangazo mbele ya mkutano wa Waislamu kwamba anafukuzwa kwa vile sio rijali. 

 Katika kulifuatilia suala hili AN-NUUR ilifahamishwa kwamba Ustadh Thabit alijieleza kwa baadhi ya wazee kwamba yeye hajaoa kwavile masikini na yatima hivyo anafunga mara kwa mara kama Mtume (s.a.w.) alivyoagiza akisubiri Mwenyezi Mungu amjaalie cha kuolea. 

AN-NUUR imefahamishwa kwamba Mzee Ali Mshanga (marehemu sasa) alijitolea kumlipia mahari pamoja na gharama nyingine, akaoe. 

Kwa shani yake Allah imeelezwa kwamba mtoto aliyezaliwa akawa nakala halisi (photocopy) ya Ustadh Thabit jambo lililowafedhehesha sana viongozi wa Bakwata waliomfukuza uimamu. 

Nikutokana na maelezo haya mama huyo aliyeomba asitiriwe jina lake anasema kwamba wakulaumiwa si viongozi wenye fitna bali Waislamu wanaowafuga toka zama hizo mpaka leo. 

Kuhusiana na tukio hili la askari kuuzingira msikiti AN-NUUR iliwasiliana kwa simu na ofisi ya Kamanda wa Polisi mjini Same, hata hivyo msemaji ambaye hakutaja jina lake wala cheo chake alisema kwamba habari hizi aulizwe R.P.C . mjini Moshi. Hata hivyo juhudi za kumpata R.P.C. kwa njia ya simu hazikuweza kufanikiwa. 

Kwa upande mwingine AN-NUUR imegundua kwamba chanzo cha mgogoro wa sasa ni Bakwata kutaka kuweka uongozi wa msikiti bila ya kufuata katiba yake yenyewe. 

Hata hivyo juhudi za kuwapata viongozi wa Bakwata Mkoani Kilimanjaro na Wilayani Same hazikuweza kufanikiwa hadi tunakwenda mitamboni. 
 

Juu 
 

YALIYOMO 
 
 

TAHARIRI 
Kuangukia makaa hakuna nafuu kwa aliye kikaangoni 

Wanawake Dodoma wataka mtoto aliyepigwa risasi akatibiwe nje 

Kesi za Mwembechai zaanza kusikilizwa 

Fitna ya Bakwata 

Dondoo za saikolojia: Tuonavyo mambo 

Waraka wa Baraza Kuu kuhusu Parole 

Inawezekana kufanyika mdahalo kati ya Waislamu na wasio Waislamu? 
Na Nandenga wa Mkomidachi 

Teknologia 
Jifunze Kuunganisha Kompyuta (2) 
Na Hassan Omar 

Serikali ihamie Dodoma kwanza ! 
Na. Said Rajab 

Mahafali ya AMSIR Iringa 
Na Mwandishi Wetu 

Madrasatul Nnajjary Islamiya 

Ijue Madrasatul Riyaadh 

Bihawana Sekondari wafungua Ijumaa 

Vijana Shinyanga watakiwa kuwa mfano mwema 
Na Jihad R. Saballa, Shinyanga 

Vyeo visiwasahaulishe majukumu yenu- Sheikh Abri 
Na Mwandishi Wetu, Iringa 

Jiandaeni na kifo – Sheikh Abdallah 
Na Mwandishi Wetu, Dodoma 

Semina zawazindua wanawake Bukoba 
Na Nadhiru Ishengoma 

Waislamu wanaomaliza Kidato cha Nne Tanga waaswa 
Na Ibn Mohamed 

Ndugu Kamuhabwa ndiye mwenye chuki na AN-NUUR 
Mwandishi: Maalim Bassalah 

'Ukombozi wa mwanamke si kugeuzwa biashara huria' 
Na Japhary Lemah, Arusha 

Polisi walinda amani katika muhadhara wa Wakristo 
Na Badru Kimwaga 

Mazengo wapewa uwanja wa kujenga Msikiti 
Na Mwandishi Wetu, Dodoma 

'Ajiengua Chuoni Z'bar kwa kutoruhusiwa kuvaa hijab' 
Na Seif Hamad Suleiman, Zanzibar 

Barua za wasomaji 

Masomo ya dini ya Kiislam 

Shairi 
Simlazimishe Yesu ukombozi wa ulimwengu (jibu) 

 

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtz.org
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita