|
|
| Mauaji
ya Mwembechai:
Spika wa Bunge aombwa
atoe gharama za kuunda Tume
Ombi hilo limetolewa na wanawake Waislamu katika kongamano lao lililofanyika mjini Bagamoyo mwishoni mwa wiki iliyopita. Bi. Fatma Lazaro akitoa salamu kwa mgeni rasmi Mbunge wa Bagamoyo Mh. Yusuf Ramia alisema kwamba suala la Mwembechai halitokwisha mpaka walioua wafikishwe mahakamani na Tume iundwe kuichunguza kadhia yote hiyo. Bi. Fatma Lazaro ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Wanawake wa Kiislamu alisema kwamba awali baadhi ya Wabunge walipodai kuundwa Tume ya uchunguzi Mh. Spika alidai kwamba hakuna fedha kwa ajili ya suala hilo. Kwa vile kuundwa Tume hiyo ni muhimu Bi. Fatma alimwomba Mh. Yusuf Juma Ramia afikishe salamu kwa Mh. Spika kwamba fedha isiwe tatizo wanawake Waislamu wapo tayari kuchanga. Mh. Ramia aliahidi kuzifikisha salamu hizo. Awali akifungua kongamano hilo, Mbunge wa Bagamoyo Mh. Ramia aliwahimiza wanawake Waislamu kushikamana na maadili ya Kiislamu na kuwalea watoto wao katika maadili mema. Aidha, alisisitiza kwamba umoja wa kweli ni silaha muhimu na kwamba ni lazima watu wajisafishe na wawe wacha Mungu ili waweze kupata nusura ya Mwenyezi Mungu. Pamoja na kurejewa maelezo ya tukio la Mwembechai ambayo yaliwafanya wanawake waangue vilio, mmoja wa wanawake waliodhalilishwa aliusimulia unyama waliofanyiwa na polisi pamoja na askari magereza. Alisema kwamba walivuliwa nguo zote na polisi wanaume na kupigwa sana; kurushwa kichura wakiwa uchi, kupekuliwa sehemu za siri na polisi wanaume na kulazimishwa kuimba nyimbo za Kikristo. Mama huyo (jina tunalihifadhi) ambaye alishindwa kuendelea kuzungumza baada ya ukumbi wote kurindima kwa vilio alichukua ahadi kwa Mola wake kwamba hatoacha kuutetea Uislamu mpaka mwisho wa uhai wake. Kwamba mateso yamekuwa kama motisha na tanuru la kumpa sifa muhimu za kuifanya kazi tukufu ya kuihami dini ya Allah. Mada mbalimbali zilitolewa ikiwemo: Hijab - mtoaji akiwa Mwaka bint Hamis kutoka Bagamoyo ambaye alikemea tabia ya kwenda uchi na kuunganisha nywele. Elimu: mtoaji akiwa Katibu wa Kamati ya Akinamama Taifa, Bi. Fatma Juma ambaye alieleza umuhimu wa elimu katika maisha ya kila siku. Vita vya fikra: mada hii ilitolewa na Fatma Mdidi aliyeelezea aina ya vita wanavyopigwa Waislamu na kisha kueleza kwa ufasaha vita vya fikra kwamba vilianza muda mwingi ili kuharibu fikra za Waislamu wawe na mtazamo wa fikra za kikafiri, wabaki Waislamu jina. Akifafanua alisema kwamba leo hii magazeti yote yanabeba fikra za kimagharibi, bila ya Waislamu kuwa na fikra za Kiislamu katika kila wanachosikia au kukiona bila shaka wataelekea pabaya. Shairi linalowataka Waislamu waache kuipigia kura CCM mwaka 2000 lilitolewa na Fauzia Mdogo. Utenzi wa mauaji ya Mwembechai: Ulitolewa na binti mmoja mdogo Fatma Rashid maarufu kwa Fatma Mdogo ambaye ni mwanafunzi wa darasa la akina wa Kiislamu Kariakoo Dar es Salaam. Utenzi uligusia kila kipengele katika tukio zima la Mwembechai kiasi kwamba wengi walitokwa na machozi, hasa alipogusia kufa akina Mzee Chata na vipi wanaume wampekue mwanamke. Jihad: Ni mada iliyotolewa na Mwenyekiti wa Idara ya Uhamasishaji ya Kamati ya Akinamama Taifa, aliwaeleza akinamama kuwa wakati umefika wa kuchukua haki yao, wasiwangoje wanaume ambao mpaka sasa bado wamelala fofofo wanaogopa watu badala ya kumwogopa Allah. Jihadi ikipotea ndio kupotea Uislamu alisema. Mwisho wa kongamano yalipitishwa maazimio kadhaa ikiwa ni pamoja na kudumisha umoja na kuanzisha miradi ya elimu. Kulaani mauaji ya Mwembechai na dhulma dhidi ya Waislamu kwa ujumla. Aidha, serikali imetakiwa ifanye uadilifu katika uwiano wa kimaendeleo katika maeneo mbalimbali. Kongamano hilo lilitoa wito juhudi zifanyike kumtibu mtoto Chuki Athumani nje ya nchi ili arejee katika hali yake ya awali. Wakati huo huo, Mbunge wa Kibaha Mh. Dk. Ibrahim Msabaha ameomba kukutana na Kamati ya Wanawake wa Kiislamu. Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa Kamati hiyo Bi Fatma Lazaro, Mh. Msabaha aliwasilisha ombi hilo kufuatia mwaliko wa kamati hiyo kwa wabunge wa mkoa wa Pwani kuhudhuria kongamano ambalo lilifanyika wiki iliyopita mjini Bagamoyo. Bi. Fatma amesema kamati yake ingeitikia ombi la Mbunge huyo mara baada ya kongamano lao litakalofanyika Sinza Jijini Dar es Salaam. |
YALIYOMO
Tahariri Umaskini unachafua mazingira! Mauaji ya Mwembechai: Spika wa Bunge aombwa atoe gharama za kuunda Tume UN yaidhinisha udhalimu wa Marekani Qur’an yachomwa moto Shinyanga Marekani yadhihirisha Ubeberu wake MARADHI
YA KISAIKOLOJIA: SEXUAL SADISM
Kitengo cha Zaka chazinduliwa Dar Tume ya Jiji kubomoa Msikiti wa vipofu Akheri ya
zamani
UWAWARU yaleta nusura Ikwiriri Tamko la Masjid NNUUR juu ya kuanzishwa kwa UWAWARU Wasomi
Waislamu wawajibike
Madrasa Akhlaqil Islamiya yapiga hatua MADRASATUL
Husseiniyi Shadhily
Changieni vyombo vya mihadhara - Sheikh Said Misikiti yakosa maji ya kutawadhia Bakwata Tanga haifuati katiba yake Sheikh Mbukuzi ataka Waislamu watafute radhi za Allah Je,
hivi tuendelee kushika amri za Mungu tena? - 3
Njia
ya uzimani ni nyembamba, waionao ni wachache - 3
Sheikh Omar Bashir afikishwa mahakamani Mufti pekee kuidhinisha watu kufunga Nguruwe wanaofugwa maeneo wanayoishi watu kusababisha magonjwa ya kuambikiza Sayansi
na Teknolojia
Chakula
na lishe
|