AN-NUUR 
Na.180 Shaaban 28 - Ramadhan 1419, Desemba 18 - 24, 1998 
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita
 
Historia: Form IV
 
Upinzani dhidi ya Serikali ya Kiislamu wakati wa Khalifa wa Kwanza 
 
 

Uchokozi wa Warumi 

Sehemu ya kaskazini ya Bara Arabu ilipakana na Dola ya Warumi wakati huo ilikuwa ikiitwa Dola ya Byzantine ambayo majimbo yaliyokuwa chini ya himaya yake ni Syria, Palestina na Misri. Jimbo la Syria ndilo hasa lililopakana na Bara Arab. 

Uchokozi wa wakristu wa Kirumi dhidi ya Dola ya Kiislamu ulianza tangu mwaka wa sita wa Dola ya Kiislamu wakati wa Mtume Muhammad (s.a.w.). Uchokozi wa Warumi kama tulivyoueleza katika Sura hii maudhui ya kidato cha tatu; ulifanya mambo matatu. Waliwaua Wajumbe wote kumi na tano waliotembelea makabila na koo zilizokuwa zinakaa kaskazini mwa Syria, ila kiongozi wa msafara Kaaba bin Umair Ghifari aliyeweza kuwatoroka na kurudi Madina na kutoa taarifa hii ya kusikitisha kwa Mtume (s.a.w.). Jambo la pili vile vile ni la mauaji ya Harith bin Umair. Mauaji haya yalifanywa na Shurahbil bin Amr gavana wa Kikristu wa Busra. Mjumbe huyu, (Harith bin Umair) alitumwa kwake na Mtume (s.a.w.). Tukio la tatu ni kuuliwa kwa Farah bin Amral Juzami kamanda wa majeshi ya Kiarabu ya Warumi. Kamanda huyu alisilimu; Caesar aliposikia aliamuru akamatwe. Alipofikishwa kwake alimwambia Aritadi na abaki na kazi yake au abaki Muislamu na afe.61 kuliko kuwa kafiri Farah bin Amral Juzami alikhiari kifo. uchokozi huu ndio uliopelekea vita vya Mutah na msafara wa Tabuk ambao ulikuwa chini ya uongozi wa Mtume Mwenyewe. Katika msafara wa Tabuk adui hakujitokeza. Lakini baada ya msafara huu wa Mtume (s.a.w.) chokochoko zilianza tena kabla ya Mtume hajatawafu aliandaa jeshi ili likabiliane na hali ya mpakani, pamoja na kulipiza kisasi vita vya mutah chini ya uongozi wa Usamah bin Zaid. Jeshi hili lilipokuwa katika maandalizi Mtume akatawafu na safari iliahirishwa. Baada ya majuma matatu hivi tangu kuzikwa Mtume Khalifa Abubakr aliliamuru jeshi hili kukamilisha ujumbe wake. Hivyo likaenda na baada ya siku 40 Usamah alirudi na ushindi mkubwa. Baada ya ushindi Caesar hakuridhika hivyo aliendelea na chokochoko na hasa baada ya ushindi wa Waislamu uajemi, Caesar alistushwa zaidi na akaona vyema aikabili nguvu ya Uislamu. Hivyo aliyavamia majeshi ya mpakani ya Waislamu. Mwanzoni Waislamu walishinda lakini walipoingia Transjordan walishindwa. Kamanda na msaidizi wake waliuawa na wakaliacha jeshi chini ya uongozi wa Ikrimah bin Abu Jahl .62 Habari zilipomfikia Khalifa akaita shura yake na wakakubaliana kutangaza Jihad dhidi ya Dola ya Kikristu ya Warumi .63 Khalifa aliwahamasisha Waislamu kwa kuwaandikia barua. Moja ya barua hizo ni kama ifuatayo: 

Kutoka kwa Khalifa wa Mtume (s.a.w.) kwenda kwa Waislamu wote wanawake na wanaume wa Yemen. Nawasalimia wote wanaosomewa barua hii. Namshukuru Mwenyezi Mungu anapaswa kuabudiwa. Mwenyezi Mungu ameifaradhisha Jihad na kuwaamuru waitekeleze wakiwa katika hali nzuri au hali ngumu, wanatakiwa wajitokeze kwenda katika jihad kwa mali zao na nafsi zao. jihad ni wajibu na malipo yake ni makubwa. Nawasihi Waislamu mjitokeze kwenda kwenye Jihad dhidi ya Warumi wa Syria. Enyi waja wa Mwenyezi Mungu; shirikini katika Jihad kwa Ikhilaswi. Hamtakosa moja ya zawadi hizi, ama kufa shahidi au ushindi na ngawira..64 

Waislamu walihamasika na kujitokeza kwa wingi. Jeshi la kutoka Madina lilikuwa na Waislamu kati ya ishirini na saba elfu 7 na thelathini elfu 8 Jeshi hili kama mbinu ya kivita ligawanywa katika bataliani nne na kila bataliani ikawa chini ya kamanda mzoefu na kila kamanda alielekea upande wake. Kutoka Madina Abu Ubaidah bin al-Jarrah alikwenda hems. Amr bin al-As alikwenda Palestine, Yazid bin Sufian alikwenda Damascus na Shurahbel bin Hasnah alikwenda Jordan.65 Makamanda hawa walipigana katika maeneo waliyokwenda kila mtu peke yake. Lakini adui aliyekuwa na jeshi lenye zana zote za lazima kwa vita kwa wakati ule lenye askari laki mbili na nusu aliamua kupiga bataliani moja hadi nyingine akianzia Bataliani ya Amri bin Al-As ambayo ilikuwa imezingirwa Khalifa Abubakr alipofahamu mpango huu, aliamuru bataliani zote ziungane na kupigana pamoja. Vile vile alimuagiza Khalid kutoka Uajemi upesi aende Syria kwenye uwanja wa vita. 

Khalid kama tulivyokwisha muelezea ni Jemadari hodari. Katika muda wa siku kumi na tano tangu atoke Syria alishinda ngome za Warumi zilizokuwa Suwa na Tadmur. Kabla habari hazijaenea za kuwepo kwake Syria tayari alikuwa Damascus. Mwanzoni Warumi waliwatumia wasaidizi wao wa Kiarabu kabila la Ghassan ambalo lilishindwa vibaya na Khalid katika mapigano yaliyofanyika Marja Rahit maili 15 kutoka Damacus. Wakati Warumi wanarudi kuilinda Damascus na kutafuta Khalid upande wa kaskazini, Khalid alibadili njia akapitia Quraqir na kwa kustukizia akaiteka Busra na kuungana na makamanda wenzie Palastine ambako majeshi ya Amr al-As yalizingirwa. Jeshi kubwa la adui lilidhamiria kuwafukuza Waislamu katika nchi yao; lakini makafiri kamwe hawatamshinda Mwenyezi Mungu hata wakiwa wengi kiasi gani. Kahalid akiongoza bataliani zote aliwashinda Warumi katika vita vya Ajnadayn Julai na Agosti 634 Jamadil-Awal 12 A.H. na Januari 635 katika vita vya Fahl. Taarifa ya ushindi wa vita vya Ajnaday ilimkuta Khalifa Abubakr katika kitanda cha mauti, alishikwa na homa na katika muda wa majuma mawili akafariki tarehe 23 Augosti 634 A.D. sawa na 22 Jamadal-Akhira 13 A.H. akiwa na umri wa miaka 61. 66 
 
 

Juu 
 

YALIYOMO 
 

Tahariri
Umaskini unachafua mazingira!

Mauaji ya Mwembechai: Spika wa Bunge aombwa atoe gharama za kuunda Tume

UWAWARU yafa Rufiji

UN yaidhinisha udhalimu wa Marekani

Qur’an yachomwa moto Shinyanga

Marekani yadhihirisha Ubeberu wake

MARADHI YA KISAIKOLOJIA: SEXUAL SADISM
Na. Abu Halima Sachangwa

Kitengo cha Zaka chazinduliwa Dar

Tume ya Jiji kubomoa Msikiti wa vipofu

Akheri ya zamani
Na Alhaj Yusuf Kalala, Washington DC. USA

UWAWARU yaleta nusura Ikwiriri

Tamko la Masjid NNUUR juu ya kuanzishwa kwa UWAWARU

Kuanzishwa kwa UWAWARU

Wasomi Waislamu wawajibike
Na Mwandishi Wetu

Albucasis  936 - 1013 (CE)

Ijue Uhuru madrasa - Morogoro

Madrasa Akhlaqil Islamiya yapiga hatua

MADRASATUL Husseiniyi Shadhily
Na Jamillah Nassoro
 
Hatimaye kesi ya kushambulia kituo nayo yafutwa

Changieni vyombo vya mihadhara - Sheikh Said

Misikiti yakosa maji ya kutawadhia

Bakwata Tanga haifuati katiba yake

Sheikh Mbukuzi ataka Waislamu watafute radhi za Allah

Je, hivi tuendelee kushika amri za Mungu tena? - 3
Na Mwinjilisti Bunga E. Dettu

Njia ya uzimani ni nyembamba,  waionao ni wachache - 3
Na Yasin Valerian Massawe

Sheikh Omar Bashir afikishwa mahakamani

Mufti pekee kuidhinisha watu kufunga

Nguruwe wanaofugwa maeneo wanayoishi watu kusababisha magonjwa ya kuambikiza

200 wamesilimu

Sayansi na Teknolojia 
[Kuiweka Modem kwenye Kompyuta] 
 
Masomo ya Dini ya Kiislamu 

Barua za Wasomaji 

Mashairi 

Chakula na lishe 
[Mlo wa Daku] 
 
Tangazo 
New Book: The untold story of the Muslim struggle against British Colonialism in Tanganyika. 
 

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtz.org
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita