AN-NUUR 
Na.181 Ramadhan 1419, Desemba 25 - 31, 1998 
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita
 
Tahariri

Hakuna Idd kwa wanafunzi Waislamu mwaka huu 

KUFUATIA kutolewa tarehe za kufanya mitihani ya kidato cha nne, wanafunzi Waislamu sasa watalazimika kuifanya mitihani hiyo ndani ya funga ya Ramadhani. Si vigumu kuelewa hali atakayokuwa nayo mwanafunzi huyu aliyefunga atakapoukabili mtihani unaoanza saa nane mchana. 

Jingine lililozaliwa na ratiba hiyo mpya ni kwamba huenda wanafunzi hao wakalazimika kuikosa swala ya Idd el Fitr. Kwa mujibu wa kanuni za Baraza la Mitihani itabidi wanafunzi hao waamue: Ama wakose mtihani au swala. Hawawezi kupata yote mawili japo ni haki yao. 

Yawezekana kabisa kwamba hapakuwa na uwezekano ama wa kuisogeza mbele au kuirejesha nyuma ratiba hii ili isigongane na funga pamoja na sikukuu ya Idd. 

Lakini yawezekana pia ratiba hii ikawa ni kielelezo cha hali halisi ya jamii yetu inayodaiwa kutokuwa na udini wala kuongozwa kwa kuelemea upande wa dini fulani. 

Ratiba ya mitihani inaanza Jumatano ya Januari 13, 1999. Kwanini isianze Jumatatu ya Januari 11? 

Januari 12 ni sikukuu ya Mapinduzi ya Zanzibar na lau mitihani ingeanza Januari 11, wanafunzi wangelazimika kufanya mitihani siku ya sherehe za Mapinduzi. 

Yawezekana zilikuwepo sababu nyingine, lakini tunadhani mazingatio ya kuwepo siku ya mapinduzi ikichangiwa na uwakilishi wa watu wanaoitukuza siku ya mapinduzi ya Zanzibar ndani ya Baraza la Mitihani na Wizara husika kumechangia uamuzi wa ratiba kuanza Januari 13 badala ya 11. 

Kwa mantiki hiyo hiyo isingewezekana kabisa ratiba hiyo kuanza kabla ya Desemba 25, kwani wapo wanafunzi ambao wangelazimika kufanya mitihani siku ya Krismasi. 

Taarifa zisizo rasmi zinaeleza kwamba hivi karibuni ndani ya Mwezi wa Ramadhani litafanyika tamasha kubwa la kusherehekea mafanikio ya Tume ya Jiji. 

Tamasha hilo ni wazi litasheheni ngoma na kila aina ya vurugu zisizokubalika hasa kwa mwezi huu wa Ramadhani. 

Uwakilishi wa Waislamu katika Tume hiyo nyeti katika ngazi za juu ni sawa na sifuri. Na hapana shaka ndio maana tamasha hilo limepangawa ndani ya Ramadhani. 

Haihitaji mtu kuwa razini sana kuelewa kwamba uwakilishi wa Wakristo ndani ya serikali na taasisi zake usingeruhusu mtihani ufanyike siku ya Krismasi au Pasaka. 

Kinyume chake ni hivyo hivyo. Wanafunzi Waislamu watalazimika kufanya mtihani siku ya Idd. Wafanyakazi watapangiwa ratiba za vikao zisizozingatia swala ya Ijumaa wala mipaka ya kula na kunywa. Ndani ya fikra za wapangaji haiwapitikii kwamba wapo Waislamu. Pale ambapo wapo Waislamu miongoni mwa wapangaji huonekana kama waliopotea njia wakaingia wasikohitajika kutokana na upogo uliopo katika uwiano. 

Itakuwa ni kuwalaghai Waislamu kama Serikali yetu itaendelea kutuambia kwamba inajenga umoja wa kitaifa usio na udini ikiwa haioni kuwa ni tatizo watu wa dini moja au wa hata dhehebu moja kuhodhi serikali na taasisi zake muhimu. 

Kwa upande wa Waislamu watakuwa wanafanya kosa kubwa na hasa kujikaanga wenyewe kama hawatapigania uwakilishi wao kila mahali na wakabakia kulewa propaganda za wanasiasa. 
 
 

Juu 
 

YALIYOMO 
 
 
Tahariri 
Hakuna Idd kwa wanafunzi Waislamu mwaka huu 

Baada ya wanafunzi Wakristo kusherehekea Krismasi: Wanafunzi Waislamu kuikosa  Id el Fitr 

Hoi hoi zatawala ziara ya Mwinyi Mwanza 

Waislamu Tunduma waswali ndani ya kilabu cha ulanzi  

MARADHI YA KISAIKOLOJIA: FROTTEURISM 

Barabara za Tabora zimepitwa na wakati 

Jicho la Uzalendo: Nihiari yetu kuendelea kujidanganya! 
Na Sompo wa Kahambwe 

Kuanza na kwisha mwezi wa Ramadhani 

Taarifa ya Kamati  juu ya yaliyotokea Mwembechai 

Hotuba ya Mwenyekiti wa Wanawake wa Kiislamu katika Kongamano lililofanyika Masjid Nnuur Sinza  19/12/1998 

Maazimio ya kongamano la wanawake wa Kiislamu 

Waislamu kijijini Kidunda Moro wahitaji mwalimu 

Waislamu Mtwara wadai jengo la Wakfu kwa CCM 

Wakati Makanisa yakimeremeta: Msikiti wageuka gofu Sanya Juu 

Sheikh Khalifa Suleiman afariki dunia 

Sheikh wa wilaya ya Lushoto afariki 

Ijue Madrasat Riyaadhwa ya mjini Dodoma 

Somo la Zaka 

Maiti ya Muislamu yasusiwa 

Mwinyi apongeza juhudi za kulea yatima Mwanza 

Tuhuma za kupindua uongozi wa Bakwata: Sheikh Hamim Boza akanusha kuhusika 

Kuongezeka kwa ajali za barabarani 

Njia ya uzimani ni nyembamba,  waionao ni wachache - 4 
Na Yasin Valerian Massawe 

Matajiri wahimizwa kutoa zaka 

Saggaf awataka watoto wahifadhi Qur'an 

Waislamu watakiwa kujitolea kupigania dini yao 

Kesi  nyingine Mwembechai yaahirishwa  

Sayansi na Teknolojia  
[Kuirekebisha Modem Yako]  

Masomo ya Dini ya Kiislamu  

Barua za Wasomaji  

Mashairi  

Chakula na lishe  
[Saumu na lishe ya mama mjamzito] 
 

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtz.org
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita