|
|
| Hotuba
ya Mwenyekiti wa Wanawake wa Kiislamu katika Kongamano lililofanyika Masjid
Nnuur Sinza 19/12/1998
Ndugu zangu katika Uislamu, Wanawake wa Kiislamu Assalam Alaykum warahmatullahi Wabarakatuh Tukio hili la siku ya leo linahitimisha mfululizo wa matukio kadhaa ya kihistoria yaliyotokea mwaka huu kwa upande wa Wanawake wa Kiislamu. Kumbukumbu zangu haziniambii ni mwaka gani au lini kabla ya mwaka huu Kina mama wa kiislamu walifikwa na yale yaliyowafika au kukutana kama walivyokutana mara kadhaa katika mwaka huu. Na vile vile sikumbuki ambalo lilijenga mshikamano kama hili la wanawake kushikamana mkoa kwa mkoa. Kushikamana kiasi hiki kunatosha kuthibitisha kuwa tukio la Mwembechai si la watu wachache. Asije akatokea mtu tena kusema eti sisi hatuna mshikamano. Huyo atakuwa mwongo na mzushi hivyo mwogopeni. Hali iliyojitokeza hapa Dar es Salaam ndiyo iliyojitokeza mikoani. Huu ni ushahidi tosha wa mshikamano wetu. Haya ni matunda ya zile propaganda za uzushi. Baada ya watu kujua ukweli wametoka na kuonyesha utukufu wa dini yao.(Alhamdulillah) Mnakumbuka zilipita propaganda kwamba sisi ni wakorofi. Sidhani kama yupo sasa atakayesema tena hivyo. Haya maazimio yaliyosemwa hapa ndio ya Wanawake nchi nzima. Labda moja wajue kwamba baada ya madhalilisho pale msikitini, Segerea na Keko pamezaliwa mashujaa, na huu ndio muujiza wa Uislamu, na huu ndio utukufu wa Uislamu na hii ndio kawaida ya Uislamu, choko choko ya makafiri hufanya waislamu wawe wamoja zaidi na huwapa ujasiri wa kuipigania na kuifia dini yao. Miaka 1400 iliyopita siku ndani ya mwezi wa Ramadhani baada ya Waislamu kuhama Makka kwenda Madina kuishi kiislamu na kueneza Taa ya Allah(s.w), Makafiri wakajidanganya kufikiri kwamba eti Waislamu wale ni wachache, Maskini, hawana silaha hivyo waliamua kuwashambulia lakini walishindwa. Waislamu walijua kwamba uadui uliopo baina yao na makafiri ni tofauti ya Imani. walikwenda kupambana na makafiri wale bila kujali umaskini wao, uchache wao, uduni wa silaha zao wakitegemea msaada wa Allah (s.w). Mapambano yale yakawa ndio sababu ya Uislamu kuenea ulimwengu mzima. Hii ndiyo kanuni ya Allah (s.w) kutoa ushindi kwa waislamu hata kama makafiri watachukia. Allah (s.w) amesema katika Qur-an sura (9:33): "Yeye ndiye aliyemtuma Mtume kwa uongofu na kuwa Dini ya Haki ili kuifanya ishinde Dini zote ijapokuwa washirikina watachukia". Historia imeshaweka kumbukumbu zake kuwa chokochoko ndio chemchem ya Uislamu. Chanzo cha chokochoko iliyopelekea yaliyotokea Mwembechai ni mihadhara yenye kueneza Dini ya Allah (s.w). Sidhani kama wale walioanzisha hili walijua lingekuwa sababu ya kuamka waislamu, sidhani kama wale walioanzisha hili walijua kama watazalisha vijana wa Kiislamu ambao wangesimama kukabiliana na askari waliokuwa na silaha za moto pale bara bara ya morogoro. Sidhani kama walitegemea kwamba Akina Mama wanaovaa Hijabu na wasiovaa wangesimama imara kuwapa vijana wao taulo za kufutia athari za mabomu. Nina hakika hawakutegemea kuwa wangekuwepo wenye magari ambao wangesimasha magari ya ili kutoa tairi za spea zichomwe moto kuyeyusha sumu ya mabomu. Sidhani kama bado wako watu wanaodhani kuwa Nuru ya Uislamu itazimwa kwa vinywa vyao na mitutu yao. Kama wapo kumbukumbu zao hazifanyi kazi. Mimi nitawakumbusha: Waliwavamia waislamu kwa vitisho na vitimbi vikubwa siku ya Alhamisii jioni 12/2/98 kuashiria ubaya waliokusudia. Wakakamata watu wakawapiga waliowapata wakitegemea vishindo na vitimbi vyao vingefanikiwa lakini wakati wa swala ya magharibi ilipotimia waislamu walizidi kuongezeka pale msikitini kwa wingi bila kutegemea kama ni watu wenye kuelewa wangefahamu hapo kuwa walioingia magharibi waliongezeka kwa wingi, hawakutoka bali waliwasubiri wenzao humo’ hawakukimbia kuuacha msikiti. Lakini bado madhalimu wale walidhani vitisho vyao ni dawa. Hivyo wakaja na vitimbi vya kuzunguka msikiti na kukata umeme na kuongeza jeshi la kuwatisha waislamu waliokuwa ndani ya msikiti. Inasikitisha waislamu wasiokuwa na silaha wake za watu, wazee na wagonjwa kwenda kuzingirwa na kufanyiwa uvamizi wa kijeshi, kufungiwa mlango na kulipuliwa na mabomu ya machozi yasiyo na idadi ndani ya msikiti. Msikiti ukavunjwa na watu wakapigwa na kupelekwa rumande, kumbe hawakujua madhalimu wale kwamba hii ni sababu tosha ya kuleta kichocheo kipya cha Uislamu. Wakati wanapongezana hawakujua kwamba wangelitokea watu kwa maelfu siku iliyofuata, kufagia msikiti wao kuchangishana fedha za kununulia dizeli kwa ajili ya Generata, hawakukujua wangetokea watu watakaoendesha swala ya Aljumaa na kupeana taarifa ya yale yaliyotokea.Walitegemea swala ya Aljumaa isingekuwepo. Laiti wangelijua hayo wasingelianzisha. Hawakujua maparoko wale fitna waliyoleta ingeleta mshikamano tulionao leo hii. Laiti wangelijua wasingelianzisha. Hii ndiyo kawaida ya Uislamu. Na bila shaka baada ya kukiri kushindwa huko ndipo walipoamua bora waue ili kuwajaza khofu Waislamu. Hiyo pia haikusaidia. Siku iliyofuata haikuwa kwa waislamu wa Dar peke yao bali na mikoani walifurika Mwembechai kudai maiti ya ndugu yao wakazike. Kuona hivyo madhalimu wale wakazuia maiti kwa aibu. Wakaitoa siku ya Jumatatu kwa matarajio ya kupunguza mahudhurio, hiyo pia haikusaidia.Waislamu kwa maelfu kutoka pande zote; Mwenge, Mwembechai hadi Mwananyamala walifurika ili wamzike ndugu yao. Inachekesha baada ya yote hayo wanatokea wakuu wa maporoko wakisema kuwa Mwembechai ni ya wachache. Hii ndio kawaida ya madhalimu. Akina mama mnahitaji pongezi, malipo yenu yako kwa Allah (s.w). Nakupongezeni wanawake wa Kiislamu kwa kuwa mmeonyesha ushujaa, hamkumchelea mtu ila Allah (s.w). Na maazimio yameonyesha hilo. "Kuonewa sasa basi". Nami naongeza Azimio langu: hizi fitna na farka mnazofanyiwa zinasukwa toka nje makao makuu huko ulaya na kisha kupitia kwa wanaodanganywa kwa mitumba, peremende na pesa za misaada., ili wavuruge amani nchini sasa sisi tunasema hii ni nchi huru fitna na farka hizo zikome. Chuki za kidini zikome. Propaganda dhidi ya waislamu zikome. Wafahamu kwamba waislamu ni raia kama raia wengine nchini hapa. Wakijitia upofu na uziwi tutalazimika kusimama kidete kuondoa dhulma na kuikomboa nchi yetu kutoka kwenye makucha ya ukoloni mamboleo kama walivyolazimika wazee wetu kuondoa makucha ya ukoloni mkongwe. 1. Hijab ndio vazi la mwanamke wa Kiislamu. Ndio utambulisho wake. Hakuna mjadala kuanzia sasa. Wafanyakazi, kina mama wa majumbani na wanfunzi "Vazi la Hijab" ni amri ya Allah (s.w.) na hili tunasisitiza kuwa halina mjadala. 2. Suala la Mwembechai halitasahauliwa wala halitakwisha ni urithi wa kizazi hadi kizazi. Leo kina Chuki, (Shahidi) Swaleh Issa, Mzee Chatta n.k. ni kumbukumbu ya yale yaliyotokea pale Mwembechai. Damu ya Muislamu lazima ichipue katika nyoyo za watu. 3. Kwa kuwa suala la kuundwa Tume kuchunguza yaliyotokea Mwembechai limepuuzwa, wanawake tunaazimia kurudi kwenye Qur’an tuone Allah (s.w.) anasemaje juu ya aliyeua kwa dhulma tuelekezane la kufanya juu ya kadhia ya Mwembechai kwa mujibu wa Qur’an na Sunnah. 4. Kuelimishana juu ya Haki zetu ili tuweze kuzitumia: - Kuchagua viongozi waadilifu. - Kutetea haki zetu kwa mujibu wa Katiba. - Na tuishi kwa mujibu wa mafundisho ya Uislamu. Tunaazimia Kamati zetu za umoja ziendelee. Katika kila mkoa uwepo uongozi na uimarishwe ili uweze kushughulikia masuala yanayohusu jamii hasa wanwake Waislamu. Tujenge ushirikiano ili tuweze kufikia lengo la kumwendeleza mwanamke Muislamu katika maeneo yafuatayo: (i) Uchumi (ii) Siasa (iii) Afya (iv) Jamii kwa ujumla Kubwa tuwe na elimu ya uraia: - Uwepo utaratibu wa kuratibu shughuli zetu kijiji, kikata, kiwilaya, kimkoa hadi kitaifa. - Pawepo mahusiano ya kimkoa ya kubadilishana
uzoefu.
|
YALIYOMO
Tahariri Hakuna Idd kwa wanafunzi Waislamu mwaka huu Baada ya wanafunzi Wakristo kusherehekea Krismasi: Wanafunzi Waislamu kuikosa Id el Fitr Hoi hoi zatawala ziara ya Mwinyi Mwanza Waislamu Tunduma waswali ndani ya kilabu cha ulanzi MARADHI YA KISAIKOLOJIA: FROTTEURISM Barabara za Tabora zimepitwa na wakati Jicho la
Uzalendo: Nihiari yetu kuendelea kujidanganya!
Kuanza na kwisha mwezi wa Ramadhani Taarifa ya Kamati juu ya yaliyotokea Mwembechai Maazimio ya kongamano la wanawake wa Kiislamu Waislamu kijijini Kidunda Moro wahitaji mwalimu Waislamu Mtwara wadai jengo la Wakfu kwa CCM Wakati Makanisa yakimeremeta: Msikiti wageuka gofu Sanya Juu Sheikh Khalifa Suleiman afariki dunia Sheikh wa wilaya ya Lushoto afariki Ijue Madrasat Riyaadhwa ya mjini Dodoma Mwinyi apongeza juhudi za kulea yatima Mwanza Tuhuma za kupindua uongozi wa Bakwata: Sheikh Hamim Boza akanusha kuhusika Kuongezeka kwa ajali za barabarani Njia ya
uzimani ni nyembamba, waionao ni wachache - 4
Saggaf awataka watoto wahifadhi Qur'an Waislamu watakiwa kujitolea kupigania dini yao Kesi nyingine Mwembechai yaahirishwa Sayansi
na Teknolojia
Chakula
na lishe
|