|
|
|
Nihiari yetu kuendelea kujidanganya! Na Sompo wa Kahambwe MIGOGORO mingi hasa ya kisiasa inayojitokeza katika jamii, mara nyingi vyanzo vyake ni tabia ya utumiaji mbaya wa nyadhifa, sera potofu, upuuziaji wa masuala muhimu, kulindana na kupendeleana. Tukiangalia sehemu mbalimbali zenye migogoro duniani ambayo imelipua mapambano ya wenyewe kwa wenyewe, tunaona kwamba zilianza chokochoko za kidogo kidogo, wengi kulalamika kutotendewa haki, wachache kushutumu ukandamizaji wanaofanyiwa au utendaji mzima wa serikali inayo watawala kuwa mbovu. Lebanon, Bosnia, Kosovo, Kongo, Rwanda, Burundi n.k. ni matokeo ya fukuto za muda mrefu; kurushiana maneno, vijembe, kejeli na kutambiana. Vyombo vya habari vimekuwa vikiripoti matukio ya vita, mauaji na vifo vya maelifu ya watu wasio na hatia kutokana na migogoro katika sehemu hizo. Ufumbuzi huchukua muda mrefu inapofikia hatua ya mapambano ya silaha. Nchi yetu hivi sasa inapita katika mkondo wenye mawimbi ya migogoro mikubwa inayotishia usalama wa wananchi na raia wake. Ipo mikwaruzano ya kidini baina ya Waislamu na Wakristo na baina ya Waislamu na serikali. Upo mtafaruku wa kisiasa unaotokana na chama fulani kuendelea kung’ang’ania kuongoza bila kujali maoni na maamuzi ya wengi. Yapo pia madai ya utendaji usioridhisha wa viongozi wa serikali iliyo madarakani. Aidha uoni wa mambo huelezwa kuwatia wasiwasi wanaoongozwa. Na vilevile wapo waliokata tamaa kabisa ya kuishi chini ya mfumo huu wa utawala usiojua haki, uadilifu, maadili, haramu wala halali. Hizi ni fukuto zilizopo nchini hivi sasa ambazo huenda zikailipua nchi siku za usoni. Bahati nzuri sana wazalendo wengi wameanza kuliona hili mapema. Utafiti unaonyesha kwamba kada mbalimbali za wananchi zimekuwa zikijadili hatima ya nchi kadri serikali inavyoendelea kuparamia visiki, miti, magogo, mabonde na maporomoko. Wengi wana mawazo kwamba Tanzania chini ya serikali ya CCM itaendelea kujichimbia kaburi. Hoja kuu hapa ni kule kushindwa kwake kutatua migogoro kwa taratibu za muafaka, badala yake kuififisha kinamna. Ubabe, dharau na upuuzaji vimeshika hatamu za maamuzi. "Kutokujali yanayowakera wananchi ni maandalizi ya mabwawa ya damu za wahanga wa miongo ijayo", anasema mtaalamu mmoja wa mambo ya siasa. Watu wanaposema hili si zuri, lile linakwaza jitihada zetu au linapindukia taratibu zilizowekwa, hapana budi wasikilizwe, kukutana nao na kutafutia ufumbuzi kero yao badala ya kuendesha propaganda na vitisho. Inawezekana tukaendelea kujidanganya kwa mbinu hiyo lakini pia inawezekana tukaja hukumiwa na historia kwa uzezeta huo! |
YALIYOMO
Tahariri Hakuna Idd kwa wanafunzi Waislamu mwaka huu Baada ya wanafunzi Wakristo kusherehekea Krismasi: Wanafunzi Waislamu kuikosa Id el Fitr Hoi hoi zatawala ziara ya Mwinyi Mwanza Waislamu Tunduma waswali ndani ya kilabu cha ulanzi MARADHI YA KISAIKOLOJIA: FROTTEURISM Barabara za Tabora zimepitwa na wakati Jicho la
Uzalendo: Nihiari yetu kuendelea kujidanganya!
Kuanza na kwisha mwezi wa Ramadhani Taarifa ya Kamati juu ya yaliyotokea Mwembechai Maazimio ya kongamano la wanawake wa Kiislamu Waislamu kijijini Kidunda Moro wahitaji mwalimu Waislamu Mtwara wadai jengo la Wakfu kwa CCM Wakati Makanisa yakimeremeta: Msikiti wageuka gofu Sanya Juu Sheikh Khalifa Suleiman afariki dunia Sheikh wa wilaya ya Lushoto afariki Ijue Madrasat Riyaadhwa ya mjini Dodoma Mwinyi apongeza juhudi za kulea yatima Mwanza Tuhuma za kupindua uongozi wa Bakwata: Sheikh Hamim Boza akanusha kuhusika Kuongezeka kwa ajali za barabarani Njia ya
uzimani ni nyembamba, waionao ni wachache - 4
Saggaf awataka watoto wahifadhi Qur'an Waislamu watakiwa kujitolea kupigania dini yao Kesi nyingine Mwembechai yaahirishwa Sayansi
na Teknolojia
Chakula
na lishe
|