AN-NUUR 
Na.182 Ramadhan 1419, Januari 1 - 7, 1998 
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita
 
Kuunganisha Kompyuta kwa Kutumia Modem
 
Na Hassan Omar

Modem inaweza bila ya wasiwasi wowote kutumika kuunganisha kompyuta mbili kwa namna nyingi sana. Tutakazozizungumzia hapa chini ni namna mbili: 

  1. Kuunganisha kompyuta mbili za kawaida zilizo mahali pamoja ambazo zote zinatumia Windows 95 (au Windows 98).
  2. Kuunganisha kompyuta mbili za kawaida zisizokuwa mahali pamoja lakini zote mbili zikiwa zimeunganishwa na line za simu zinazofanyakazi kama kawaida, na zote zinatumia Windows 95 (au Windows 98).
  

Kuunganisha kompyuta mbili zilizo mahali pamoja kwa kutumia modem 

Tuseme unazo kompyuta mbili na ungependa kunakili faili moja kutoka kwenye kompyuta moja kuingia kwenye kompyuta ya pili. Lakini kwa bahati mbaya huna diskette za kukusaidia kuifanya kazi hiyo; huna vifaa vya kukuwezesha kuziunganisha kompyuta hizo kwa kutumia Direct Cable Connection; na pia huna namna ya kuziunganisha kompyuta hizo kwenye LAN. Kama kompyuta zote mbili zina modem, basi ipo njia nyengine rahisi ya kuziunganisha. Fuata hatua zifuatazo: 

  1. Ziweke kompyuta zako karibu karibu, na uziwashe kama kawaida. Kama unatumia modem za nje, nazo pia ziwashe.
  2. Chomeka ncha moja ya waya wa simu (telephone cord) kwenye soketi iliyoandikwa TELCO au LINE kwenye modem iliyounganishwa na kompyuta ya kwanza, na ncha ya pili ya waya huo ichomeke kwenye soketi iliyoandikwa TELCO au LINE kwenye modem iliyounganishwa na kompyuta ya pili.
  3. Bonyeza Start -> Programs -> Accessories -> Hyperterminal. Bonyeza mara mbili (double-click) juu ya icon ya Hypertrm. Kwenye kidirisha cha Connection Description kama kinavyoonekana kwenye Picha 1, kwenye sehemu ya Name: jaza neno "blindial" na kwenye sehemu ya Icon: bonyeza picha ya icon unayoipenda kati ya icon zilizopo, na kisha bonyeza OK.
  4.  
    Picha 1: Kuanzisha HyperTerminal 
     

     
    Picha 2:  Kupiga simu kwenye HyperTerminal 
     

  5. Kwenye sehemu ya Phone Number ya kidirisha kitakachotokezea, weka nambari ya simu yoyote ile, kwa mfano "12345", na kisha bonyeza OK. Kwenye kidirisha cha Connect kitakachotokezea, bonyeza Cancel.
  6. Kwenye dirisha la HyperTerminal kama linavyoonekana kwenye Picha 2, andika neno AT na kisha bonyeza Enter. Likitokezea neno OK basi mambo mazuri. Kama hukupata OK basi modem yako labda hukuiwasha – iwashe na ujaribu tena kuipeleka amri ya AT. Ukiendelea kutopata OK, basi angalia vizuri ulivyoiunganisha modem yako na kompyuta. Inawezekana waya wa modem haukuungwa vizuri.
  7. Rudia hatua ya 3, 4, na 5 kwenye kompyuta ya pili.
  8. Kwenye kompyuta ya kwanza, kwenye dirisha la HyperTerminal, andika amri ifuatayo: ATM1X3D12345, kisha bonyeza Enter.
  9. Bila kuchelewa, kwenye dirisha la HyperTerminal la kompyuta ya pili, andika amri: ATA. Utasikia modem zikifanya mapatano (handshaking) na mwisho neno CONNECT litatokezea kuthibitisha kuwa kompyuta zako zimeungana.
Amri ATM1X3D12345 iliyotolewa kwenye hatua ya 7 inatafsirika kama ifuatavyo:  M1: Tunaiamrisha modem itoe sauti, ili tusikie kinachoendelea. 

X3: Tunaiambia modem ipige simu bila kungojea dial tone. Hiyo ni kwa sababu, modem zetu hatukuziunga kwenye line ya simu yoyote – tumeziunga zenyewe tu kwa hivyo hakuna dial tone. Dial tone huwa inatoka kwenye mitambo ya simu. Kupiga simu bila kungojea dial tone kunaitwa "blind dialing" – ndio maana tukatumia jina "blindial" kwenye hatua ya 3, ingawa haikuwa lazima kutumia jina hilo. Amri ya X3 ndiyo inayoruhusu kufanya blind dialing. 

D12345: Tunaiambia modem ipige simu nambari 12345. Nambari hiyo bila shaka ni ya bandia tu lakini kwa matumiazi yetu itakidhi haja. Tungeweza kutumia nambari nyengine yoyote ile. Sisi tunachotaka ni kuwa modem ipige simu – basi!

Amri ATA iliyotumiwa kwenye hatua ya 8 ni kuiambia modem ipokee (Answer) simu iliyopigwa. Kwa maelezo zaidi ya amri za modem soma kitabu (manual) kilichokuja na modem yako. 

Baada ya kompyuta zako mbili kuungana, unaweza kupeleka faili lolot lile kutoka kwenye kompyuta moja kwenda nyengine kwa kutumia HyperTerminal na kuchagua Transfer -> Send File, kama inavyoonekana kwenye Picha 3. Kwenye sehemu ya Filename kama inavyoonekana kwenye Picha 4, andika jina la faili unalotaka kulituma au unaweza kutumia Browse kulitafuta. Kwenye sehemu ya protokali ya Zmodem. Protokali hiyo ni protokali madhubuti sana ya kusafirishia mafaili kwa njia ya modem. Jinsi ilivyo madhubuti, ikitokezea kiungo kati ya modem na modem kukatika kutokana na sababu yoyote ile kabla ya faili halijamalizika kupelekwa, ukijaribu tena kulituma hilo file kwa njia hiyo, basi litaendelea kupelekwa sehemu iliyobaki tu, yaani halitaanza kupelekwa upya. 

 
Picha 3: Kupeleka faili kwa kutumia HyperTerminal 
 
 

 
Picha 4: Kuingiza jina la faili la kupelekwa 
 
 

Ukishachagua Zmodem bonyeza Send na mara nyingi hutahitaji kufanya chochote kwenye kompyuta ya pili – moja kwa moja (automatically) faili hilo litapokelewa na kuwekwa kwenye jalada C:\Program Files\Accessories\HyperTerminal. Kama hukuliona hapo, basi tumia Start-> Find ulitafute lilipowekwa. Kama itahitajika, unaweza kwenye HyperTerminal ya kompyuta ya pili kubonyeza Transfer -> Receive File na uchagua jalada (directory) la kuwekwa faili hilo na kuwa Zmodem ndiyo protokali ya kutumika, na kisha bonyeza Receive. 

Ukimaliza shughuli zako, kwenye dirisha la HyperTerminal la kompyuta ya kwanza, toa amri ATH ya kukata mawasiliano (Hangup). 

  
Kuunganisha kompyuta mbili zilizo mbali mbali kwa kutumia modem na line ya simu 

Tumeona hapo juu hapakuwa na lazima ya kuwa na line ya simu inayofanyakazi, kuunganisha kompyuta mbili zilizo mahali pamoja. Tumeziunganisha kwa kutumia waya tu wa simu (telephone cord) ambao unakuja pamoja na modem unapoinunua. 

Kama kompyuta ziko mbali mbali, tuseme moja iko nyumbani kwa rafiki yako na nyengine iko nyumbani kwako, au moja iko Dar es Salaam na nyengine iko Nairobi; hapo hatuna ujanja – itatubidi tutumie mawasiliano ya simu. Njia ya kutumia mawasiliano ya simu ni mufaka sana!  

Kwa mfano kampuni yako ina ofisi Arusha na ofisi hiyo inataka kutuma ripoti fulani makao makuu ya kampuni hiyo yaliyoko Dar. Kama ripoti hiyo imeandikwa kwa kutumia Excel basi ni kiasi cha kulituma tu hilo faili la Excel kwa njia tutakayoieleza hapa chini. Tutautumia mfano huo ili kurahisisha maelezo yetu. 

Mambo yanayohitajika ni kwa ofisi ya Arusha pamoja na ya Dar, kuwa na kompyuta zenye Windows 95, modem, na line za simu zinazofanyakazi. Utaratibu wa kuunganisha kompyuta hizo ni kama ulivyoelezwa kwenye hatua ya 1 mpaka ya 8 zinazohusu kuunganisha kompyuta zilizo mahali pamoja, isipokuwa kuna tafauti ndogo zifuatazo: 

  1. Kwenye hatua ya 2, ncha moja ya waya wa simu utahitaji kuchomekwa kwenye sehemu ya TELCO au LINE ya modem, na ncha nyengine iunganishwe na line ya simu – yaani ichomekwe kwenye soketi ya simu iliyo ukutani.
  2. Kwenye hatua ya 7, badala ya kutumia nambari 12345, itakupasa kuandika nambari hasa ya simu. Kwa mfano, kama ofisi ya Arusha ndiyo inayounganisha na makao makuu yaliyo Dar ambayo yanatumia nambari ya simu 960473, basi amri itakayotumika itakuwa ATM1DP051960473. Amri ya DP ni kuiamrisha modem ipige simu kwa kutumia "pulse dialing." Kama simu yako inatumia "tone dialing", itakupasa kutumia DT badala ya DP. Nambari 051 ni city code ya Dar es Salaam. Angalia pia hapa haikuwekwa X3 kwa vile modem ni bora kupata "dial tone" kabla ya kupiga simu – lakini itafanyakazi hata kama X3 itatumiwa.
  3. Wakati modem ya Arusha itakapoipigia simu modem ya Dar, kompyuta ya Dar iwe imewashwa na HyperTerminal imefunguliwa kama ilivyoelezwa kwenye hatua ya 3 na 4 ya sehemu iliyopita. Ikiwa katika hali hiyo, kwenye HyperTerminal utaona neno RING na ndio hapo utakapoandika amri ATA ili kukamilisha mawasiliano. Kama kwenye HyperTerminal ya kompyuta ya Dar, uliwahi kutoa amri ATS0=1 kabla ya kupigwa simu, modem hiyo ya dar itajibu yenyewe – yaani hutahitaji kutumia amri ATA. Amri ATS0=1 inaifanya modem ijibu baada ya simu kulia mlio mmoja tu. Kama unataka ijibu baada ya milio mitatu utatumia amri ATS0=3.
Hatua za kusafirisha faili kwa kutumia Zmodem ni kama zilivyoelezwa kwenye sehemu iliyopita. Baada ya shughuli kukamilika, tumia amri ATH kukata mawasiliano. 

  

Hitimisho 

Kwenye sehemu hii tumejifunza kuunganisha kompyuta mbili zilizo mahali pamoja kwa kutumia modem bila ya kuhitaji line ya simu. Pia tumejifunza kuunganisha kompyuta mbili zilizo mbali mbali kwa kutumia modem na mawasiliano ya simu. Katika njia zote mbili tumeweza kuona jinsi ya kusafirisha mafaili kwa kutumia protokali ya Zmodem. Tumejifunza kuwa kumbe modem hazitumiki kompyuta na Intaneti (Internet) tu kwa kupitia mitambo ya wanaotoa huduma za Intaneti (Internet Service Providers), bali hata sisi wenyewe kwa wenyewe tunaweza kuziunganisha kompyuta zetu kwa kutumia modem na tukaweza kupelekeana mafaili moja kwa moja badala ya kuepelekeana diskette kwa njia ya posta. 

Juu 
 

YALIYOMO 
 
 
Tahariri 
Kingunge, kweli upo uonevu na dhulma

Wananchi wahoji kuhusu polisi aliyeua Arusha

Matokeo ya Darasa la Saba yacheleweshwa kusherehekea sikukuu ya Krismasi: Wananchi wahoji je, nchi hii ina dini moja tu?

Njaa yaikumba Kilwa

Dondoo za Saikolojia
Na. Abu Halima Sachangwa

Kona ya Wacha Mungu
Mavuno yangu yasiwe...

Jicho la Uzalendo: Bhabhoo! Muungwana huyoo!
Na Sompo wa Kahambwe

Maulana Sayyid Jamal-Din Afghan 1214 - 1254 (1838-1897)

Mafunzo kuhusu funga ya Ramadhani
Imetayarishwa na Africa Muslims Agency

Marekani ni mtetezi au adui wa haki?: Umoja wa Mataifa upo upande gani?
Na Abu Salim

Dawa ya ukimwi ni mwenendo mwema
Na Habiba Swedi, Arusha

Mwalimu Maif: Mwanamke aliyetumia maisha yake kufundisha Qur'an

Ijue  Madrasa Hudaa Arusha

Wazazi waaswa kutoshabikia maovu

Mzee maarufu afariki Moro

Je, hivi tuendelee kushika amri za Mungu tena? (jibu) 
Na Ally Said

Mapinduzi, Muungano kwa manufaa ya nani?

Fufueni EAMWS - Sheikh Amana
Na Habiba Swedi

Msiitupie lawama serikali - Dk. Omar

Baada ya kuvunjiwa nyumba, kuchomewa vyakula na Serikali: Nzasa sasa wafuturu Maembe
Na Q. Mtaita

Acheni mifumo mibovu, fuateni Qur'an - Sheikh Kilemile

Sayansi na Teknolojia 
[Kuunganisha Kompyuta kwa Kutumia Modem

Masomo ya Dini ya Kiislamu 

Barua za Wasomaji 

Mashairi 

Chakula na lishe 
[Saumu na lishe ya mama anayenyonyesha] 
 

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtz.org
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita