|
|
| Tahariri
Onyesheni ushujaa wa Badri Dhulma itaondoka
mtakapoamua kuiondoa
WIKI ijayo wanafunzi wa kidato cha nne wanaanza mitihani yao ya mwisho. Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa, wanafunzi Waislamu licha ya kufanya mitihani yao huku wakiwa ndani ya swaumu; lakini pia watalazimika kufanya mitihani hiyo siku ya Eid el Fitr. Yaelekea serikali katika kutoa ratiba hii haikufikiria wala kujali hisia za wale ambao watakuwa wamefunga au kulazimika kufanya mitihani siku ya Eid el Fitr. Inawezekana hii ni kutokana na ukweli kwamba serikali haina dini japo inadai kwamba inaheshimu dini za watu. Lakini katika kipindi hicho hicho cha kutolewa ratiba hii; serikali hiyo hiyo imetutangazia kwamba imeahirisha kutangaza matokeo ya darasa la saba ili kusiwe na dosari katika kusherehekea sikukuu ya Krismasi. Kwamba lau matokeo hayo yangetangazwa siku chache kabla ya Krismasi wale watoto wa Kikristo ambao wamefeli wasingekuwa na furaha katika sikukuu hiyo. Lililo wazi hapa ni kuwa serikali inajali na kuheshimu hisia za Wakristo katika utendaji wake. Haitendi kana kwamba Wakristo hawapo wala haingoji kuombwa au kukumbushwa na Wakristo juu ya yale wayatakayo. Wengi watakuwa wanajiuliza ni ujumbe gani huu serikali imekusudia kuwawasilishia Waislamu? Huyu wa kusherehekea Krismasi; kutangazwa mitihani kabla au baada ya Krismasi hakuathiri lolote matokeo yake ya mtihani. Lakini pamoja na hayo serikali inamwambia; "tunakujali". Ila huyu ambaye matokeo ya mitihani yake yaweza kuathiriwa na mazingira anayoyafanyia mtihani sasa, hakuna anayejali. Yapo mengi ambayo wanafunzi Waislamu wamekuwa wakiyalalamikia huko mashuleni. Kwa hiyo, hili haliwezi kuwashtua sana. Pengine imekuwa ni kheri ili umma upate kufahamu kwamba yale wanafunzi Waislamu wanayolalamikia juu ya uonevu na dhulma dhidi yao ni kweli. Hapana shaka wanafunzi hawa wataingia katika vyumba vyao vya mitihani wakiwa mashujaa wa Badri. Mashujaa ambao wamepata bahati ya kushuhudia ule upendeleo wa kutangazwa waziwazi katika kipindi chao. Mashujaa ambao wanaingia kwenye vyumba vya mitihani wakijua kwamba hawana wa kuwajali kama wengine. Kama walivyokuwa Mashahid wa Badri karne 15 zilizopita, hatuna shaka tanuri hili la kufanya mitihani ndani ya swaumu na siku ya Eid el Fitr litanoa fikra zao na ushujaa wao wawe wapiganaji hodari wa kuleta ukombozi wa Waislamu. Ni kwa mantiki hiyo hiyo hatutarajii yeyote katika wanafunzi Waislamu afuate ushauri wa wale wenye kuifanyia stizai dini ya Allah (s.w.). Wale ambao hudai kwamba katika Uislamu kuna dharura na hivyo kuwataka waache kufunga siku za mitihani. Suala la msingi linalopasa vijana wetu walitambue ni kwamba hoja hapa si kufanya mitihani mwezi wa Ramadhani, lakini ule upeo wa ubaguzi, dhulma na upendeleo ulipofikia. Kwamba serikali haioni taabu kuwaambia wanafunzi Waislamu wafanye mtihani siku ya Eid el Fitr yao, lakini hujali kila Mkristo aisherehekee vyema Krismasi yake. Kubwa kwa sasa ni umma kushuhudia upendeleo huu na maadhali serikali ina uwezo na mabavu na mwelekeo wake ndio huu, bado tutaendelea kushuhudia mengi. Lakini, je, tushuhudie mpaka lini? Haki haiombwi wala dhulma haiondoki yenyewe, huondolewa. |
YALIYOMO
Tahariri Onyesheni ushujaa wa Badri Daniel kuwatimua waumini Msikitini Waislamu Moshi: Wadai kulishwa nguruwe, vibudu Dondoo za Kisakolojia
Maulana Sayyid Jamal-Din Afghan 1214 - 1254 (1838-1897) - 2 MASHAMBULIZI YA MAREKANI NCHINI IRAQ Njia bora zitakazotusaidia kuwalea
watoto
Ijue Madrasatul-Qaadiriya Sokoni
I Arusha.
Tutafute kwanza ufalme wa Allah (s.w.)
Chuo cha Kilimo Ukiriguru kupata
Msikiti mpya
Huduma za maji Kondoa haziridhishi
Mnyororo wa imani
Je, Yesu alibatizwa?
Kufuatia Waislamu kuritadishwa Merela Morogoro: Masheikh wa mjini watupiwa lawama Abiria walaani kumwagiwa pombe Kondoa Sheikh Bafadhil ateuliwa
kudhamini waandishi wa habari Morogoro
Sayansi na Teknolojia
Chakula na lishe
|