AN-NUUR 
Na.183 Ramadhan 1419, Januari 8 - 14, 1998 
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita
 
Sheikh Kisiwa atunuku zawadi
 

WAISLAMU wametakiwa kutumia mali zao vizuri kwa kufuata maadili ya Uislamu katika maisha yao ya kila siku. 

Hayo yalisemwa na Sheikh Kisiwa Ally baada ya kutunuku zawadi kwa wanafunzi na walimu katika tamasha la mashindano ya kusoma kwa kuhifadhi Qur’an lililofanyika hivi karibuni katika shule ya msingi Uhuru mjini hapa. 

Sheikh Kisiwa ambaye pia ni Sheikh wa Mkoa wa Arusha, alikuwa mgeni rasmi kwenye tamasha hilo lililoandaliwa na taasisi ya Masjidul Hidaya and Islamic Centre Olmatejo. 

Awali, Sheikh Kisiwa aliipongeza taasisi ya Masjidul Hidaya and Islamic Centre kwa kuandaa tamasha hilo kwa kusema kuwa ni jambo zuri kwani linatoa fursa ya kuwapima vijana juu ya ufahamu wao wa Qur’an na kiwango walichokihifadhi. 

Aliwaeleza wazazi na wageni mbalimbali waliohudhuria kuwa ni bora wakajizatiti ili kuyakuza mashindano hayo yafikie ngazi za juu kimkoa hadi taifa ili kuweka ushindani mkubwa ambao vijana kutoka madrasa mbalimbali ndani na nje ya mkoa watachuana. 

Pia aliwataka Waislamu kujitolea kwa hali na mali kutunisha mfuko ili kufanikisha mashindano ya aina hiyo kwa siku zijazo na kuweka mkakati wa pamoja wa kujihimiza madrasa zitilie nguvu suala la usomaji wa Qur’an. 

Aidha, Sheikh Kisiwa alifahamisha kuwa uongozi wa Manispaa ya Arusha unakamilisha taratibu za kupatikana kwa eneo jipya la makaburi kufuatia kujaa kwa eneo lililopo hivi sasa. 

Hata hivyo alitahadharisha kuwa eneo hilo jipya liko nje kidogo ya mji wa Arusha, na kwamba usafiri wa kumudu utahitajika ili kurahisisha mawasiliano. 

Hivyo, aliwataka Waislamu Arusha kujiandaa na michango ya kupata usafiri pindi watakapotakiwa kutekeleza hivyo. 

Mashindano hayo ya kuhifadhi Qur’an yaliwashirikisha zaidi ya wanafunzi 34 kutoka Madrasatul Hidaya inayomilikiwa na taasisi iliyoandaa na mwanafunzi mmoja kutoka madrasa ya Majengo kitongoji kimoja cha hapa Arusha. 

Pia wazazi na wageni mbalimbali mashuhuri walihudhuria ambapo ni pamoja na Sheikh wa Wilaya Sheikh Shaaban Juma, Ustadh Yahya Mgeni kutoka Nairobi, Bwana Miraji kutoka Shia Centre na Sheikh Hashim Lema, hao ni baadhi yao tu. 

Akitoa taarifa fupi, Katibu wa Taasisi hiyo Sheikh Juma Saidi Mndeme alisema azma kubwa ya mashindano hayo ni kuwalea vijana wa Kiislamu waweze kuifahamu Qur’an kwani ndio mwongozo pekee uliobaki na kwamba hiyo Qur’an iweze kutumika kama chombo cha kuwaunganisha Waislamu wa madhehebu zote kwa kuondoa tofauti zao na kuweza kushirikiana kuinua kiwango cha usomaji Qur’an. 

Jumla ya majaji watatu kutoka baadhi ya Misikiti ya mjini hapa walishiriki kikamilifu katika utafutaji wa washindi. 

Washindi 16 walipatikana waliohifadhi Qur’an kuanzia juzuu ya kwanza hadi ya kumi na tano. Wote hao walizawadiwa zawadi mbalimbali zikiwa ni pamoja na mshindi wa kwanza wa kuhifadhi juzuu kumi na tano Issa Yahya (15) kutunukiwa baiskeli aina ya Phoenix yenye thamani ya shilingi 75,000, mshindi wa pili wa kuhifadhi juzuu kumi na tano alipata Radio Cassette bendi 4. 

Zawadi nyingine kwa washindi wa kuanzia juzuu kumi hadi moja ni cherehani aina ya Butterfly yenye thamani ya shilingi 70,000 iliyotwaliwa na Naima Saidi mshindi wa kuhifadhi juzuu kumi. 

Magodoro, Redio, pasi ya umeme aina ya Philips, kanzu, hijab, saa za ukutani na majiko ya mafuta ya taa. 

Zikiwemo pia zawadi za jumla kwa washiriki nazo ni tochi, misahafu na saa za mkononi. 

Kivutio kikubwa katika mashindano hayo kilikuwa ni pale mtoto Gingi Issa Gingi (8) aliposoma Qur’an vizuri na wengi kufurahia. Alishinda katika waliohifadhi juzuu moja na kupata saa ya adhana. 

Walimu watano nao walitunukiwa zawadi siku hiyo mwalimu wa siku nyingi madrasani hapo, Maalim Juma Haji alipata televisheni aina ya Hitachi inchi 14 yenye thamani ya shilingi 220,000, Mwalimu Mkuu alipata saa ya mkono, Maalim Yasiri alipewa saa ya ukutani, Maalim Adam alipata saa ya mkono na Mwalimu wa kinamama Ustadha Mariam alitunukiwa saa ya mkono. 

Wakati huo huo, jumla ya fedha taslim shilingi 20,300 zilikusanywa katika tamasha la kusoma na kuhifadhi Qur’an kama mwanzo tu wa kutunisha mfuko wa mashindano yajayo. 

Akitangaza kima hicho, Sheikh Hashim Lema aliwashukuru wote waliotoa michango yao na kukaribisha michango zaidi kutoka kwa Waislamu. 


Chuo cha Kilimo Ukiriguru kupata Msikiti mpya
 
Na Mwandishi Wetu, Mwanza

WATUMISHI wa Chuo cha Kilimo cha Ukiriguru kilichoo mjini Mwanza wameanza rasmi ujenzi wa Msikiti katika eneo ambalo wamepewa na Utawala wa Chuo. 

Eneo hilo ambalo limo ndani ya Chuo hicho, kuna Msikiti ambao ni wa zamani mno na tayari kuta zake zina nyufa na baadhi zimeanguka kabisa. 

Akiongea na ANNUUR, mjumbe mmoja wa kamati ya Msikiti huo alidokeza kuwa wamekuwa katika hali ngumu ya kuuendeleza Msikiti huo. Kwa muda mrefu, wamekuwa wakichangishana kwa kila mwezi kwa kila familia. 

Amesema kuwa pesa hizo hazitoshi kuanza ujenzi kutokana gharama za vifaa vya ujenzi kuwa kubwa, alitaja kuwa kuna familia arobaini za Waislamu chuoni hapo, kwa kuwa wamelazimika kumuweka Mwalimu wa Madrasa wa kuwasomesha watoto wao imekuwa ni vigumu wao kumudu gharama zote kwa wakati mmoja. 

Umoja wa ufundishaji Madrasa (UUM) ambao ni mchanganyiko wa vijana ambao wamejikusanya ili kuhuisha elimu katika madrasa mbalimbali hasa za nje ya mji wa Mwanza, makao yako Msikiti wa Memani, Mwanza na wanaendesha masomo mbalimbali hasa Qur’an kwa watu wazima saa za jioni Msikitini hapo. 

Mwenyekiti wa umoja huo ni Ustadh Shaaban Juma Kondo aliliambia ANNUUR kuwa pamoja na kutoa misaada mbalimbali kwa madrasa za nje ya mji wa Mwanza pia wamekubali kushirikiana na uongozi huo wa Msikiti wa Ukiriguru kujenga Msikiti ho kwa kutoa vifaa vya ujenzi na wao kwenda huko kila Jumapili kufanya kazi ya kawaida kupunguza gharama za ujenzi. 

Vijana wa UUM tayari wanaendesha madrasa za Usagara, Fela ambapo wanajenga madrasa katika kiwanja kilichotolewa na Muislamu mmoja mkazi wa hapo Fela, tayari wameshatoa vifaa vya kufundishia kwa madrasa za Igogo, Kalunda, Katunguru na baadhi ya madrasa za Mwanza Mjini. 

Hali kadhalika, wanalipa posho kwa walimu ambao madrasa zao hazina vipato ili kukidhi mahitaji muhimu ya maisha, wamebuni Sylabasi ya namna ya kusomesha Qur’an kwa muda mfupi na mtoto kuweza kusoma bila matatizo yoyote. Katika madrasa ambazo wanashirikiana wao ndio wanaowatungia mitihani kwa mujibu wa sylabasi zao. 


Huduma za maji Kondoa haziridhishi

Na Abu Zuberi, Kondoa 

WAKAZI wa kijiji cha Hamai Tarafa ya Goima wilayani Kondoa wamekuwa na usumbufu wa muda mrefu na adha kubwa ya kutembea mwendo mrefu kuchota maji. 

Mama mmoja aliyejitambulisha kuwa Mama Bahati ambaye ni mkazi wa kijijini hapo, akizungumza na mwandishi wa habari hizi alisema kuwa muda wetu wa uzalishaji unaathiriwa sana na kuhangaika kuchota maji, kwani inawabidi kuamka asubuhi sana na kutumia zaidi ya masaa matatu kwa kuyapata maji hayo. 

Mwandishi wa habari hizi alibahatika kufika hapo kisimani na kumwona mama Bahati akiwa ndani ya kisima huku kikikanyagwa kwa miguu na kufikia hatua ya kuyachafua hayo maji. 

Katika kijiji cha Hamai na Songolo, kuna wakazi wasiopungua 3000, wenyeji wake hulima mazao ya mtama, uwele, ulezi na mbaazi. 

Mwandishi wa habari hizi alishuhudia vijana wadogo wakitoa huduma za kusafirisha abiria kwa kutumia baiskeli na kwa bei atakayopanga mteja. 

Serikali katika ilani yake ya uchaguzi ilitoa ahadi nyingi na nzuri. Lakini machungu yanayowapata wananchi vijijini hawana hamu hata ya kuishi. 

Wakati huo huo, Waislamu wa kijiji cha Songolo tarafa ya Goima wilayani Kondoa, wamewaomba Waislamu kuisaidia madrasa ya Shamsiya iliyopo kijijini hapo kumalizia jengo. 

Akitoa taarifa hizi, Katibu wa kamati ya ujenzi, Sheikh Rashid Ally alimuelezea mwandishi wa gazeti hili kuwa tangu mwaka 1992 wakati Mufti Mkuu Sheikh Hemed bin Juma bin Hemed alipoweka jiwe la msingi hapakutokea jitihada za kuridhisha kuendeleza jengo hilo. 

Madrasatil Shamsiya yenye wanafunzi 65, wakiwa na darasa la kina mama wapatao 20 wanasomea ndani ya jengo ambalo halikuwezekwa, hivyo hali ya kuendelea na ratiba ya kusoma wakati wa mvua huwa ngumu, aidha kipindi cha jua kinawafanya wanafunzi kuwa katika hali ngumu ya joto. 

Ustadh Mohamed Rashidi ambaye ni mwalimu wa madrasa hiyo alimueleza mwandishi wa habari hizi kuwa Waislamu hawana mzuri wa kutoa hata hili jengo la madrasa lilikuwa ni nyumba ya mtu, na hata hivyo, Waislamu wameshindwa kuliendeleza kwa muda wa miaka saba sasa. 

Pamoja na hali hiyo, wanawaomba ndugu zao wa Kiislamu kuwasadia katika ujenzi wa jengo hilo ambalo limefikia sehemu ya linta 

Juu 
 

YALIYOMO 
 
 
Tahariri 
Onyesheni ushujaa wa Badri 

Daniel kuwatimua waumini Msikitini 

Waislamu Moshi: Wadai kulishwa nguruwe, vibudu 

Dondoo za Kisakolojia 
Na. Abu Halima Sachangwa 

Kona ya WachaMungu  

Jicho la Uzalendo 

Maulana Sayyid Jamal-Din Afghan 1214 - 1254 (1838-1897) - 2 

Vipi umoja wetu uwe hatari ? 

MASHAMBULIZI YA MAREKANI NCHINI IRAQ  

Marekani si rafiki mwema  

Tunahitaji UN ya Waislamu - 2  

Njia bora zitakazotusaidia kuwalea watoto 
Na Ust. Hashim Rusaganya, Mombasa 

Ijue Madrasatul-Qaadiriya Sokoni I Arusha. 
Na Habiba Swedi, Arusha 

Tutafute kwanza ufalme wa Allah (s.w.) 
Na Mwapwani Mohammed 

Sheikh Kisiwa atunuku zawadi 

Chuo cha Kilimo Ukiriguru kupata Msikiti mpya  
Na Mwandishi Wetu, Mwanza  

Huduma za maji Kondoa haziridhishi 
Na Abu Zuberi, Kondoa  

Mnyororo wa imani 
Na Sheikh Bernard P. Nyangasa 

Je, Yesu alibatizwa? 
Na Muhibu Said  

Kufuatia Waislamu kuritadishwa Merela Morogoro: Masheikh wa mjini watupiwa lawama  

Abiria walaani kumwagiwa pombe Kondoa 

Sheikh Bafadhil ateuliwa kudhamini waandishi wa habari Morogoro 
Na Mussa Ally, Morogoro 

Sayansi na Teknolojia 
[Tatizo la mwaka 2000] 

Masomo ya Dini ya Kiislamu 

Barua za Wasomaji 

Chakula na lishe 
[Mlo wa siku ya Idd] 


Bonyeza hapa
kushriki mjadala au kutoa maoni juu ya habari hizi na masuala mengineyo ya Kiislamu kwenye Baraza ya Wasomaji

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtz.org
 
Home Links Islam Tanzania Matoleo yaliyopita