|
|
|
WAISLAMU Jijini wamekamata mali ya Wakfu iliyoachwa na marehemu Hajat Aziza Omar ambayo iliporwa kwa njia za udanganyifu na mtu mmoja aliyefahamika kwa jina la Daniel Zakaria (Mkristo) miaka sita iliyopita. Mali hiyo ambayo ni nyumba Na. 58 iliyopo Mtaa wa Somali Gerezani Jijini Dar es Salaam, ilirejeshwa kwa Waislamu baada ya Khitma na Dua iliyosomwa mahali hapo Jumapili iliyopita. ANNUUR ilishuhudia umati wa vijana kwa wazee uliohudhuria dua hiyo ambapo mwishoni mwa hafla hiyo Waislamu hao waliingia ndani ya nyumba hiyo na kuanza kuitwaharisha ambamo walikuta maboksi kadhaa ya kondomu na chupa za konyagi zilizoashiria nyumba hiyo ilivyogeuzwa Danguro . Akitoa historia fupi ya nyumba hiyo ya Wakfu, mhadhiri wa hafla hiyo kwa niaba ya waliohudhuria hapo, alisema kwamba kabla ya kifo cha mmiliki wa nyumba hiyo Hajat Aziza uliandikwa wasia ambao ulithibitishwa na mahakama ya Kariakoo kwamba nyumba hiyo imetolewa Wakfu kwa Waislamu na Masjid Mwinyi uwe mdhamini wake. Baada ya kufariki dunia Hajat huyo mwezi Mei 1991 miezi minne baadaye (Septemba 13, 1991) wadhamini walitoa tangazo la mirathi katika gazeti la Uhuru lililokuwa gazeti pekee la kila siku wakati huo kwa lugha ya Kiswahili. Mhadhiri huyo aliendelea kueleza kuwa tangazo hilo halikupingwa na yeyote mpaka siku 90 kisheria zilipokwisha. "Daniel alianza utapeli wake kwa kutoa tangazo la mirathi kwenye "Government Gazette" ambalo halisomwi na watu wa kawaida; hapa ndipo alipoanza udanganyifu wake", alisema mhadhiri huyo. Ilielezwa kuwa baada ya tangazo hilo alipeleka "madai" yake mbele ya Mahakama ya Kisutu ambako alifanikiwa kuidanganya mahakama na kupewa haki ya kurithi nyumba hiyo. ANNUUR imefahamishwa kuwa Daniel alishirikiana na mtu mwingine anayeitwa Pius Kipengule waliweza kuwazunguka wasimamizi wa Masjid Mwinyi na kufanikiwa kupora nyumba tangu wakati huo ambapo waliigeuza na kuwa baa hali ambayo iliwakasirisha hata majirani walio karibu na nyumba hiyo. Mama mmoja ambaye hujishughulisha na biashara ya mama ntilie mtaani hapo aliliambia gazeti hili kuwa alikuwa akiona uchungu jinsi uovu ulivyokuwa ukiendelea nyumba hiyo wakati alimfahamu mwenyewe marehemu Hajat Aziza kwa ucha Mungu wake. "Kila mwaka mfungo sita alikuwa akisoma ziara (Maulid Nabi) watu walikuwa wakijaa mtaa huu mzima", mama huyo alimweleza mwandishi wa habari hizi. Aidha, alisema ameshangazwa na jinsi Daniel ambaye ni Mkristo alivyovamia nyumba hiyo na kurithi wakati Bibi huyo alikuwa Muislamu na hakuwa na mtoto wala ndugu wa nasaba. "Nimezaliwa mimi hapa mtaani mpaka napata akili namkuta bibi akiwa peke yake na nyumba yake alikuwa akiita Wakfu", ameeleza mama huyo anayekisiwa kuwa na umri wa miaka isiyopungua 45. Alimtuhumu Bi. mkubwa mmoja Mkristo mtaani hapo kwamba huenda alikuwa akishirikiana na "waporaji" hao. Aliyekuwa mjumbe wa nyumba kumi wa mtaa huo Bwana Haruna Said Muchunguzi ambaye hivi sasa anaishi maeneo ya Kigogo akieleza kwa mwandishi njama za Daniel kupora nyumba hiyo, alisema yeye alimsaidia marehemu pale alipoibiwa nyaraka zake za nyumba. Bwana Muchunguzi ambaye alikuwa mfanyakazi wa Bandari wakati huo, amesema baada ya wizi huo wa nyaraka kutokea walipiga ripoti kituo cha polisi Msimbazi na kumtaja waliyemtuhumu (Daniel Zakaria). Ameeleza Bwana Muchunguzi kuwa polisi Msimbazi ilitoa hati ya kukamatwa (RB) Bw. Daniel ambaye alikimbia tangu wakati huo hadi alipofariki bi kizee huyo ambapo aliibuka na kudai nyumba hiyo ni yake. "Alifukuza wapangaji wote, majirani wote waliojitokeza kumpinga aliwaweka ndani (polisi), mimi na Bwana Semvua tu ndio hakuweza", ameeleza Bwana Muchunguzi alipokuwa akihojiwa na mwandishi wa ANNUUR nyumbani kwake Kigogo jioni ya Jumanne wiki hii. Aidha, Bwana Muchunguzi amesema suala la nyumba za Hajat Aziza Omar walilifikisha kwa aliyekuwa Rais wa Awamu ya Pili Alhaj Ali Hassan Mwinyi ambaye amesema walimkabidhi baadhi ya nyaraka za nyumba za bibi huyo. ANNUUR ilijaribu mara kadhaa katika kipindi cha wiki moja iliyopita
kuwasiliana na Bwana Daniel kuhusiana na mkasa huu hata hvyo katika hali
ya kutatanisha haikuweza kumpata katika maeneo anakopatikana.
|
YALIYOMO
Tahari
Kupokelewa kwa malalamiko ya Waislamu: Masheikh wasubiri ukweli wa Mkapa Afariki baada ya kutokwa damu nyingi: Yadaiwa hakuwa na sh. 4,000 Nyumba ya Wakfu iliyoporwa yarejeshwa Kamanda Gewe atakiwa amkamate Daniel Sheikh awasambaratisha walevi Liwale Msikiti wavamiwa na kuvunjwa milango, madirisha Msikiti wa Mwinyimkuu wafanya sensa Njaa hakuna, tunategemea kula silaha Mabaraza yawatetee Waislamu - Sheikh Bafadhil Hali ya Uislamu Lukulunge, Kongwa inatisha Waislamu Kondoa waagizwa kuyatunza magazeti ya ANNUUR Sabato ni ya Waisraeli, Mungu alikwishaiondoa
Tume ya kubadili Katiba Kenya: Waislamu kuwakilishwa Waislamu Msonge waomba wanusuriwe Sayansi na Teknolojia
Chakula na Lishe
|