Aidha, Mwalimu huyo amemshutumu Mbunge wa Kigamboni Mh. Kitwana Kondo kwa kumwita mchochezi mkubwa.
Mama Paulina ametoa shutuma hizo wakati akijieleza ni kwanini aliwazuia wanafunzi Waislamu waliovaa Hijab kuingia darasani.
Akiongea na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake jana, Mwalimu huyo alisema pamoja na kuwepo taarifa za serikali kupitia vyombo vya habari kwamba wanafunzi wanaovaa Hijab wasibughudhiwe, yeye hatawaruhusu kwani hana waraka unaompa maelekezo hayo.
Huku akikariri mara kwa mara kauli ya kujinasibu na Ukristo wake, Mwalimu Paulina alisema kwamba kuruhusu Hijab shuleni ni kuifanya shule yake kuwa ya Kiislamu hivyo, akawataka wanafunzi Waislamu wenye kuvaa Hijab waende kwenye madrasa kwani huko ndiko kwenye Hijab.
Alipoulizwa ni vipi anapingana na agizo la Waziri wake tena lililotolewa katika kikao kizito cha Bunge; Mwalimu Paulina alijibu kwa jazba huku akinasibisha maelekezo hayo ya Mh. Waziri na kile alichokiita uchochezi wa Mh. Kitwana Kondo na kuendelea kudai kwamba "Kapuya mwenyewe kalipua mambo Bungeni na kukimbilia Tabora".
Gazeti hili liliwasiliana na Wizara ya Elimu na Utamaduni kutaka kujua maoni ya Mh. Waziri juu ya kauli ya Mwalimu Paulina kwamba hawezi kufanya kazi kwa kauli za Waziri na kwamba amekuwa mlipua mambo Bungeni na kukimbilia Tabora; hata hivyo msemaji wa Ofisi yake alisema kwamba Waziri Kapuya yupo Tabora.
Kwa muda wa wiki mbili sasa pamekuwa na mvutano kati ya Mwalimu Mkuu huyo na wazazi wa baadhi ya wanafunzi ambao wamezuiliwa kuingia darasani kwa vile wamevaa vazi la stara.
Akiongea Bungeni hivi karibuni Waziri wa Elimu Mh. Profesa Juma Kapuya alisisitiza juu ya agizo la serikali kwamba watoto Waislamu wanaotaka kuvaa Hijab waruhusiwe na vile vile utolewe muda wa kutosha siku ya Ijumaa waende kuswali.
Ufafanuzi huo wa Mh. Profesa Kapuya ulifuatia ombi la Mbunge wa Kigamboni Mh. Kitwana Kondo kutaka Waziri atoe maelezo juu ya masuala hayo.
|
|