Suala la uvaaji wa Hijab mashuleni
Maafisa Elimu ‘wapewa semina’:
 

WATENDAJI wa Wizara ya Elimu na Utamaduni wametakiwa wasilitilie unyeti na kulibinafsisha suala la uvaaji hijabu mashuleni. Aidha watendaji hao wametakiwa wasilete mgongano na wazazi na wakuu wa shule kwa tabia yao ya kutokupeleka waraka na maagizo mbalimbali kwa wakuu hao yanayolenga kutekelezwa kwa sera na maelekezo ya Wizara.

Wito huo ulitolewa na wazazi Waislamu kwa Maofisa wa Wizara ya Elimu waliokutana nao katika shule ya Msingi Mlimani Februari 24, 1999.

Maafisa hao walifika shuleni hapo ili kuonana na baadhi ya wazazi ambao watoto wao walizuiliwa kuingiamadarasani kwa vile walikuwa wamevaa Hijab.

Kwa mujibu wa maelezo ya mzazi mmoja aliyehudhuria kikao hicho; hali ya kutokuelewana ilitokea pale Maofisa hao waliposisitiza kwamba wangeongea na mama wa Mariam (Mapi Kitama) na wala sio baba yake wala wazazi wengine kwa hoja kwamba yeye ndiye aliyeandika barua Wizarani kulalamika.

Hata hivyo, mzazi huyo Bi. Asha amesema kwamba wazazi walisisitiza kwamba hilo sio suala binafsi la Mama Mariam bali watoto na wazazi wote Waislamu. Na ilichotakiwa Wizara si kwenda kila shule na kuongea na mzazi mmoja mmoja binafsi bali kutoa maelekezo kwa waalimu wakuu wa shule kote nchini.

Bi Asha amesema kwamba aliyejitokeza kama kiongozi wa msafara huo wa Maafisa wa Elimu aling’ang’ania msimamo wake wa kutokusema lolote mpaka aongee na Mama Mariam na wala si baba yake au mzazi mwingine yeyote.

Kwa msimamo huo anasema Bi Asha, wazazi walieleza wasiwasi wao kwamba palikuwa na agenda ama ya kuzuia maelekezo ya Wizara kuwafikia wazazi na pengine hata kumtisha mzazi mmoja mmoja ili warejee nyuma.

Wazazi walimtaka Afisa huyo ambaye hakutaja jina wala cheo chake aeleze endapo ana maelekezo yoyote toka Wizarani kuhusu hijab au kama hana basi wao wampe salamu za kupeleka Wizarani.

Kufika hapo anasema Bi Asha; Afisa huyo mwanamke alilazimika kuwaita wenzake wapatao watano ambao walikuwa kwenye chumba kingine wakisubiri kumhoji Mama Mariam.

Maofisa hao nao walisisitiza msimamo wao kulifanya suala hilo kuwa la kibinafsi. Hata hivyo baada ya kukosa hoja walikubali kupokea maoni ya wazazi wote ambapo waliambiwa wapeleke salamu Wizarani kwamba suala hili wasilifanye nyeti wala la kibinafsi. Pili; waharakishe kutuma maelekezo kwa wakuu wa shule ili kuondoa migongano baina ya wazazi na wakuu hao.

Aidha, walielezwa kwamba siku nyingine wasipange kikao saa saba kwani huo ni muda wa swala. Kama kikao italazimika kiwe mchana basi kianze saa nane na kwisha kabla ya saa kumi wakati wa swala ya Alasiri; au kama kitaendelea basi pawe na mapumziko baina ya saa 10 na saa 10:30 kwa ajili ya swala.

Hata hivyo, wazazi wengine wameeleza kwamba Maofisa hao baada ya kukosa hoja waliwaeleza wazazi kwamba tayari wakuu wa shule zote za mkoa wa Dar es Salaam walishapewa maelekezo jinsi ya uvaaji wa hijab. Maelekezo hayo yalitolewa katika kikao kilichofanyika Jumamosi ya Februari 20, 1999.

Maelezo hayo yaliungwa mkono na Mkuu wa Shule ya Mlimani Paulina Mndolwa aliyefafanuwa kwamba ushungi unatakiwa uwe mweupe na uwe wa pembetatu na uwezeshe nembo ya shule kuonekana.


Wakatoliki wawafurusha Waislamu
 

HUKUMU ya Hakimu wa Wilaya ya Same Bw. S. N. Mtui imewawezesha Wakatoliki wa Duma Mbanga kuwafurusha kwenye eneo lao ambalo wamekuwa wakilimiki toka mwaka 1953.

Hukumu hiyo ya Bw. Mtui inafuatia rufaa iliyoombwa na Wakatoliki baada ya kushindwa katika Mahakama ya Mwanzo.

Katika hukumu ya awali mahakama iliwaona Wakatoliki wenye hatia ya kuvamia eneo la Waislamu na kujenga nyumba ya kudumu kwa makusudi ili iwe njia ya kunyanyang’a eneo hilo.

Kutokana na ushahidi uliotolewa mahakamani ikiwa ni pamoja na mahakama kuzuru eneo hilo, hukumu ilitolewa kwamba eneo lenye mgogoro ni la Waislamu na Wakatoliki wakaamriwa kubomoa nyumba zao.

Hisia na maoni mbalimbali yameibuka huko Mbaga kufuatia hukumu ya Bw. S.N. Mtui.

Waislamu wengi wamekuwa wakidai kwamba haki haikutumika bali ‘udini’ umeingia kati. ANNUUR ilipotembelea eneo hilo hivi karibuni ilielezwa kwamba Wakatoliki wamekuwa wakiwasuta Waislamu kwamba wamelala ndio maana wamewapora eneo lao.

Aidha, imeelezwa kwamba pamekuwa na majigambo kwamba Waislamu hawawezi kushinda hata wakikata rufaa kwani hakuna mahakimu Waislamu wa kuwasimamia wala hawana fedha.

Mzee mmoja akiongea na mwandishi wa habari hizi mjini Same alilalamika akisema "wenzetu (Wakatoliki) wanajigamba kwamba wao ni mbwa mweusi asiyeogopa kichaka na kwamba wana mahakimu wa kusimamia kesi zao".

Mzee huyo ambaye hakutaka jina lake litajwe gazetini ameeleza kwamba wao Waislamu wa Mbaga wataendelea kufuata mlolongo wa sheria lakini kama sheria na haki haikutendeka "ijulikane na mapema kwamba hata kama Wakatoliki watakuwa wameshajenga hawatokaa, watalikimbia jengo hilo", alisema mzee huyo bila ya kufafanua.

Naye Mzee mwingine aliyejitambulisha kwa jina moja tu la Mmbagha alisema kwamba hawana sababu ya kuhisi kwamba Ukatoliki umetumika katika kutoa hukumu ya shauri hili katika ngazi ya wilaya.

Hata hivyo, akasema kwamba majigambo na maneno ya kejeli toka kwa wenzao ndiyo yanayoibua wasiwasi.

Bw. Mmbagha alidai kwamba toka awali walimjua Bw. Mtui kwamba ni Mkatoliki safi ambaye kila alfajiri hakosi ibada ya saa 12 katika Kanisa la Katoliki Same mjini japo anakaa mbali. Lakini hawakuwa na wasiwasi kwamba Ukatoliki wake ungeathiri kesi ambayo mshitakiwa ni Mkatoliki akishitakiwa na Muislamu.

Hata hivyo, anasema hali ya kutamba ya Wakatoliki wa Mbaga imewatia wasiwasi.

Aidha, amesema vikwazo ambavyo wamekuwa wakivipata katika kufuatilia hukumu na taratibu za kukata rufaa imezidi kuwaongezea wasiwasi.

Habari tulizozipata tukienda mitamboni zimeeleza kwamba Waislamu wameshawasilisha maombi yao ya kukata rufaa katika mahakama kuu Moshi.

 

Juu RUDI


Bonyeza hapa
kushriki mjadala au kutoa maoni juu ya habari hizi na masuala mengineyo ya Kiislamu kwenye Baraza ya Wasomaji

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtz.org
 
An-nuur Home | Ukurasa wa Mwanzo | Islam Tanzania 
Links | Matoleo Yaliyopita | Sign our Guestbook