SHIRIKA la Habari la Sudan ‘SUNA’ limemkariri kiongozi mmoja wa serikali akisema kuwa, tangu utangazwe mpango wa kusimamisha vita baina ya serikali ya Sudan na waasi katika eneo la El-Ghazal El-Kubra mwaka jana, jeshi la waasi limekuwa likiwashambulia na kuwauwa wananchi wa eneo hilo.
Aidha, jeshi hilo la waasi limekuwa likiwashambulia na kuwaua wanajeshi wa serikali pamoja na kutega mabomu katika maeneo mbalimbali ya ukanda huo, huku ikitupilia mbali makubaliano ya kusitisha vita.
Imeripotiwa kuwepo vitendo vya wizi na kupora mali za wananchi katika sehemu mbalimbali hasa Ouwel na Wawi katika kipindi chote cha makubaliano.
Vitendo hivyo vimeonyesha na kuthibitisha nia ya waasi ya kuvunja makubaliano na au kushindwa kwa uongozi wa waasi kuyadhibiti majeshi yake katika uwanja wa vita.
Vile vile ukiukaji wa makubaliano ya kusitisha vita umedhihirishwa na vitendo vya waasi kutoa mafunzo na mazoezi ya kijeshi katika maeneo ya Rumbik, Otiit na Waaraap.
Msemaji wa serikali ya Sudan amenukuliwa kusema idadi kubwa ya wanajeshi wa waasi wanahitimu mafunzo hayo mara kwa mara ili kuuthibitishia ulimwengu kuwa waasi wa Sudan "SLP" walikubali mkataba wa kusitisha vita ili wapate fursa ya kujiandaa kijeshi na ili jeshi la serikali lisivishambulie vituo vyao vya mafunzo ya kijeshi na wala si kweli eti walitia sahihi makubaliano ya kusitisha vita kwa kuwaonea huruma wananchi wa Sudan".
|
|