Na Mwandishi Wetu, Kigoma
WAISLAMU nchini wametakiwa kutosahau uvamizi, utesaji na udhalilishaji uliofanywa na polisi dhidi ya Waislamu pale Mwembechai mwaka jana.
Akihutubia mamia ya Waislamu waliojazana ndani na nje ya Msikiti wa Ijumaa Shaurimoyo hivi karibuni Mwanga mjini hapa, Sheikh Ayubu Sadiki ambaye pia ni Makamu Sheikh wa Mtaa wa Mwanga Kusini (BAKWATA) na mmoja wa Makhatibu wa Msikiti wa Ijumaa Shaurimoyo alionya kuwa wako Waislamu wanaochukulia suala la Mwembechai linawahusu Waislamu wa Dar es Salaam peke yao na kusema dhana hiyo ni potofu kabisa.
Aidha, Sheikh huyo aliwatahadharisha Waislamu kuwa yale yaliyowakuta Waislamu Mwembechai yanaweza kuwakuta hata wao. Na akawakumbusha kwamba adui wa Waislamu na Uislamu kamwe hatoridhika mpaka ahakikishe Waislamu na Uislamu vimetoweka katika ardhi hii.
"Wako wale wanaojifanya hawahusiki na kadhia hii nzito ya Mwembechai. Na pindi wanapoombwa michango ili kuwasaidia ndugu zetu waathirika wa Mwembechai, hutaka kuhoji sana na kutoa vijisababu visivyo na msingi wowote ule, basi waache kabisa tabia hiyo. Huo sio Uislamu", alisema Sheikh Ayubu.
Aidha alisema, viongozi wa kidini wamekuwa wakitoa mawaidha mbalimbali na kwa muda mrefu, lakini hakuna mabadiliko yoyote katika jamii ya Kiislamu.
Kauli hiyo ya Sheikh Ayubu imekuja wakati ambapo kuna habari kwamba viongozi wa Kamati ya Akinamama Taifa wakiongozwa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo ya Taifa Bi. Fatma Lazaro pamoja na akinamama waathirika watafika hivi karibuni ili kuadhimisha mwaka mmoja tangu polisi walipowaua Waislamu wasio na hatia pale Mwembechai.
Kwa mujibu wa maelezo ya viongozi wa Misikiti ya hapa Mwanga, kutakuwepo na kongamano kubwa la kitaifa litakalowahusisha Waislamu toka mikoa yote ya Tanzania ambalo litafanyika hapa Mwanga.
Wakati huo huo, mtoto wa kwanza wa mwanaharakati mashuhuri wa Kiislamu mjini hapa Maalim Hassan Mtabindi ameuawa kwa kupigwa risasi na majambazi.
Mtoto huyo Rajabu Hassan (19) alipigwa risasi mgongoni sehemu za begani na mguu wa kushoto, risasi ambayo ilimvunja mguu na marehemu alifariki hapo hapo.
Tukio hilo lilitokea katikati
ya mwezi uliopiga, mwaka huu siku ya Jumamosi saa saba na nusu usiku eneo
la Vamia Mwanga Kusini. Mtoto huyo alikuwa ni mwanafunzi wa sekondari ya
Mlole (Sabasaba).
|
|