Masahiri

Mashairi ya zamani

Uhuru, Jumanne Agosti 5, 1969

Mzazai hana kinyongo, kwa wanao wacha inda,
Ukawatenga mtengo, kuchagua wa kupenda,
Huo ndugu si mpango, usijaribu kutenda,
Hachagui wa kupenda, mzazi mwenye busara.

Mzazi mwenye busara, uwa hodari kuunda,
Huunda kama Sonara, unyosha kilicho pinda,
Ndipo upewa hongera, kwa ujuzi wakufunda,
Hachagui wa kupenda, mzazi mwenye busara.

Mungu kakupa bahati, kuzaa watoto kenda,
Wavulana na binati, wako nyumbani waranda,
Baba uwe katikati, hadabu njema kudunda,
Hachagui wa kupenda, mzazi mwenye busara.

Usichague kikundi, wengine wabaki munda,
Kwa sababu si washindi, miili yao imekonda,
Mzazi haitwi fundi, kwa Majura ni Kamanda,
Hachagui wa kupenda, mzazi mwenye busara.

Ewe mzazi mwenzangu, sikia ino agenda,
Unao gawa mafungu, watoto kama matunda,
Hapendezwi bwana Mungu, kwa hayo unayotenda,
Hachagui wa kupenda, mzazi mwenye busara.

Chonde ninakuchondela, moyo wako wachainda,
Baba usiwe nahila, kama mti na maganda,
Huo ni ukabaila, Tanzania twauponda,
Hachagui wa kupenda, mzazi mwenye busara.

Hivyo ukiwa tajiri, umeanzisha kiwanda,
Watumishi tawadhiri, kuwafanya makinda,
Wengine nguo nzuri, wengine wavae gwanda?
Hachagui wa kupenda, mzazi mwenye busara.

Hapa ndio kaditama, sifikishi beti kenda,
Siku nyingi sijasema, nafasi inanishinda,
Leo ninaunguruma, katu simba hawi punda!
Hachagui wa kupenda, mzazi mwenye busara.

H.S. Kibugo (Nkojabuli)
S.L.P. 20592,
Dar es Salaam.



Ahadi kuitimiza

Mwafrika na Taifa Novemba 10, 1962

Leo napiga kilemba, nitoe wangu undani,
Nina wimbo naimba, umenijaa kinywani,
Nacheza huku nayumba, furaha tele moyoni,
Ahadi kuitimiza, dunia huwa ni pepo.

Dunia huwa ni pepo, ahadi ikitimizwa,
Na akherza uendapo, pema utapokelewa,
Wallahi nala kiapo, motoni hutochelezwa,
Ahadi kuitimiza, dunia huwa ni pepo.

Ahadi unapotowa, yangojea kutimizwa,
Thawabu utapewa, duniani utapendwa,
Uwongo ukiutoa, madhambi utavishwa,
Ahadi kuitimiza, dunia huwa ni pepo.

Ndugu ahadi ni deni, kuna msemo wasemwa,
Na asolipa deni, daima atasakamwa,
Abishae ni nani, apinge yalosemwa,
Ahadi kuitimiza, dunia huwa ni pepo.

Ahadi ni hazina, duniani na akhera,
Yaleta mengi mema, kuonekana ni bora,
Utakumbukwa daima, ulalapo akhera,
Ahadi kuitimiza, dunia huwa ni pepo.

Leo nasema hivi, na kesho wabadilisha,
Bure utaota mvi, wacha kujiabisha,
Ahadi ya hivi hivi, motoni utakawilishwa,
Ahadi kuitimiza, dunia huwa ni pepo.

Muhakikishe mwenzako, ndivyo ilivyo dunia,
Uwache urongo wako, kheri utajipatia,
Timiza ahadi zako, usije kuangamia,
Ahadi kuitimiza, dunia huwa ni pepo.

Kaditama washairi, dunia huwa ni pepo,
Eewo ndugu muhariri, ufanye maakuli,
Niwache ninakiiri, chipukizi ndilo hili,
Ahadi kuitimiza, dunia huwa ni pepo.

Athumani A. Kido,
El Baajuny,
Tanga.



Iwe Iddi - Mubaraka

Kwa jina la Rahmani, Ya Illahi Ya Rabuka,
Wa mbingu na ardhini, yu pweke amepwekeka,
Njema zote shukurani, Yeye anawajibika,
Iwe Iddi - Mubaraka, wa mina-lifahizina.

Wa mina-lifahizina, iwe Iddi Mubaraka,
Kwa mabibi na mabwana, wote Makka walofika,
Aidha ajimaina, Mungu alipe baraka,
Iwe Iddi - Mubaraka, wa mina-lifahizina.

Wote walokwenda hiji, kule na huko kutoka,
Kwenye miji na vijiji, India na Amerika,
Urusi China na Fiji, Ulaya na Afrika,
Iwe Iddi - Mubaraka, wa mina-lifahizina.

Zifaulu zao sai, Marwa Swafa kutimka,
Shetani kwa kutumai, eti watu kupotoka,
Kimpate kipapai, fudifudi kuanguka,
Iwe Iddi - Mubaraka, wa mina-lifahizina.

Twaomba Ya Jabari, Mungu wetu mtukuka,
Iwe Hija mabururi, isiyo na shakashaka,
Wao uwalipe kheri, tusokwenda kadhalika,
Iwe Iddi - Mubaraka, wa mina-lifahizina.

Waliokwenda Madina, pale walipomzika,
Tumwa wetu Seyyidina, Muhammad mtajika,
Wape wao Subuhana, kila lenye kupendeza,
Iwe Iddi - Mubaraka, wa mina-lifahizina.

La Muhammad kaburi, naomba kueleweka,
Khalifa Abubakari, karibu yamepangika,
Na la Khalifa Umari, kuzuru yakubalika,
Iwe Iddi - Mubaraka, wa mina-lifahizina.

Mahaji na Mahujaji, tawafu na kuzunguka,
Na kwenda kwao matiti, labeka wakiitika,
Na kupiga jamarati, radhi ya Mungu kutaka,
Iwe Iddi - Mubaraka, wa mina-lifahizina.

Kaditama nilitinde, shairi latamatika,
Waliokwenda washinde, hija iwe muafaka,
Na sisi tuombe twende, nasi tukahiji Makka (Amina)
Iwe Iddi - Mubaraka, wa mina-lifahizina.

(Mshairi - Bora)
Amiri A.S. Andanenga
S.L.P. 4775,
Kinondoni Shamba,
Safarini Mvuti Kijijini - Dar es Salaam.



Ulaji wa dafu

Nakwita Maji ya Ndimu, labeka uniitike,
Kwa swali lako muhimu, imefanya niinuke,
Kukujibu yalazimu, kutojua kukutoke,
Dafu ndivyo kula kwake, kunywa maji kisha nyama.

Kunywa maji kisha nyama, dafu ni hivyo huliwa,
Sababuye ya hekima, hii hapa unapewa,
Kwanza ‘kiu’ kukizima, nyama hula ukipowa,
Dafu inavyotakiwa, kunywa maji kisha nyama.

Dafu ni kitu azali, ndivyo inavyotumika,
maji hunywewa awali, ukisha kuburudika,
Nyama yake hukabili, kilaji cha kupendeka,
Dafu inavyotumika, kunywa maji kisha nyama.

Aidha nakupa usi, maji ya ndimu yashike,
Dafu inavyo halisi, ukivunja maji yake,
Siyo katika gilasi, unywee dafuni mwake,
Dafu ni mwenendo wake, kunywa maji kisha nyama.

Nakwambia yapasayo, madafu yaek dhamiri,
Uanze kupoza moyo, itoweke yote hari,
Mwisho wake nyama ndiyo, ule dafu kwa uzuri,
Dafu yake fakhari, kunywa maji kisha nyama.

Dafu sikio la mbuzi, ni nyama yake laini,
Hilo ni dafu azizi, linalopita kooni,
Linafanya utelezi, halitati abadani,
Dafu ni yake kanuni, kunywa maji kisha nyama.

Na swala la ukwamaji, ajali hailindiki,
Unaweza kwamwa maji, ajali haiepuki,
Ajali usiihoji, kamwe haiepukiki,
Bali ni yake kanuni, kunywa maji kisha nyama.

Isiwe maji ya dafu, utie kwenye kikombe,
Ili uyanywe halafu, nyama kwanza uirambe,
Mwendo utauhalifu, maji yatakuwa pombe,
Dafu ili ulipambe, kunywa maji kisha nyama.

Ubeti huu shairi, usemi wangu nafunga,
Mtungaji ni Amiri, maarufu Andanenga,
Mbora wa Washairi, pembe zote nimezinga,
Dafu katika kupanga, kunywa maji kisha nyama.

Amiri A.S. Andanenga,
S.L.P. 4775,
Kinondoni - Shamba,
Dar es Salaam.



Dama umesema kweli...

Dama umesema kweli, faraja wawe wawili,
Ni ruhusa ya Jalali, kuikwepa udhalili,
‘Wallah’ wake wawili, ni raha sio mithili,
Wake wawili faraja, bora iwe kwa nikaha.

Ameagiza Jalali, Mola mwenye kutukuka,
Tuanzie na wawili, moyo pate burudika,
Watatu pia halali, mwenyewe keshatamka,
Wake wawili faraja, bora iwe  kwa nikaha.

Ukewenza maumbile, ndiyo maana ni faraja,
Mola wetu wa milele, hutujuwa wake waja,
Singeruhusu jambo lile, pasingekuwa na haja,
Dama umesema kweli, faraja wake wawili.

Mke mmoja karaha, kwa mwanamume ‘rijali’,
Roho inakosa raha, kutamani walo mbali,
Tusijinyime furaha, faraja wawe wawili,
Dama umesema kweli, faraja ni ukewenza.

Ni ruhusa ya Muumba, kuoa wake wawili,
Sharti lake ni kwamba, uadilifu wa kweli,
Usiye kuwa mshamba, haki kufanya batili,
Wake wawili faraja,bora iwe kwa nikaha.

Waume hufarijika, wanawake kadhalika,
Aibu  husitirika, mabinti hunusurika,
Jamii uhifadhika, na zinaa hutoweka,
Wake wawili faraja, Dama umesema kweli.

Faraja ukewenza, Dama nakupasulia,
Ni uadilifu kwanza, na siyo kukimbilia,
Unaweza kujiponza, motoni ukatupiliwa,
Wake wawili faraja, bora iwe kwa nikaha.

Mhariri beti nane, sioni pa kuongeza,
Tuwaoe mpaka wanne, Rabbi ameelekeza,
Wembamba pia wanene, hata wenye makengeza,
Wake wawili faraja, Dama umesema kweli.

Said Rajab,
Box 16000,
Dar es Salaam.



Haipo mbali safari, yapasa kujiandaa

Yaillahi Rahmani, Mola uso mshirika,
Mjuzi wa kila fani, wewe ndiwe msifika,
Nijaalie Manani, ujumbe uweze fika,
Haipo mbali safari, yapasa kujiandaa.

Ni mpito duniani, hilo linatambulika,
Kwa mfano majumbani, kwa kweli tumepunguka,
Wanetu na majirani, duniani wametoka,
Haipo mbali safari, yapasa kujiandaa.

Na Mitume kadhalika, mingi imetangulia,
Hawa wailchagulika, kwa Mola wtu Jalia,
Mola hakuacha katu, roho zao kuchukua,
Haipo mbali safari, yapasa kujiandaa.

Yu wapi Adam wetu, Mungu alimjalia,
Na mkewe mama yetu, peponi wakatulia,
Mola hakuacha katu, roho zao kuchukua,
Haipo mbali safari, yapasa kujiandaa.

Nuhu pia yupo wapi, na umri alopewa,
Pia Musa simtupi, na Mungu alijaliwa,
Jabarini mara ngapi, ujumbe alipatiwa,
Haipo mbali safari, yapasa kujiandaa.

Daudi namkumbuka, chuma kwake kukifuwa,
Mikononi akishika, huyuyeka kilikuwa,
Roho yake imetoka, Mola ameichukuwa,
Haipo mbali safari, yapasa kujiandaa.

Muhammd Rasuuli, huyu pia katutoka,
Ni kipenzi cha Jalali, Miraji kampeleka,
Hilo Mungu hakujali, roho yake kaitaka,
Haipo mbali safari, yapasa kujiandaa.

Waislamu wenzangu, tutendeni mambo mema,
Roho kutoka uchungu, tena sana inauma,
Tusije muasi Mungu, motoni atatuchoma,
Haipo mbali safari, yapasa kujiandaa.

Nyoyo zetu ngumu sana, wala hazisikilizi,
Makatazo yake Bwana, yamekuwa simulizi,
Na mifano twapeana, ya adhabu za Mwenyezi,
Haipo mbali safari, yapasa kujiandaa.

Hapa mwisho namaliza, ujumbe wangu mfupi,
Mambo mema kuhimiza, umri wangu mfupi,
Kama tutayapuuza, tutasalimika vipi?
Haipo mbali safari, yapasa kujiandaa.

Hamis M. Rutengo,
Ubungo Islamic High School,
S.L.P. 55105,
Dar es Salaam.
 

Juu RUDI


Bonyeza hapa
kushriki mjadala au kutoa maoni juu ya habari hizi na masuala mengineyo ya Kiislamu kwenye Baraza ya Wasomaji

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtz.org
 
An-nuur Home | Ukurasa wa Mwanzo | Islam Tanzania 
Links | Matoleo Yaliyopita | Sign our Guestbook