Mungu mlaze peponi
Kilio kimetufika, watoto
wa Khalfani,
Kaka yetu katutoka, katuachia
huzuni,
Daima twakukumbuka, akurehemu
Manani,
Marehemu kaka yetu, Mungu
mlaze peponi.
Pemba alikozaliwa, sehemu
za Kikunguni,
Kalelewa akakua, akapelekwa
chuoni,
Elimu akapatiwa, ya kumjua
Manani,
Marehemu kaka yetu, Mungu
mlaze peponi.
Akasomea elimu, ya Kizungu
darasani,
Hadi alipohitimu, masomo
yake shuleni,
Akawaaga walimu, karudi
zake nyumbani,
Marehemu kaka yetu, Mungu
mlaze peponi.
Alioa marehemu, mtoto wa
Selemani,
Jina lake Mariamu, na mtoto
Khalfani,
Awarehemu Rahimu, akhera
na duniani,
Marehemu kaka yetu, Mungu
mlaze peponi.
Ilipofika ahadi, ya kuhama
duniani,
Ikawa hakuna budi, kwenda
kwa Rabi Manani,
Kamchukua Wadudi, yu mgonjwa
kitandani,
Marehemu kaka yetu, Mungu
mlaze peponi.
Amezikwa marehemu, kijijini
Magodini,
Bado tuna kwake hamu, tuwe
nae duniani,
Bali kwa wanaadamu, akhera
ndo maskani,
Marehemu kaka yetu, Mungu
mlaze peponi.
Tunakushukuru nyote, ndugu
pia majirani,
Wa Unguja na wa Wete, mlofika
msibani,
Na rafiki zake wote, mtalipwa
na Manani,
Marehemu kaka yetu, Mungu
mlaze peponi.
Zuena Khalfan Salim,
P.O. Box 5478,
Usagara,
Tanga.
Zuberi jibu pokea, kwa swali
uliuliza,
Nakujulisha sawia, sipendi
kukutatiza,
Majibu yako sikia, wazi
wazi nakweleza,
Shamba hilo lamhusu, yule
alolima kwanza.
Na huyu mtu wa pili, inafaa
tumcheke,
Kafanya kazi thakili, na
shamba wala silake,
Katwaa ya watu mali, akayafanya
ni yake,
Shamba hilo lamhusu, yule
alolima kwanza.
Wa tatu akili hana, kafanana
na wa pili,
Akapalilia sana, akatoka
jasho mwili,
Mazoeya yakafana, shamba
kwake si halali
Shamba hilo lamhusu, yule
alolima kwanza.
Mwenye haki ni wa kwanza,
kama nilivyobaini,
Ndie yeye aloanza, kulima
hapo shambani,
Kufungwa kwake si manza,
kwa kuwekwa gerezani,
Shamba hilo lamhusu, yule
alolima kwanza.
Wawili ni wavamizi, kupora
haki ya watu,
Wanastahili wizi, adhabu
imethubutu,
Ni ya bure yao kazi, malipo
hawana katu,
Shamba hilo lamhusu, yule
alolima kwanza.
Nimefika kwenye safu, tamati
kwa kuandika,
Ndugu usiwe na khofu, moyoni
kuhuzunika,
Soma kwa ukamilifu, nadhani
utatosheka,
Shamba hilo lamhusu, yule
alolima kwanza.
Suleiman Khamis
P.O. Box 571,
Arusha,
Tanzania.
Si kila kilo kinono, kipanuliwe
mdomo,
Vyengine vina ndoano, vitakuziba
mdomo,
Tena jihadharini mno, wazi
kuweka mdomo,
Chakula chenye ndoano, kitakuziba
mdomo.
Ya kwangu haya maono, nimepima
kwa kipimo,
Dhalimu mbaya mno, achimba
yake mashimo,
Akukite kisigizo, ukatumbukie
humo,
Chakula chenye ndoano, kitakuziba
mdomo.
Hatoi bure vinono, zingatia
hili somo,
Hataki mshikamano, kuwepo
na msimamo,
Akutega kwa ndoano, upigepige
midomo,
Chakula chenye ndoano, kitakuziba
mdomo.
Ndugu usiwe mfano, baada
ya hili somo,
Usirukie vinono, ukaja kwenda
mchomo,
Nimetafakari mno, nasema
kwa mtizamo,
Chakula chenye ndoano, kitakuziba
mdomo.
Hasa kwenye mapambano, yahitaji
msimamo,
Mibaya mifarakano, jengo
yabomoa bomo,
Mafunzo ya sala tano, yajenge
wetu mfumo,
Chakula chenye ndoano, kitakuziba
mdomo.
Nyuma rudisha mikono, wako
zuia mdomo,
Yakate mahusiano, sijali
zake ngurumo,
Akitaka michuano, mtupie
misukumo,
Chakula chenye ndoano, kitakuziba
mdomo.
Nakoma kuwamba wino, nimekwisha
toa somo,
Nakoma yangu maneno, yapimwe
kimtazamo,
Nakoma onyo vinono, uchunge
wako mdomo,
Chakula chenye ndoano, kitakuziba
mdomo.
IDD S. Kikong’ona,
Morogoro.
Bismillahi naanza, kwa jina
la Mola wetu,
Ambaye dniye wa kwanza,
hilo halipingwi katu,
Elimu ametufunza, hakuacha
hata kitu,
Serikali hii vipi, mbona
haitendi haki.
Matukio mbalimbali, yenyewe
yasababisha,
Kisha inaruka mbali, ukweli
kuupotosha,
Inajifanya ukali, kwa kauli
za kutisha,
Serikali hii vipi, mbona
haitendi haki.
Mfano Mwembechai, vurugu
ilianzisha,
Harafu ikajidai, uongo kuvumisha,
Ilijifanya ni chui, mabomu
kuyatupisha,
Serikali hii vipi, mbona
haitendi haki.
Iliuwa Islamu, kwa makusudi
hakika,
Kwa risasi na mabomu, roho
za watu kutoka,
Harafu inashutumu, eti haikuhusika,
Serikali hii vipi, mbona
haitendi haki.
Nguruwe sasa halali, hilo
wamelitamka,
Kufugwa kila mahali, mtu
anapopataka,
Bila hata ya kujali, mipaka
waliyoweka,
Serikali hii vipi, mbona
haitendi haki.
“Kiti Moto” mabuchani, hilo
halivumiliki,
kuuzwa hadi sokoni, Isilamu
hatutaki,
Mtasema ni udini, hilo hatuliafiki,
Serikali hii vipi, mbona
haitendi haki.
Sasa ni mtasema, kuhusu hizi
hijabu,
Ni mavazi ya heshima, katuamuru
Wahabu,
Kwa mwanamke lazima, kulivaa
si ajabu,
Serikali hii vipi, mbona
haitendi haki.
Hapa mwisho ninakoma, mbele
sitaendelea,
Islamu hima hima, serikali
twaijua,
Tusiregee daima, itakuja
kutuua,
Serikali hii vipi, mbona
haitendi haki.
Hamisi M. Rugengo,
Ubungo Islamic High School,
S.L.P. 55105,
Dar es Salaam.
Natafakari bunduki, kulengwa
kwa kijana Chuki,
Moyoni sifurahiki, upumbavu
siutaki,
Sipendipendi muziki, vichupi
na ushabiki,
Iwache yako dhihaki, sipumbazwi
kwa muziki.
Tena nasema sitaki, mipango
ya kishabiki,
Jazba zenye mikiki, za kimuziki
muziki,
Upambe na chukichuki, usinifanye
rafiki,
Iwache yako dhihaki, sipumbazwi
kwa muziki.
Nyimbo nyimbo sishiriki,
kwangu hazistahiki,
Kwa upambe sipambiki, nawapasha
halaiki,
Usije kujenga chuki, vipi
kwangu hupendeki,
Iwache yako dhihaki, sipumbazwi
kwa muziki.
Bora nikamate chaki, au nicheze
na biki,
Niwaseme wenye chuki, walotupiga
bunduki,
Upotee ufisasikia, dhuluma
haki ibaki,
Iwache yako dhihaki, sipumbazwi
kwa muziki.
Nataka niwashitaki, walouwa
bila haki,
Mpaka itendeke haki, walouwa
wahaliki,
Jahadi haizimiki, kwa vishindo
vya bunduki,
Iwache yako dhihaki, sipumbazwi
kwa muziki.
Siupendi unafiki, na kufanywa
mamluki,
Ikiwa huambiliki, utakong’otwa
kwa biki,
Usije ukahamaki, gazeti
kulishitaki,
Iwache yako dhihaki, sipumbazwi
kwa muziki.
Tambua sibadiliki, kwa vinyimbo
na miziki,
Naitaka yangu haki, nipate
kuimiliki,
Mikononi idiriki, si huku
kunidhihaki,
Iwache yako dhihaki, sipumbazwi
kwa muziki.
Ulingo nautariki, nyimbo
miziki sitaki,
Ulingo nataka haki, agendani
sibanduki,
Ulingo naweka biki, mekasirika
sicheki,
Iwache yako dhihaki, sipumbazwi
kwa muziki.
Idd S. Kikong’ona,
Morogoro.
Naona ni adhuhuri, mchana
wa jua kali,
Imekuwa ni vizuri, kuwaulizeni
swali,
Sitakuwa na kiburi, jibu
nitalikubali,
Linalosomwa Bungeni, ni
dua la dini ipi?
Husomwa kwa lugha nzuri,
na unyenyekevu kweli,
Wabunge hukaa turi, wakiwa
wanakubali,
Kikao huwa kizuri, likisha
somwa awali,
Linalosomwa Bungeni, ni
dua la dini ipi?
Nchi hii ipo huri, dini si
za serikali,
Ajabu inashamiri, dua kusomwa
halali,
Au ni masihari, wapagani
wanasali,
Linalosomwa Bungeni, ni
dua la dini ipi?
Msekwa ni mlozari, hilo mimi
silijali,
Vipi hii Jamhuri, ndio muje
kujadili,
Nataka mutafakari, Bungeni
wanakosali,
Linalosomwa Bungeni, ni
dua la dini ipi?
Dodoma mnishauri, pamoja
nanyi wa mbali,
Nataka watu mahiri, wamchao
Mungu kweli,
Majibu kwa Mhariri, wa AN-NUUR
jabali,
Linalosomwa Bungeni, ni
dua la dini ipi?
Kwangu mimi si vizuri, kuombewa
na jahili,
Mungu kwake ni sifuri, hamfahamu
wa kweli,
Vipi iwe desituri, Wabunge
mnakubali,
Linalosomwa Bungeni, ni
dua la dini ipi?
Huwa halisomwi siri, Redioni
kunakili,
Kipindi kikiwasiri, utafikiri
maswali,
Leo katika Bungeni, Wabunge
wanajadili,
Linalosomwa Bungeni, ni
dua la dini ipi?
Hapa mwisho wa shairi, njoo
Dettu Muinjili,
Nijibuni si zohari, wote
wake na rijali,
Nitakuwa na fahari, jibu
likiwa kamili,
Linalosomwa Bungeni, ni
dua la dini ipi?
Zuberi Mohammed Mwinyi
(Amir),
S.L.P. 61428,
Dar es Salaam.
|
|