MASHAIRI
 

Kuna jambo latafutwa

Simanzi zimenishika, Ponda kusakwa nchini,
Mikono yatetemeka, nashindwa kushika peni,
Amekuwa kama paka, mwizi wa nyama jikoni,
Kuna jambo latafutwa, ukweli kuupotosha.

Kwake kusema ukweli, kumekuwa uchochezi,
Atafutwa kweli kweli, kuliko hata jambazi,
Lengo kubwa kubadili, ukweli ulio wazi,
Kuna jambo latafutwa, ukweli kuupotosha.

Lengo lao si zuri, hilo nimelibaini,
Rundo la maaskari, walijaa Mtambani,
Wengine kwenye magari, na bunduki mabegani,
Kuna jambo latafutwa, ukweli kuupotosha.

Awe hai wamesema, au mfu wamtaka,
Askari hima hima, sasa wanahangaika,
Kweli kuna usalama, siku watayomshika?
Kuna jambo latafutwa, ukweli kuupotosha.

Anaachwa mchochezi, vifo alosababisha,
Tena huku wamuenzi, kama kawafurahisha,
Kumbe kaacha majonzi, nyoyoni yatukondesha,
Kuna jambo latafutwa, ukweli kuupotosha.

“Piga huyu piga yule”, kauli ilisikika,
Askari mteule, kauli akaitika,
Aliuwa pale pale, wale aliowataka,
Kuna jambo latafutwa, ukweli kuupotosha.

Hawa hawana makosa, huru wameachiliwa,
Wanapita “wakitesa”, bila ya kusumbuliwa,
Atafutwa asokosa, hatiani anatiwa,
Kuna jambo latafutwa, ukweli kuupotosha.

Hapa mwisho kituoni, peni ninaachilia,
Islamu chunguzeni, ukweli kuugundua,
Ponda yupo msakoni, yapo “maiti” sheria?
Kuna jambo latafutwa, ukweli kuupotosha.

Hamisi M. Rutengo,
Ubungo Islamic High School,
P.O. Box 55105,
Dar es Salaam.



“Mchumba”

Bismillahi awali, kwa jina lako Karima,
Ninakuomba mwalali, tena kwa taadhima,
Ambaye wasitahili, dua kwangu kulisema,
Mola wangu nakuomba, nijalie mke mwema.

Atoke pande za kwetu, hata kama ugenini,
Kilicho bora ni utu, ndicho kilicho thamani,
Walio roho za kutu, Rabi waweke pembeni,
Mola wangu nakuomba, nijalie mke mwema.

Isilamu yangu dini, na wala siyo pagani,
Mke wangu kuamini, isiwe ni ubishani,
Asije kufanya kani, miye tamuona duni,
Mola wangu nakuomba, nijalie mke mwema.

Nijalie ewe Mola, roho yangu itulie,
Upweke kwangu madhila, hapa usiishilie,
Unalingana na jela, ni nani akimbilie,
Mola wangu nakuomba, nijalie mke mwema.

Picha na barua zenu, wenye sifa zitumeni,
Nina haja si fununu, namtafuta mwandani,
Ndoa si jambo la tunu, ni sheria ya Manani,
Mola wangu nakuomba, nijalie mke mwema.

Arubaini na moja, miaka nimeshatimu,
Msije kujenga hoja, utuli wanilazimu,
Kuowa japo mmoja, Mola wangu nikarimu,
Mola wangu nakuomba, nijalie mke mwema.

Beti saba nashiliza, machache  haya yanatosha,
Mola nifutie kiza, taa njema kwangu washa,
Naomba nisikiliza, upweke kuniondosha,
Mola wangu nakuomba, nijalie mke mwema.

Khamis Lali Pashua (Mwangwena)
Kijiji cha Mavumbi Pande,
S.L.P. 5332,
Tanga.



Dua Bungeni (jibu)

Walishasema wahenga, kuuliza si ujinga,
Zuberi wataka mwanga, swali lako sitapinga,
Majibu sasa napanga, kusudi upate mwanga,
Mungu yeye ni wa wote, dua za dini ni zako.

Wapumbavu duniani, ni wasomjua Mungu,
Kwanza wao wanadhani, kwamba hakuna Mungu,
Bunge letu ni makini, mambo huanza na Mungu,
Mungu yeye ni wa wote, dua za dini ni zako.

Aleta jua na mvua, kwa wema na wachawi,
Na hapendi kubagua, japo hapendi uchawi,
Wote anawatambua, awapenda wastani,
Mungu yeye ni wa wote, dua za dini ni zako.

Wabunge hawana dini, lakini wanaye Mungu,
Kuwavisha upagani, Zuberi umekufuru,
Waweza kuwa na dini, lakini ukakosa Mungu,
Mungu yeye ni wa wote, dua za dini ni zako.

Dua za dini ni nini, hata shetani anazo,
Kwanza kaanzisha dini, aomba mfululizo,
Tena akiwa gizani, kwake hafanyi mchezo,
Mungu yeye ni wa wote, dua za dini ni zako.

Tamati natamatisha, wenye macho wameona,
Dunia sasa yaisha, tusibaki kubishana,
Tuyaandae maisha, kwa kumuabudu BWANA,
BWANA Mungu ni wa wote, wamwombao kwa imani.

Mwinjilisti B.E. Dettu,
S.L.P. 60474,
Dar es Salaam.



Malenga niambieni

Allah aliye Alimu, naja kwako nikirimu,
Unipatie mwalimu, anifunze nifahamu,
Kwenye sira ya Hashimu, huyu Abali Kasimu,
Mafundisho ya muhimu, nipate kuyafahamu.

Jamii yake Nabia, gizani alizamia,
Dhuluma iliwajaa, haki waliipotoa,
Nuru iliwakimbia, njia wakipotea,
Twafautiana nini, malenga niambieni.

Allahu mwenye uwezo, katoa maelekezo,
Kwenye wake mwongozo, kwamba Nabia kigezo,
Awe ni kielelezo, kinachotoa mafunzo,
Ili pasiwe kikwazo, tukafuata uozo,

Tangu utotoni mwake, machafu hakufahamu,
Hakupata uso wake, kuabudia sanamu,
Mkweli wasifu wake, watu walimuheshimu,
Nipeni fundisho lake, malenga nawaombeni.

Biashara kaifanya, alipokuwa kijana,
Dhuluma hakuifanya, wateja walijazana,
Hakuweza kudanganya, apate kuuza sana,
Hapa kuna funzo gani, malenga niambieni.

Kwa uaminifu wake, watu walimthamini,
Kwa ule ukweli wake, watu walimwamini,
Kweli waliweka kwake, vitu vyao vya thamani,
Kipi twajifunza kwake, malenga niambieni.

Moyoni aliungua, dhuluma kutoridhia,
Kutwa alifikiria, namna ya kuing’oa,
Mapesa alitumia, watumwa kuwakomboa,
Tunapata funzo gani, malenga niambieni.

Chamani akaingia, cha wanyonge kutetea,
Apate kupigania, wanyonge kuwaokoa,
Haki wapate kupewa, utu wao kuinua,
Hapa twajifunza nini, malenga niambieni.

Matatizo ya jamii, yeye hakuyamezea,
Machafu kwenye jamii, hakuwa kayaridhia,
Mejitenga na jamii, dawa kuyatafutia,
Twajifunza kitu gani, malenga niambieni.

Dini za wakati ule, yeye alizikataa,
Dhuluma za wateule, macho ziliyafumbia,
Mejaa uongo tele, wakubwa zawatetea,
Hapa kuna funzo gani, malenga niambieni.

Pangoni kaelekea, mlima Jabar Hira,
Jibrili kamjia, ZANA akampatia,
Karudi kwenye jamia, maovu kuyafyagia,
Hapa twavuna nini, malenga niambieni.

Bado ninajisomea, sira ya wetu Nabia,
Pale nisipoelewa, malenga nitawajia,
Maswali tawatupia, ili nipate kujua,
Hapa sasa natulia, majibu natarajia.

Idd S. Kikong’ona,
Morogoro.



Mungu mmoja dini moja (jibu)

Bwana Meena hujambo, Dettu ninakusalimu,
Mungu anilinda sijambo, na wanangu nawakimu,
Umeniletea jambo, wataka niwe hakimu,
Nami sisemi kwa fumbo, nakujibu ya muhimu,
Mungu wetu ni mmoja, aloumba mbingu na nchi.

NAFSI tatu sihofu, siwaze kibinadamu,
Akili zetu hafifu, kuelewa ya muhimu,
Kwanza tumejaa hofu, ya Mungu hatufahamu,
Hata tunavyomsifu, ni kama wendawazimu,
Mungu wetu ni mmoja, Muumba wa mbingu na nchi.

Ona mkono mmoja, una vidole vitano!
Bado mkono mmoja, na si mikono mitano,
Vipi mkono mmoja, useme ipo mitano?
Kwetu Mungu ni mmoja, ndiye mwisho wa maneno,
Mungu wetu ni mmoja, Muumba wa mbingu na nchi.

Wewe unawaza sokoni, kwenye mafungu ya nyama,
Kisha waleta mizani, kumpanga kama nyanya!
Tuna wasema kwa nini, yu mafungu kama nyanya,
Hivyo Mungu hamuoni, taona mafungu ya nyanya!
Mungu wetu ni mmoja, Muumba wa mbingu na nchi.

Na ndiye huyo mmoja, aliyefanya Sabato,
Mungu moja Dini moja, katuwekea Sabato,
Jumamosi ya faraja, tufurahi na Sabato,
Na hiyo haina hoja, yake BWANA wa Sabato,
Mungu wetu ni mmoja, Muumba wa mbingu na nchi.

Huyu Mungu wa Rehema, si Mungu wa kujadili,
Bora tu nimesema, machache yenye adili,
Ilimpasa kusema, kukujibu lako swali,
Basi miye nasimama, nenda Pasaka kusali,
Mungu wetu ni mmoja, Muumba wa mbingu na nchi.

Mwinjilisti B.E. Dettu,
S.L.P. 60474,
Dar es Salaam.



Mauwa Mbwana

Maulana yarabuka, Mola ulie mbinguni,
Kila unalitaka, hakuna wa upinzani,
Mauwa kakuitika, hayuko ulimwenguni,
Mlaze pema peponi, Mauwa Mbwana Ngowa.

Siku aliyoandika, lipofika kasaini,
Ndipo alipoitika, akatutoka machoni,
Nasi zetu zikifika, twaja huko masikani,
Mlaze pema peponi, Mauwa Mbwana Ngowa.

Likuwa mswali hina, kutwa mpaka jioni,
Funga zote paka suna, alizifunga yakini,
Ee Mola Maulana, mama mweke peponi,
Mlaze pema peponi, Mauwa Mbwana Ngowa.

Mazoeya ni mabaya, Ngare tamwambia nani,
Mema ama mabaya, nikienda Bomandani,
Sasa nitawayawaya, nipeni  pole jamani,
Mlaze pema peponi, Mauwa Mbwana Ngowa.

Ombi nakuomba Mola, siwaombi mashetani,
Mauwa alipolala, pajengee busitani,
Na siku ya palapala, awe mbali na motoni,
Mlaze pema peponi, Mauwa Mbwana Ngowa.

Nyuma kaacha watoto, waume na wana ndani,
Na wajukuu tomito, watiaji wa ubani,
Mke wangu ni mtoto, wa tano mwao tumboni,
Mlaze pema peponi, Mauwa Mbwana Ngowa.

Namba saba naishia, naofia gazetini,
Ningetunga beti mia, wenzangu ningewahini,
Hili pia nahofia, litachakaa kapuni,
Mlaze pema peponi, Mauwa Mbwana Ngowa.

J.S. Ngare (Liwalo),
P.O. Gombero,
Tanga.
 

Juu RUDI


Bonyeza hapa
kushriki mjadala au kutoa maoni juu ya habari hizi na masuala mengineyo ya Kiislamu kwenye Baraza ya Wasomaji

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtz.org
 
An-nuur Home | Ukurasa wa Mwanzo | Islam Tanzania 
Links | Matoleo Yaliyopita | Sign our Guestbook