MAKALA
Usafi na mafundisho ya Uislamu

Na Mwl. Zuhura Tajiri

UISLAMU, dini ya Allah (s.w.) iliyotimia, haukuacha kuzungumzia na kufundisha juu ya kipengele hiki muhimu sana katika maisha ya mwanadamu. Maagizo ya Mtume (s.a.w.) juu ya suala hili yanasema wazi kuwa; "Uislamu ni usafi, basi jisafisheni, kwa hakika hatoingia mtu peponi ila yule msafi".

Hata hivyo neno "Usafi" lina mana pana sana. Kwa mujibu wa mafundisho ya Uislamu tunaweza kuugawa usafi katika maana mbili, kwanza usafi wa nje na pili usafi wa ndani (usafi wa moyo).

Usafi wa nje ni ule unaohusisha mavazi, kiwiliwili na mazingira yote anayoishi mwanadamu pamoja na yale yanayozungumzwa. Tabia ya usafi au unadhifu ni tabia iliyo na athari sana kwa watu, ni tabia yenye mvuto mkubwa kiasi kwamba kwa kulijua hili baadhi ya watu hutumia unadhifu wao kufikia malengo yao mbalimbali.

Ndiyo ukaona mvulana anajitahidi sana kuwa nadhifu muda mwingi wakati akichumbia na binti nae kuwa hivyo hivyo wakati akichumbiwa, ndiyo ukaona vile vile akina changudoa wakioga vizuri, wakajikwatua na kuvalia kwa unadhifu sana pamoja na kujitia manukato makali tayari kwa mawindo yao, ndiyo hata ukaona wezi na matapeli wakavalia vizuri katika hali ya unadhifu ili isiwe rahisi kwa watu kuwafikiria kuwa ni watu wabaya, na ndiyo vile vile ikawa mtu nadhifu na yule aliyevalia ovyo ovyo wakienda pamoja kukopa mahali, basi ataaminiwa zaidi kupewa mkopo yule aliye nadhifu. Hii ndiyo faida ya usafi na hata watu wabaya wakaitumia kama silaha katika kufikia waliyoyakusudia.

Faida nyingine ya usafi wa aina hii ni ile ya kuepukana na maradhi mbalimbali yanayomtaabisha mwanadamu kutokana na kukithirisha kwake uchafu katika mazingira anayoishi. Kampeni mbalimbali za kusafisha mazingira dhidi ya kipindupindu, kuhara damu na maradhi mengine yasababishwayo na uchafu ni kama tu utekelezaji wa mafundisho ya Uislamu kwani dini hii imelihimiza sana hili katika mafundisho yake.

Waislamu kwa mujibu wa mafundisho yao hawatakiwi kusubiri kuzinduliwa kwa kampeni za usafi baada ya milipuko ya maradhi kutokea, hawatakiwi kusafisha mazingira ya nyumba zao na miji yao kwa ajili ya mwenge au ziara ya Waziri Mkuu wala hawatakiwi na hasa si stahili yao kusafisha mazingira yao kwa kusimamiwa na mgambo au mkuu wa wilaya. Wao wanatakiwa wawe ndio watu wa mwanzo kuwahimiza wengine juu ya faida ya usafi.

Faida nyingine ya usafi huu ni ukweli kwamba usafi au unadhifu ni "nanga" imara sana katika maisha ya ndoa, kina mama na hasa kina mama wa Kiislamu wanizingatie vyema hapa. Usafi humfanya mke kuwa na mvuto kwa mume na kinyume chake na hivyo kustawisha na kudumisha mapenzi baina yao. Nadhafa ya mke, watoto na mazingira ya nyumba kwa ujumla ni silaha muhimu sana ya kumfanya mume awe ni mtu wa kufikiria kurudi nyumbani mapema hasa inapokuwa keshama.ilza majukumu yake ya nje kwa siku.

Usafi huliwaza na kuchangia kwa kiasi kikubwa kuleta utulivu katika maisha ya ndoa.

Nadhani wanafanya makosa sana wale wanawake ambao huvaa vizuri na hata wengine kujidodeka manukato wakati wanapotoka kwenda makazini kwao hali ya kuwa warejeapo majumbani baada ya kazi "hujipamba" kwa khanga na vitenge vilivyochoka kwa ajili ya waume zao. Hata hivyo wanaume nao wajue kuwa huu ni wajibu wa wote. Ili maisha yaende vyema ni lazima mvuto na utulivu vipatikane pande zote mbili. Wanawake nao hupenda na kuona fahari kwa mumewe kuonekana nadhifu muda wote na kwa mwanamke anayelijua hili hatoacha "kumkera" mumewe kwa maji ya kuoga kila atokapo na kurudi, atahakikisha kuwa nguo za mumewe ni safi kila wakati na hata kumchagulia nguo gani ya kuvaa wakati wa kutoka. ]

Na ndiyo maana vile vile Uislamu ukahimiza watu wachukue mapambo (nguo nzuri) wakati wa kwenda Msikitini na kujitia manukato (kwa waliofaradhiwa jamaa Msikitini) ili kuondoa kero zinazoweza kusababishwa na uchafu wa mwili na nguo wakati wa swala, hivyo kuharibu utulivu wa kiibada na mahusiano mazuri ambayo hujengeka kwa kuswali pamoja Msikitini.

Ni vyema basi kwa umuhimu huu wa usafi katika Uislamu, kila familia ya Kiislamu ijitahidi kutenga bajeti maalumu kwa ajili ya masuala ya usafi kwa ujumla na kuhimizana na kukumbushana mara kwa mara kuhusu umuhimu wa usafi katika maisha yetu ya kila siku.

Usafi kwa maana ya pili ni ule usafi wa ndani, usafi wa moyo ambao unatokana na itikadi safi na sahihi. Itikadi ya kuamini Mungu mmoja asiye mfano, mwana wala baba. Matunda ya usafi huu huonekana kwa tabia njema zinazoupamba utu. Uaminifu, ukweli, kujiheshimu, kutojivuna, kutokuwaringia watu, kuwasaidia wenye shida, kuwatendea wema watu wengine, kuwafikiria watu wengine vizuri na tabia nyingine zote nzuri ni matokeo ya usafi huu wa ndani.

Usafi wa aina hii tu ndio utakaoiweka dunia katika hali ya usalama na amani. Aidha, kukosekana kwake ndiko kulikoitumbukiza dunia katika machafuko na misukosuko isiyokwisha ya vita vya wenyewe kwa wenyewe, mauaji ya kinyama na dhulma kama yale ya Soweto, Rwanda, Burundi, Liberia, Somalia, Mwembechai, Bosnia, Kosovo na kwingineko kwingi tu katika ulimwengu huu.

Watawala na watu wao katika nchi hizo kwa tamaa zao, choyo chao na chuki zao juu ya watu wengine ndivyo vinavyoihilikisha dunia hasa tangia pale wale wenye itikadi safi na sahihi walipopokonywa khatamu za kuiongoza dunia.

Wapo watu tulioambiwa kuwa wao ni watu safi sana na hivyo ndio wanaofaa kutuongoza. Tukashangilia na kuzunguka huku na huku kuwanadi kwa wenzetu ili wachaguliwe, na walichaguliwa bila shaka. Usafi tulioambiwa tulitegemea kuuona katika utekelezaji wa ahadi walizotoa zionyeshazo kuwa raia wote katika nchi yetu ni sawa na wana haki inayolingana.

Bahati mbaya sana usafi unaojulikana na wao si huu tuujuao siye. Usafi katika mioyo yao ambayo imeridhia kwa furaha kabisa binadamu wenzao kuuawa kwa kulengwa risasi hadharani, usafi katika mioyo yao ambayo imeridhia wanawake wadhalilishwe hadharani na kuvuliwa nguo zao na wanamume, usafi wa mioyo yao unaotambulika kwa kuwatesa Waislamu na hata wengine kufia gerezani, usafi ambao unaonekana kwa kuwavunjia watu nyumba zao na kuwacha wakishangaa kwa majonzi chini ya miti bila kujua cha kufanya, hawa ndio wasafi tulioambiwa na hayo ndiyo mapenzi na huruma kwa raia inayotokana na usafi wao!

Elfu mbili panapo majaliwa si mbali na bila shaka washaanza kuandaliwa wasafi wengine. Uislamu umeshafundisha usafi wa kweli na tunaujua, lakini ole wetu tuje tuisahau tafsiri sahihi ya usafi kwa baiskeli, pea za khanga na sahani za pilau, tusije tukaulizana imekuwaje!
 

Juu RUDI


Bonyeza hapa
kushriki mjadala au kutoa maoni juu ya habari hizi na masuala mengineyo ya Kiislamu kwenye Baraza ya Wasomaji

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtz.org
 
An-nuur Home | Ukurasa wa Mwanzo | Islam Tanzania 
Links | Matoleo Yaliyopita | Sign our Guestbook