MASHAIRI
 

Dhibiti yangu maguvu

Allah wewe una nguvu, umeniumba kiumbe,
Wangu ujana na nguvu, visinioteshe pembe,
Vikanipa ukomavu, kudhuru wako viumbe,
Dhibiti yangu maguvu, ujana usinishinde.

Allah umrehemevu, nakuita unilinde,
Unikinge na maovu, nisije kwenda upande,
Nifanye niwe shupavu, mabaya nisiyapende,
Dhibiti yangu maguvu, ujana usinishinde.

Nichukize na mabovu, hata kama wayapambe,
 Nipambane na waovu, na wale wao wapambe,
Nivunje yao mabavu, niwazime wasitambe,
Dhibiti yangu maguvu, ujana usinishinde.

Ya kwangu haya maguvu, yafanye haki itendwe,
Wanyonge waso na nguvu, kwa zangu nguvu walindwe,
Masikini walemavu, wote hawa wanipende,
Dhibiti yangu maguvu, ujana usinishinde.

Nifanye mnyenyekevu, yalomema niyatende,
Niwe na fikra pevu, ziongoze ummah wende,
Niwe kijana mwerevu, na stadi nizipende,
Dhibiti yangu maguvu, ujana usinishinde.

Nifanye mkakamavu, vita nipige uzembe,
Nisifanye ulegevu, wako kufata ujumbe,
Nikitoka mvi ndevu, nyingi hekima nipambe,
Dhibiti yangu maguvu, ujana usinishinde.

Niwe mtu msikivu, machafu nipige pande,
Nifunike utulivu, jazba zitoke zende,
Nilinde na upumbavu, kwangu usiranderande,
Dhibiti yangu maguvu, ujana usinishinde.

Madhalimu wapotevu, niwatwange kwa vijembe,
Uwakamate uchovu, wazidiwe ndembendembe,
Yakome yao mabavu, kudhuru wako viumbe,
Dhibiti yangu maguvu, ujana usinishinde.

Nipe mwenza mtulivu, anilinde nimlinde,
Aliye mvumilivu, mitihani aishinde,
Kizazi chenye wakovu, akifunze kisipinde,
Dhibiti yangu maguvu, ujana usinishinde.

Aniamshe kwa nguvu, visimamo tujipinde,
Usiku ulo mpevu, ili Allah atupende,
Tuswali kinyenyekevu, atupe nguvu tushinde,
Dhibiti yangu maguvu, ujana usinishinde.

Nyumba iso na mabavu, ya kupotosha viumbe,
Ing’are kama mapovu, meupe yaso na chembe,
Iuzime upotevu, kwa nuru giza lifumbe,
Dhibiti yangu maguvu, ujana usinishinde.

Zangu pumzi na nguvu, kwa wema zishe niende,
Itoke kwa utulivu, roho mwili usidunde,
Nisitajwe kwa maovu, nyuma mema yayashinde,
Dhibiti yangu maguvu, ujana usinishinde.

Allah wamiliki nguvu, kwa jihadi unipambe,
Washeheneze maguvu, Wajahidi wasiyumbe,
Wawashinde wapotevu, wenye akili za pombe,
Dhibiti yangu maguvu, ujana usinishinde.

Peni inakuwa kavu, nakoma mbele nisende,
Na waasa wanyenyekevu, dhulma msiitende,
Allah anateza nguvu, atawavunja vipande,
Dhibiti yangu maguvu, ujana usinishinde.

Said Ally Mubaraka Soud (Mzee wa Shaksiyya)
Ubungo Islamic College of Education,
S.L.P. 55105,
Dar es Salaam.


Vazi lenye heshima

Bismillahi naanza, kutoa yangu maoni,
Kwa baraka za Muweza, ya Karima ya Manani,
Kwa kalamu nacharaza, kwa moyo wenye imani,
Buibui natamka, ni vazi lenye heshima.

Mungu ni mwenye busara, na hekima teletele,
Katuwekea ishara, tujue nyuma na mbele,
Sharia yake imara, kabisa haina ndele,
Buibui natamka, ni vazi lenye heshima.

Enyi wake watiifu, msifunge masikio,
Sifuati uzandifu, kisha takuwa kilio,
Wala dini sikashifu, andama yote yalio,
Buibui natamka, ni vazi lenye heshima.

Miaka tisa kitimu, uchanga ushakimbia,
Fuata njema elimu, Kurani ilotimia,
Wazee wako heshimu, sikia wanakwambia,
Buibui natamka, ni vazi lenye heshima.

Mungu amewatukuza, wanawake Islamu,
Kawatoa kwenye kiza, kuwaonya ya haramu,
Mwili kujifunikiza, Ni sheria mufahamu,
Buibui natamka, ni vazi lenye heshima.

Mola huwapenda waja, wenye kuandama ndia,
Cheo cha mtu si hoja, ikiwa hana sheria,
Amini Mungu mmoja, Mola takuangalia,
Buibui natamka, ni vazi lenye heshima.

Sijifanyi hayawani, kuwa kiguu na ndia,
Ukosefu wa imani, jeuri kupakilia,
Tuputupu manjiani, watu kushangilia,
Buibui natamka, ni vazi lenye heshima.

Na tabia angalia, sikuzunguke na kelele,
Maguu kupigilia, jitembeze pole pole,
Upuuzi si tabia, na maasi yastole,
Buibui natamka, ni vazi lenye heshima.

Mola tuongeze njia, tufate yalo ya kheri,
Tufuate ya sheria, tujikinge na ya shari,
Mema kuyashikiria, tuwe Islamu kweli,
Buibui natamka, ni vazi lenye heshima.

Kabola J. Sokwa,
Ubungo Islamic High School,
S.L.P. 55105,
Dar es Salaam.



Mwaka mpya umefika 1420 AH

Bismillahi naanza, naingia mitamboni,
Nilo nayo kueleza, msikize kwa makini,
Huenda mkajifunza, kupitia shairini,
Mwaka mpya umefika, sote tuupokeeni.

La mgambo limelia, toka bara hadi pwani,
Mwaka mpya kuwadia, hapa petu duniani,
Ni elfu nne mia, na ishirini yakini,
Mwaka mpya umefika, sote tuupokeeni.

Elfu na mia nne, pamoja na ishirini,
Kwenye mema tuungane, mabaya tuyahameni,
Na wala tusigombane, katika mambo ya dini,
Mwaka mpya umefika, sote tuupokeeni.

Bora tushukuru Mungu, ikiwa tuna imani,
Kwa rehema zake Mungu, bado tupo duniani,
Ni wangapi walimwengu, wametoweka machoni,
Mwaka mpya umefika, sote tuupokeeni.

Mema tuyatafakari, ya mwaka jana jamani,
Pamoja na kukhiyari, kuyadumisha yakini,
Dhambi kustaghfari, kwa kutubu kwa Manani,
Mwaka mpya umefika, sote tuupokeeni.

Tuupokee kwa wema, sote tuwe furahani,
Kwa kula vilivyo vyema, na vinywaji majumbani,
Kupongezana ni vyema, ulevi tusithamini,
Mwaka mpya umefika, sote tuupokeeni.

Nimelitunga shairi, ili tuwe furahani,
Mwaka mpya umejiri, mwaka wetu waumini,
Wa kuhama Mukhtari, kwenda Madina mjini,
Mwaka mpya umefika, sote tuupokeeni.

Shairi nimelitunga,  kupitia gazetini,
Ambalo hutupa mwanga, kwa amri ya Manani,
Mtume kwambiwa anga, safari na waumini,
Mwaka mpya umefika, sote tuupokeeni.

Mtume kutoka Makka, kuhamia ugenini,
Na Madina akafika, akakaa kwa amani,
Ndipo ikakubalika, kalenda yetu ya dini,
Mwaka mpya umefika, sote tuupokeeni.

Alipofika Madina, walimngoja njiani,
Kwa mashairi kunena, umechomoza langoni,
Karibu kwetu Madina, tunakupa shukrani,
Mwaka mpya umefika, sote tuupokeeni.

Mwisho ninasisitiza, Mungu tumuogopeni,
Atakayo kutimiza, mawi kuweka pembeni,
Kwa wema kuzungumza, na wenzetu duniani,
Mwaka mpya umefika, sote tuupokeeni.

Twalaal Badru Alayna, Min Thaniyyaatil Wadai,
Wajabash Shukru Alayna, Madaalillaahi Dai,
Ayyuhal Mab Uthu Fiyna, Jiita Bil Amril Mutwai,
Jiita Sharraftal Madina, Marhaban ya Khayra Dai.

Juma M. Bwanakheri,
(Ustaadh),
S.L.P. 45245, Dar es Salaam.



Hawa ndio waja wema

Ninamlaani shetani, alotoka rehmani,
Nachukua Qur’an, nataka yaliyo ndani,
Nipate kuzibaini, sifa zao waumini,
Hawa ndio waja wema, awapenda Rahmani.

Katika ya upuuzi, kuwakuta ni muhali,
Na maneno ya kuudhi, wajipushie mbali,
Tupu wanazihifadhi, kuzini hawakubali,
Hawa ndio waja wema, awapenda Rahmani.

Sala zinawahifadhi, wafanya mambo azizi,
Na hawayawii radhi, machafu yaliyo wazi,
Dhuluma kwenye ardhi, wakata yake mizizi,
Hawa ndio waja wema, awapenda Rahmani.

Mema wanayapupia, mabaya wayakimbia,
Pale wanapokosea, haraka wanatubia,
Na wanapokosolewa, wanarudi kwenye njia,
Hawa ndio waja wema, awapenda Rahmani.

Mema wayalingania, mabaya wayakemea,
Muda wanautumia, na mapesa kwa mamia,
Bongo wanazisugua, kalamu wazitumia,
Hawa ndio waja wema, awapenda Rahmani.

Islamu anuani, wanojitambulishia,
Nyingine hawazioni, zenye kupoteza njia,
Nyongeza hawatamani, kamba wanashikilia,
Hawa ndio waja wema, awapenda Rahmani.

Mikakati wanabudi, lengo wapate fikia,
Mbinu wazitathmini, mipango wajiwekea,
Vikwazo wavibaini, vilivyoko kwenye njia,
Hawa ndio waja wema, awapenda Rahmani.

Daima huwa mfano, kwa vitendo na maneno,
Watu wenye msimamo, mwenendo wao ni kisomo,
Wenye kujali kisomo, pamoja na kisimamo,
Hawa ndio waja wema, awapenda Rahmani.

Pamoja washikamana, huruma waoneana,
Mema huamrishana, maovu wakatazana,
Wenye kusaidiana, wanaosameheyana,
Hawa ndio waja wema, awapenda Rahmani.

Watu wasio papara, wenye kufanya subira,
Wafanyao biashara, ya dunia kwa akhera,
Wanosimama imara, wasokubali khasara,
Hawa ndio waja wema, awapenda Rahmani.

Watu wanotafakari, wasopenda yafakhari,
Uongo hawakariri, ukweli wanaukiri,
Tena hawi kiburi, kwa tajiri na fakiri,
Hawa ndio waja wema, awapenda Rahmani.

Watendao kwa Ikhlasi, mambo bila wasiwasi,
Muumba hawamuasi, hata iwe kwa risasi,
Wagumu kwa vishawishi, kawashindwa Ibilisi,
Hawa ndio waja wema, awapenda Rahmani.

Allah ndiye Mkwasi, tuondoe wasiwasi,
Tukinge na vishawishi, tusome kwa urahisi,
Moyoni tuwe wasafi, mema yapate nafasi,
Nimechoka najihisi, kalamu naijilisi.

Idd S. Kikong’ona,
Morogoro.



Hijabu ni vazi jema

Wenzetu akinamama, Dada mwatuaibisha,
Mavazi yaso heshima, kuvaa yasikitisha,
Yanaleta uhasama, waume kutamanisha.
Hijabu ni vazi jema, tulivae kinamama.

Tulivae kina mama, Hijabu kulidumisha,
Staha ya mwili mzima, burudani hiyo tosha,
Hakuna kukusakama, wala kukubabaisha,
Hijabu ni vazi jema, tulivae kinamama.

Vimini sasa kukoma, kuvaa kuvifupisha,
Fahamu mwili mzima, jua unauonyesha,
Maadili yamehama, ya asili kupotosha,
Hijabu ni vazi jema, tulivae kinamama.

Imebaki dhahama, matusi kutukanisha,
Wengine watu wazima, vijana wawapotosha,
Wawe ni mfano mwema, kuweza kuwafundisha,
Hijabu ni vazi jema, tulivae kinamama.

Badala yake lawama, wazazi kujibebea,
Wana Harakati Wima, fedheha kuondoa,
Liwe jambo la lazima, mkazo kulitilia,
Hijabu ni vazi jema, tulivae kinamama.

Mwenyekiti Mama, Fatma Lazaro katuambia,
Tusibakie kusema, vitendo twarajia,
Yapungue lau kama, nguo fupi kutupia,
Hijabu ni vazi jema, tulivae kinamama.

Pongezi kwako Waziri, Elimu Utamaduni,
Kupasisha vazi zuri, livaliwe mashuleni,
Tunataka lisafiri, mijini na vijijini,
Hijabu ni vazi jema, tulivae kinamama.

Ni vazi la kujistiri, refu hadi miguuni,
Linahimiri kikiri, hata kazi za nyumbani,
Beni nane nasafiri, kalamu naweka chini,
Hijabu ni vazi jema, tulivae kinamama.

Umoja wa Kinamama Gongo la Mboto,
Dar es Salaam.
 
 
 

Juu RUDI


Bonyeza hapa
kushriki mjadala au kutoa maoni juu ya habari hizi na masuala mengineyo ya Kiislamu kwenye Baraza ya Wasomaji

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtz.org
 
An-nuur Home | Ukurasa wa Mwanzo | Islam Tanzania 
Links | Matoleo Yaliyopita | Sign our Guestbook