WATU MAARUFU
 

Malcolm X (Alhaj Malik Al Shabbaz): Mwanaharakati aliyepigania usawa kwa watu wa rangi zote - 2
 

Na 'nilipoteleza' katika mahojiano ya televisheni, basi mtangazaji aliingia katika mtego wangu (aliingia kwenye ndoano yenye chambo) na kudai, "Ahhh! Hakika, Bwana Malcolm X huwezi kukanusha kwamba haya ni maendeleo kwa watu wenye rangi kama yako (kwamba na wao wameruhusiwa kujiunga na Vyuo Vikuu!)"

Kisha nilitikisa kidogo mti ulioshika hiyo ndoano yenye chambo na kusema "Siwezi kugeuka upande wowote bila kusikia kuhusu 'maendeleo ya haki sawa kwa watu wa rangi zote'. Wazungu wanaonekana kudhani kwamba watu weusi watashangilia kauli zao kama hizi na kupiga kelele za 'halleluyah'! Kwa muda wa miaka mia nne mtu mweupe amechomeka kisu chake chenye urefu wa futi moja ndani ya mgongo wa mtu mweusi, na sasa mzungu ameanza kuchomoa kisu hicho, tuseme kwa urefu wa inchi sita. Je mtu mweusi ana wajibu wa kushukuru hapa? Kwa nini? Hata kama mzungu atakitoa kisu chote nje bado na lazima litabaki kovu.!

Licha ya kwamba maneno ya Malcolm X yaliwauma waliowabagua na kuwanyima haki Wamarekani wenye asili ya Afrika, lakini mtazamo wa kibaguzi sawa na huu wa Taifa la Kiislam ulimfanya asikubali kumpokea mweupe yeyote kama ni mkweli au mwenye uwezo wa kusaidia kuirekebisha hali ya kibaguzi iliyokuwepo. Kwa muda wa miaka kumi na miwili, alihubiri kwamba mzungu au mtu mweupe ni shetani na "Mheshimiwa Elijah Muhammad' ni mtume wa Mwenyezi Mungu. Kwa bahati mbaya, picha tunayopewa leo hii juu ya Malcolm X inaonyesha maisha yake katika kipindi hiki, na ingawa mabadiliko aliyoyafanya yalimfanya awe tofauti na alivyokuwa hapo mwanzo, na zaidi ya yote ujumbe wake kwa watu wote wa Marekani.

Kubadilika na kuingia Uislam wa kweli

Mnamo March 12, 1964, ikichochewa na wivu dhidi yake ndani ya Taifa la Kiislamu na kudhihirika kwa makosa ya zinaa ya Elijah Muhammad, Malcolm X aliondoka Taifa la Kiislamu akiwa na nia ya kuanzisha jumuiya yake mwenyewe.

"Najisikia kama mtu aliyekuwa amelala usingizi mzito na nilikuwa chini ya udhibiti wa mtu mwingine. Sasa naona kwamba ninachokifikiria na kusema kinatokana na mimi mwenyewe. Hapo kabla, ilikuwa ni kwa ajili na kwa muongozo wa mwingine; sasa nafikiria kutumia akili yangu mwenyewe."

Malcolm X alikuwa na umri wa miaka 38 wakati alipoachana na mafundisho ya Elijah Muhammad katika Taifa la Kiislamu. Akikumbuka juu ya mambo yaliyotokea kabla ya kuondoka, Malcolm X anasema:-

"Katika Chuo Kikuu kimoja au kingine, mara nyingi katika mikusanyiko isiyo rasmi baada ya mimi kuhutubia, walinijia kiasi cha watu kama kumi hivi au zaidi kidogo, ambao rangi zao zilionekana kuwa nyeupe na wakajitambulisha kama Waarabu toka Mashariki ya Kati au Afrika ya Kaskazini, na kwamba wao ni Waislamu ambao aidha wanatembelea, wanasoma au wanaishi Marekani. Waliniambia kwamba licha ya kwamba nilitoa kauli za lawama kwa uovu uliofanywa na watu wote weupe dhidi ya watu weusi, bado walidhani kwamba nilikuwa mkweli kwa kujiita Muislamu, na walihisi kwamba iwapo ningefahamu "Uislamu wa kweli" basi "ningeuelewa na kuufuata" Kama kawaida, nikiwa kama mfuasi wa Elijah, nilipuuzia kila wakati yaliposemwa maneno kama haya. Lakini nilipokuwa peke yangu na kufikiria baada ya makutano kama hay, nilijiuliza: hivi kama mtu alikuwa mkweli katika kudai kwamba ni mfuasi wa dini fulani kwa nini niepuke kupanua elimu yangu juu ya dini hiyo?.

Hao Waislamu wa kweli ambao nilikutana nao, mmoja baada ya mwingine, walisisitiza nionane na kuongea na Dr. Mahmoud Youssef Shawarbi. Kisha siku moja Dr. Shawarbi na mimi tulikutanishwa na mwandishi wa gazeti fulani, na tuliongea kwa dakika kumi na tano au ishirini hivi. Wote tulilazimika kuagana ili kutimiza miadi tuliyoweka, na hapo aliniambia maneno ambayo mantiki yake haitaondoka kichwani mwangu. Alisema "Hajaamini Muislamu kwa ukamilifu mpaka amtakie nduguye (katika Uislamu) kheri anayojitakia yeye".

Athari ya Hija

Mnamo mwaka 1964 Malcolm X alisafiri kwenda Makkah kufanya Hija. Naye anasimulia juu ya Hajj na jinsi ilivyoathiri mtazamo wake alioushikilia:

Kuzuru Makkah, ambayo hujulikana kama Hajj, ni moja ya nguzo za Uislamu ambapo kila Muislamu mwenye uwezo lazima aitimize angalao mara moja katika maisha yake.

Qur'an Tukufu inasema "Na Mwenyezi Mungu amewawajibishia watu wafanye Hija katika nyumba hiyo (iliyojengwa na Nabii Ibrahim; yule awezaye kufunga safari kwenda huko)" (3.97).

Allah anasema, "..Na utangaze kwa watu habari za Hija, watakujia, (wengine) kwa miguu na (wengine) juu ya kila mnyama aliyekonda (kwa machovu ya njiani wakija kutoka kila njia ya mbali)" (22.27). Kila mmoja katika maelfu ya watu uwanja wa ndege, waliokuwa tayari kuondoka kwenda Jeddah, alivaa kama hivi. (nayo ni shuka wanayovaa mahujaji). Ungeweza kuwa mfalme au mkulima na hakuna ambaye angejua. Miongoni mwa watu maarufu na wenye mamlaka katika jamii, walionyeshwa kwangu, nao walivaa vazi hilohilo nililovaa mimi. Mara baada yakuvaa vile, wote tukaanza kuita kwa kurudiarudia "Labbayka! (Allahumma) Labbayka!" (Nimeitika wito wako ewe Mola wangu). Watu waliojaa ndani ya ndege tuliyopanda walikuwa weupe, weusi, kahawia, wekundu na manjano, macho ya bluu na nywele za njano za kizungu zilizosokotana pamoja na nywele zangu nyekundu za kipilipili - wote tulikuwa pamoja kama ndugu! Wote tukimpa heshima Mwenyezi Mungu mmoja na wote tukipeana heshima sawa miongoni mwetu.

Hapo ndipo nilipoanza kuangalia upya mtazamo wangu juu ya "Mtu mweupe mzungu". Hapo ndipo ulipokuwa mwanzo na mimi kuelewa kwamba "Mtu mweupe" kama jina hili lilivyotumika, lina maana ya rangi ya ngozi kwa tafsiri ya kijujuu. Kimsingi hasa jina hili linaelezea fikra na vitendo.

Katika Amerika "mtu mweupe" ilimaanisha tabia, fikra na vitendo kadhaa dhidi ya mtu mweusi, na dhidi ya watu wote wasiokuwa weupe. Lakini katika ulimwengu wa Kiislamu, niliona kwamba watu wenye ngozi yenye rangi nyeupe walikuwa ni ndugu wa kweli zaidi ya yeyote niliyepata kumuona. Asubuhi ile ilikuwa ndiyo mwanzo wa mabadiliko makubwa juu ya mtazamo wangu kwa watu weupe.

Walikuwepo makumi kwa maelfu ya mahujaji, toka ulimwenguni kote. Walikuwa watu wa rangi zote, toka wenye macho ya rangi ya bluu na nywele za njano, hadi Waafrika wenye rangi nyeusi. Lakini sote tulikuwa tukishiriki katika ibada hiyo hiyo, huku tukidhihirisha moyo wa umoja na udugu ambao uzoefu wangu katika Amerika ulinifanya niamini kwamba ni kitu kisichokuwepo na kisichowezekana kati ya weupe na wasiokuwa weupe. Amerika yapaswa kuuelewa Uislamu, kwa sababu hii ndiyo dini pekee inayofuta katika jamii tatizo la ubaguzi wa rangi.

Katika safari zangu katika ulimwengu wa Kiislamu, nilionana na kuongea na hata kula pamoja na watu ambao katika Amerika wangeonekana kuwa ni weupe lakini fikra za "weupe" zilikwisha-ondolewa katika akili yao na dini ya

Kiislamu. Sijawahi kuona hapo kabla udugu wa kweli ukifanywa na watu wa rangi zote kwa pamoja bila kujali rangi za ngozi zao kama ilivyofanyika hapa kwenye ulimwengu wa Kiislamu".

Mtazamo mpya wa Malcolm X juu ya Amerika

Malcolm X anaendelea kusema:-

"Kila saa ninayopitisha hapa katika Ardhi Takatifu, inaniwezesha kuweza kuelewa kwa upana zaidi na kupata ufahamu wa kiroho wa yale yanayotokea Amerika kati ya weupe na weusi. Mnegro wa Amerika asilaumiwe kabisa kwa uadui wake dhidi ya wazungu weupe. Upinzani anaoufanya (mtu mweusi) ni matokeo ya miaka mia nne ya ubaguzi wa wazi uliofanywa na Wamarekani weupe. Lakini wakati ubaguzi wa rangi unaiongoza Amerika katika njia ya kifo bado naamini, kutokana na uzoefu nilioupata pamoja nao weupe wazungu, kwamba weupe wa kizazi cha vijana, katika Vyuo Vikuu, wameshaona ujumbe wa maandishi ulioandikwa ukutani na wengi wao watageukia njia ya kweli ya kiroho (nayo ni Uislamu); nayo ndiyo njia pekee iliyobaki kwa Amerika

kuepuka matokeo mabaya ya ubaguzi wa rangi ambao bila shaka ndio utakuwa mwisho wake iwapo hilo halitafanywa.

Ninaamini kwamba, Mungu anatoa nafasi ya mwisho kwa ulimwengu wa 'Wakristo' weupe kutubia na kuomba msamaha kwa makosa yao ya kuunyonya na kuutia utumwani ulimwengu wa wasio weupe. Nayo ni sawa kabisa na wakati Mwenyezi Mungu alipompa firauni nafasi ya kufanya toba. Lakini Firauni akadumu katika kukataa kwake kutoa haki kwa wale aliowagandamiza. Na tunajua Allah mwishowe akamwangamiza Firauni.

Sitaweza kusahau chakula cha jioni nyumbani kwa Dr. Azzam kwa mwaliko wake nilipokuwa Jeddah. Jinsi tulivyozidi kuongea, ndivyo hazina yake kubwa ya elimu ilivyozidi kudhihirika na mambo mengi aliyoyafahamu yalionekana kama hayana mwisho. Aliongea juu ya kizazi cha Mtume Muhammad (SAW) na akanifahamisha kwamba walikuwepo weusi na weupe. Kisha akanielewesha jinsi ambavyo rangi ya mtu na matatizo yake yaliyopo katika ulimwengu wa Kiislam, yamekuwepo pale ambapo na kwa kiwango ambacho sehemu ile ya ulimwengu wa Kiislamu imeathiriwa na nchi za Magharibi. Alisema kwamba kama utakutana na tofauti zozote zenye msingi wa ubaguzi wa rangi, basi hii moja kwa moja inaashiria kiwango cha athari zilizoachwa na Umagharibi".
 
 

Juu RUDI


Bonyeza hapa
kushriki mjadala au kutoa maoni juu ya habari hizi na masuala mengineyo ya Kiislamu kwenye Baraza ya Wasomaji

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtz.org
 
An-nuur Home | Ukurasa wa Mwanzo | Islam Tanzania 
Links | Matoleo Yaliyopita | Sign our Guestbook