Wastaafu wazee wetu wapendwa tafuteni hatma njema
Ndugu Mhariri,
Makusudio ya maoni haya ni kuwakumbusha wazee wetu viongozi wastaafu ambao wananchi wa nchi hii bara na visiwani hasa Waislamu wanawahishimu na kuwastahi licha ya kumbukizi ya machungu yao.
Namuheshimu mzee Jumbe kwa kuthubutu kueleza ukweli; mbele ya kikao kizito cha chama chake kuhusu jinamizi la Muungano na haki ya wananchi wa Zanzibar kujitawala wenyewe, ukweli uliosababisha ashinikizwe kujiuzulu nyadhifa zote. Namuheshimu kwa kurudia kuueleza ukweli huo na dhulma inayofanywa dhidi ya wananchi waliowengi hapa nchini.
Kwa upande wake namuheshimu Mzee Mwinyi kwa busara na uongozi uliojali wananchi ambao uliiwezesha nchi hii kuondokana na sera za ujima za utawala wa "nongwa" na ajenda za siri ( Sivalon).
Chini ya uongozi wa Mzee Mwinyi(baba wa hekima) watu walipiga hatua kuyaelekea maendeleo kibinafsi na hata kijamii. Kwa haya, namuheshimu san Mzee Mwinyi.
Jumapili iliyopita jumuiya ya World Muslim Congress tawi la Tanzania chini ya uenyekiti wa mzee Jumbe iliwaalika wanawake wa kiislamu jijini na baadhi ya mikoa katika semina iliyofanyika kwenye ukumbi wa Starlight.
Ingawa awali ilidaiwa kuwa semina hiyo ililengwa kujadili maendeleo ya waislamu lakini hali iliyokuja kujitokeza ilielekea mkondo ule ule wa kuwaandalia majukwaa waheshimiwa wasiowatakia mema Waislamu.
World Muslim congress chini ya uongozi wa Mzee Jumbe na katibu wake aliyekuwa Mkurugenzi wa Rabita bwana Mohammed Rukara raia wa Burundi, nadhani ilitumika tu kuitisha "semina" hiyo ya siku moja ili lipatikane jukwaa la kidini kuwatisha Waislamu wanaofungua midomo kukemea dhulma na ukandamizaji wa CCM na serikali yake.
Jukwaa lingine huenda likaandaliwa si muda mrefu mkoa wa Tabora chini ya mwavuli wa mashindano ya kusoma Qur-an na kuhimiza mshikamano miongoni mwa Waislamu!
World Muslim Congress chini ya Uenyekiti wa Mzee Jumbe haiwezi kukwepa lawama kutokana na shutuma, kejeli na masimango ya muheshimiwa katika semina ya starlight. Kwa sababu hiyo wasi wasi wangu wa muda mrefu juu ya jumuiya hiyo kwamba huenda ajenda yake ni ile ya kuwa karibu au kutoa fursa viongozi wa serikali kuwanyamazisha Waislamu umepata nguvu.
Kama muelekeo wa jumuiya ndiyo huu, kwa kuzingatia heshima kubwa aliyonayo Mzee Jumbe hivi sasa na kwa kumtakia hatma njema, pengine ningemshauri afuatilie kwa karibu utendaji wa jumuiya au ajiengue kabisa. Vinginevyo heshima yake yaweza kuwa hatarini.
Mzee Mwinyi naye amekuwa akifanya ziara za ama kualikwa na jumuiya za kiislamu au zile za kichama (CCM) au serikali mikoani. Katika ziara hizo amekuwa akitoa hotuba zenye muelekeo wa kuwatuhumu Waislamu kuleta vurugu za kidini miongoni mwao au kati yao na madhehebu mengine.
Si hivyo tu bali amekuwa akiwashutumu kuwa hawajafanya jitihada zozote kujiletea maendeleo badala yake huilaumu serikali na chama tawala.
Namuomba Mzee Mwinyi asite kuwasaidia madhalimu. Nina Hakika kabisa anaelewa mengi juu ya ukwamishwaji wa makusudi wa jitihada za Waislamu katika uwanja huo wa "elimu dunia".
Anafahamu kuvunjwa kwa EAMWS, anafahamu pia kuundwa kwa Bakwata na madhila ya Bakwata juu ya Waislamu tangu mwaka !968. Anafahamu utawala wa Mwalimu Nyerere ulivyowabinya Waislamu. Anafahamu watoto wa kiislamu walivyozuiliwa kielimu kwa njama maalum hadi pale Marehemu Prof. Malima alipobaini na yepi yaliyoendelea dhidi yake hadi kifo chake. Na anafahamu jitihada za Waislamu kuichukua Bakwata ili iwaunganishe wapige hatua kimaendeleo na jinsi jitihada hizo zilivyokwamishwa. Yeye mwenyewe alinawa mikono pale Ikulu kuwa jambo hilo hakuwa na ubavu wa kulitolea uamuzi wa mwisho!
Mzee Mwinyi yeye aache tu. Tunakumbuka masheikh na Waislamu wengine walivyodhalilishwa , kusota rumande kwa miezi kadhaa na hatimaye wengine kufungwa kidhulma chini ya utawala wake.
Hata hivyo hayo yote hatimaye tulimsamehe baada ya kuonyesha dalili za majuto na hatua aliyoichukua kama rais wakati ule kuwaachia huru wadhulumiwa wale. Na vile vile hayo yote tulimsamehe kwa hoja kwamba mawakala wa kanisa serikalini wakiongozwa na aliyekuwa naibu waziri Mkuu na Waziri wa mambo ya ndani Agustino Lyatonga Mrema walimzidi nguvu.
Hapana sababu ya msingi kwa Mzee Mwinyi hivi sasa kujivurugia heshima yake. Waislamu tumechoka kunyanyaswa, kudhulumiwa, kukejeliwa na kupuuzwa nchini mwetu. Tumechoshwa na utawala usiojali shida za raia, usiozingatia Katiba wala sheria. Tunataka mabadiliko.
Hatutamstahi yeyote yule hatakama ni jumuiya ya kiislamu, Imamu, sheikh, Ustaadh, mwanasiasa, kiongozi wa juu aliyepo au mstaafu serikalini atakayesimama upande wa madhalimu.
Wale wenye ndoto za kuwarubuni Wadhulumiwa kupitia taasisi hizo au nyadhifa hizo wafahamu kuwa wamenoa kwani hapendwi mtu kwa kuswali kwake, maneno matamu au dini yake bali uadilifu, haki na usawa na kujali matatizo ya Watu wote ndiyo kipimo chetu.
Nawaomba wastaafu wetu wakae mbali na siasa kandamizi za wale wanaojivika ufalme kinyemela. Wastaafu wetu watafute hatma njema ya maisha yao kwa kusimama sambamba na wadhulumiwa kupigania usawa kwa watanzania wote.
Abdallah Khalfan Zumbe
Private Bag
Kibamba
Ndugu Mhariri
NAOMBA nami niweke kwenye gazeti lako ili nitoe maoni yangu juu ya ruhusa iliyotolewa na Bwana A.S. Mbegu katika gazeti la Aprili 2 - 8, mwaka huu Na. 195 Dhulhija 1419, lenye kichwa cha habari Hijab kuvaliwa rasmi mashuleni.
Ufafanuzi wa Hijab umeishaelekezwa na Mwenyezi Mungu. Hayo maelekezo ya vikao vya kina Mbegu ni hijabu gani tena? Tunachohitaji sisi sio maelekezo bali turuhusiwe bila kubugudhiwa vazi hilo liweje tuachiwe wenyewe. Kwani ni kikao gani kilichokaa kikawapangia Masister kuvaa mavazi hayo wanayovaa mashuleni?
Ombi langu kwa wazazi wa Kiislamu nchi nzima wawashonee watoto wao vazi hilo kama Mtume (s.a.w.) alivyoelekeza na sio Mbegu na wenzake.
Pia naomba walimu Waislamu kuanzia shule za msingi, sekondari na vyuo tuanzishe umoja utakaotuunganisha kuanzia ngazi ya shule, kata, tarafa, wilaya, mkoa na taifa ili kuwa na sauti moja ya kutetea haki za msingi za Waislamu mashuleni na vyuoni.
Mwisho naiomba serikali itangaze tena kuwa hijab ruksa kwani inaonyesha waraka huu ulifichwa mahali kiasi kwamba sasa hivi imekuwa kero kubwa kwa Waislamu wanaokumbushia kutekelezwa kwa waraka huo.
Mwalimu wa Shule ya Msingi
Miembe Saba,
S.L.P. 94,
Bagamoyo, Pwani.
Ndugu Mhariri
UISLAMU kuuzungumzia tunaweza sana, lakini vitendo inakuwa vigumu sana. Je, kama tukiendelea na hali hiyo tutafika kweli?
Yale tunayozungumza kwenye mikutano yetu tukiimaliza wenyewe tunarudi majumbani kulala wenzetu hawalali, huyajadili mpaka wana hakikisha wanapata ufumbuzi.
Leo tunazungumzia uchaguzi wa mwaka 2000, lakini wenzetu tayari wako hatua ya mwisho ya maandalizi yao, sisi bado tunasuasua wala hatujaelewa tuanzie wapi.
Na bahati mbaya tumekubali propaganda inayotupumbaza ya tusichanganye (dini na siasa) wakati wao wanaitumia sana Misikiti kuendeleza na kulinda tawala zao.
Maoni yangu ndugu Waislamu tafadhali sensa ya waumini lazima iendelee kila Msikiti ili tujijuwe tuko wangapi pia na katika kuandikisha jina la mtu aulizwe je unakubaliana na harakati, akisema ndio basi jina lake liandikwe.
Sensa hii iwe ya nchi nzima, wanaharakati wetu watengeneze kanda zipelekwe mikoani ili kuwaelimisha juu jambo hli wasije wakasema ni dini mpya, kama si kwenda kwenyewe basi naiomba kamati isimamie zoezi hili na ihakikishe inapata orodha ya waumini wote nchi nzima InshaAllah bila kuogopa vitisho vya yeyote kwani MwenyeziMungu amesema:
Hawatakuwa radhi juu yako Mayahudi wala Wakristo mpaka ufuate mila yao. Sema: "Hakika uwongozi wa Mwenyezi Mungu ndio uwongozi (khasa)." Na kama ukifuata matamanio yao baada ya yale yaliyokufikia ya ujuzi (wa kweli) hutapata msaidizi yoyote wala mlinzi kwa Mwenyezi Mungu. (Qur. 2:120)
Hilo la kwanza, pendekezo langu la pili kuandaa watu wetu tukaowatuma huko Bungeni.
Yahya Rashidi Makame,
Mburahati, National,
Dar es Salaam.
Ndugu Mhariri
NAPENDA kuunga mkono Waislamu wa Mwanza na kina mama wa Mwanza kwamba kanda ya mauaji ya Mwembechai ziandaliwe kwa wingi kwa ajili ya kuonyesha wakati wa kampeni ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2000.
Mwaka 1995 CCM iliwaonyesha wananchi wa Tanzania mauaji ya Rwanda kuwa kama watachagua chama kingine wajuwe hali itakuwa kama hiyo ya Rwanda. Mwaka 2000 Waislamu muwaonyeshe Watanzania mauaji ya Mwembechai ili waelewe kuwa kama mwaka 2000 wataiweka madarakani serikali iliyopo wajuwe watakiona cha moto zaidi. Hawa watafanya makubwa zaidi kwa kibri.
Ombi langu kampeni hizo zilenge mikoa ambayo uwezo wa kuona mbali ni mita 100 sawa na uwanja wa mpira, kilicho zaidi ya urefu huo hawakioni kwa sababu baadhi yetu tumefunikwa na kitambaa cheusi usomi toka Amerika, Italia na Uingereza hasa mikoa ile ya bondeni ambako mimi nimezaliwa na kuishi.
Othuman Abdurahman,
Masasi.
NAPENDA nitoe wito huu kwa Waislamu wenzangu wanaume kwa wanawake kwamba mwaka 2000 unakaribia wasije wakajisahau wakatupa kura zao kuipa CCM.
Wasije wakadanganyika kwa vishawishi vyovyote au lugha tamu ya makada wa CCM, kwa kila Muislamu amuelimishe Muislamu nwenziwe ubaya wa CCM, na yaliyowapata Waislamu kwa serikali ya CCM na kila Muislamu awe muhamasishaji kwa Waislamu wenzake, ndugu, jamaa, marafiki kutopoteza kura mwaka 2000.
Kumbukeni Waislamu yaliyotupata ni makubwa sana yanatia uchungu, lakini yasimulieni popote mlipo, na mzidi kukumbushana maovu ya CCM dhidi ya Waislamu.
Karim Athumani,
Kinondoni A,
Dar es Salaam.
|
|