Kubadili anuani
Salamu alaykumu, amani nawaombea,
Ndugu zangu Isilimu, ANNUUR
nikipitia,
Nimeishika kalamu, habari
kuwaletea,
Nimeona ni muhimu, watunzi
kuwaambia,
Kubadili anuani, Mwadui
nimeondoka.
Mwadui nimeondoka, nyumbani
nimerejea,
Riziki imekatika, mgodi
nawaachia,
Kazi yake mtukuka, yote
amenipangia,
Wala sinayo mashaka, Mola
atanijalia,
Kubadili anuani, Mwadui
nimeondoka.
Namshukuru Rabuka, kweli
amenijalia,
Kumi na nne miaka, Mwadui
kujikalia,
Ualimu kuushika, wanafunzi
kuwanoa,
Leo hii kuondoka, salama
nafurahia,
Kubadili anuani, Mwadui
nimeondoka.
Nimerejea nyumbani, ni hapa
Mwanza mjini,
Sehemu ni Mabatini, ni karibu
na sokoni,
Barua nitumieni, na nyumbani
karibuni,
Anauani nawapeni, nitaiandika
chini,
Kubadili anuani, Mwadui
nimeondoka.
Samahani marafiki, habari
kutowafika,
Kuhama kuna mikiki, muda
ulinikatika,
Kwangu ilikuwa dhiki, barua
kuziandika,
Naomba mniafiki, msiache
kuandika,
Kubadili anuani, Mwadui
nimeondoka.
Nawaaga kina mama, pale Shinyanga
mjini,
Bi Zuhura nimehama, mtihani
wa Manani,
Muhibu Daresalama, Bi Batuli
wa Pangani,
Mtandika nimehama, Rufiji
nieleweni,
Kubadili anuani, Mwadui
nimeondoka.
Zuberi wa Mohamed, Singida
kwako Mugoo,
Jumanne bin Undi, Shinyanga
Jihad njoo,
Muifanye jitihadi, ANNUUR
iwe kioo,
Kwaherini nnarudi, jikoni
mboga jogoo,
Kubadili anuani, Mwadui
nimeondoka.
Mwl. Zabibu Iddi Ng'onda,
Box 7165,
Mabatini,
Mwanza.
Akhera
Nikifikiri jamani, akhera
najililia,
Moyo wangu watamani, nisiitoke
dunia,
Nayo haiwezekani, Mola ameahidia,
Sijui nitafanyaje, akhera
kuna mazito.
Akhera siitamani, kila nikikumbukia,
Akhera kuna huzuni, nikiwaza
najutia,
Akhera ni mtihani, kuushinda
nahofia,
Siku hiyo ya Qiyama, nzito
inaogopesha.
Qiyama siyo utani, Mola ametuambia,
Qiyama chake Manani, mmiliki
tunajua,
Qiyama nambari wani, swala
kutuhesabia,
Qiyama ni siku nzito, Yarabi
tishio kubwa.
Sina raha asilani, kila nikifikiria,
Hata nile biriani, ni kama
najisumbua,
Mawazo yako motoni, Mungu
kisha uchochea,
Qiyama kitakapofika, tabu
tupu na mashaka.
Nikiwepo kitandani, usingizi
unapaa,
Najiona wa motoni, sina
kitakachonifaa,
Nimetanguliza nini, mwenyewe
najikosoa,
Maisha yake akhera, hasara
ni kubwa sana.
Najionea imani, mimi dhaifu
najua,
Nitashika mti gani, huo
wa kuniokoa,
Yarabi wangu Manani, nisamehe
ya dunia,
Unipe chumba cha mwisho,
kwa daraja za peponi.
Hakuna kujua mama, baba,
shoga, wala mwana,
Roho zataka salama, hakuna
saidiana,
Vitisho vyake Qiyama, wote
ni kukimbiana,
Tuhurumie Maliki, adhabu
hatuiwezi.
Utusamehe Karima, mimi na
wangu wazazi,
Tuepushe jahanama, na changu
hiki kizazi,
Utuonee huruma, Allahu,
Rabbi, Azizi,
Kwetu itakuwa vipi, siku
ya msukosuko.
Qiyama kikisimama, mambo
yatakuwa wazi,
Kila kitu kitasema, kushitaki
kwa Azizi,
Ushahidi kusimama, tutashikwa
bumbuazi,
Akhera ni nzito sana, nitamlilia
nani?
Mchana ukitokea, na usiku
kuingia,
Hasara najipatia, kifo kukimbilia,
Kaburini kuingia, ardhi
yaningojea,
Tusamehe ya Al-Jabar, waja
wako ni dhaifu.
Askari watiifu, walinzi watasimama,
Malaika watukufu, kwa kumtii
Karima,
Wajipange safusafu, ni wapi
pa kuegama,
Akhera yakaribia, Al-Ghafuur
tusamehe.
Mwl. Zabibu Iddi Ng'onda,
S.L.P. 7165,
Mabatini,
Mwanza.
Kwa jina la Subhana, ninaishika
kalamu,
Niwajuze waungwana, wakae
wakifahamu,
Mkwezi tuliyenena, ahadiye
ilitimu,
Mkwezi wa sifa gani, mimi
atayenifaa?
Mkwezi alipokwama, niliwajuza
kaumu,
Zuberi akaja hima, pamoja
na Kuluthumu,
Nasaha wakazisema, atawalipa
Karimu,
Mkwezi wa sifa gani, mimi
atayenifaa?
Mikidadi Burhana, hakusita
kukalimu,
Mwinyikai akanena, pikelele
kajihimu,
Sharifu aliungana, tawalipa
Muadhamu,
Mkwezi wa sifa gani, mimi
atayenifaa?
Si kama nilinyamaa, kwa hayo
lonilazimu,
Watu niliwagutia, na kuomba
kwa Rahimu,
Mkwezi kajiachia, kabla
hawajatimu,
Mkwezi wa sifa gani, mimi
atayenifaa?
Mkwezi tulimzika, kwa yote
yanolazimu,
Hayo ndiyo yalotuka, hadi
kimya kikadumu,
Tumuombee Rabbuka, ende
Jannatu Naimu,
Mkwezi wa sifa gani, mimi
atayenifaa?
Si ndwele yalotendeka, tugange
yanolazimu,
Nazi zimeshakauka, kuzivuna
yangu hamu,
Nyingine zapukutika, zawa
mbata humuhumu,
Mkwezi wa sifa gani, mimi
atayenifaa?
Ushauri nautaka, wafaida
ya kudumu,
Kwa mkwezi wa hakika, awezaye
kazi ngumu,
Ninaogopa hakika, mkwezi
mwingine humu,
Mkwezi wa sifa gani, mimi
atayenifaa?
Beti tisa zinatosha, majibu
ninayo hamu,
Malenga nawaamsha, nyote
shikeni kalamu,
Mkwezi gani atosha, kwa
sifa zinolazimu?
Mkwezi wa sifa gani, mimi
atayenifaa?
Juma M. Bwanakheri,
(Utaadh),
S.L.P. 45245,
Dar es Salaam.
Awali amani kwenu, hali nataka
kujua,
Kuhusu mimi mwenzenu, sijambo
najizuwia,
Tatizo langu ni lenu, ndiyo
ninaulizia,
Msikiti rudisheni, ni mali
ya Muumba.
Mtume ameondoka, dini ni
ya waumini,
Sembuse wewe Mloka, mwenye
tamaa moyoni,
Bagamoyo unatoka, unadai
udhamini,
Msikiti rudisheni, ni mali
ya Muumba.
Walidai Msikiti, Mwembechai
Magomeni,
Wakaleta tofauti, vurugu
kwa waumini,
Sasa chini wameketi, wakusali
hawamwoni,
Msikiti rudisheni, ni mali
ya Muumba.
Misikiti ni majumba, ya Mola
wetu Manani,
Vipi wewe unatamba, kwa
makeke mitaani,
Unapita na jalamba, asubuhi
na jioni,
Msikiti rudisheni, ni mali
ya Muumba.
Madhambi yenu makubwa, ukifanya
tathimini,
Wamekufa waloumbwa, hawakuwa
hatiani,
Dhuluma ni jambo kubwa,
wacheni ushindani,
Msikiti rudisheni, ni mali
ya Muumba.
Watu wengi walilani, mauaji
balozini,
Vipi ya Msikitini, mlichokifanya
nini?
Chuki kakaa wodini, serikali
ni ya nani,
Msikiti rudisheni, ni mali
ya Muumba.
Kalamu ninaiwacha, nawahi
Msikitini,
Endapo mtauwacha, Mungu
tawaghufirini,
Ombeni usiku kucha, Msikiti
rudisheni,
Msikiti rudisheni, ni mali
ya Muumba.
Zuberi M. Mwinyi (Amir),
P.P. Box 614228,
Dar es Salaam.
Dini tunaiharibu
Dini ni utaratibu, wa maisha
yetu sisi,
Dini siyo madhehebu, na
wala si taasisi,
Dini si ya Waarabu, na si
wa watu weusi,
Kutukanana matusi, dini
tunaiharibu.
Dini tunaiharibu, Mola tunapomuasi,
Na kufanya taasubu, kubaguana
kwa jinsi,
Sisi tunacho kitabu, ndiyo
yetu silabasi,
Kutukanana matusi, dini
tunaiharibu.
Pengine ni maaribu, yatuzingayo
nafusi,
Shida zinapotuswibu, imani
huwa nyepesi,
Ndipo twatia irabu, zitupazo
kujihisi,
Kutukanana matusi, dini
tunaiharibu.
Nyingi hazina hesabu, mahakamani
zetu kesi,
Za kututia aibu, kwa nguvu
za ibilisi,
Ambae atughilibu, na kutupa
wasiwasi,
Kutukanana matusi, dini
tunaiharibu.
Ni wakati wa kutubu, na kufanya
majlisi,
Qiyama kiko karibu, kuhukumiwa
unasi,
Ni lipi tutalojibu, kwa
Rabbi Muumba insi,
Kutukanana matusi, dini
tunaiharibu.
Beti sita matulubu, nimezitunga
kwa kasi,
Ninahofu Wahhabu, khofu
yenye ikhlasi,
Anepushiye adhabu, kubwa
na ndogo kiasi,
Kutukanana matusi, dini
tunaiharibu.
Beti saba mansubu, hapa ninasema
basi,
Washairi mawhubu, nawaachia
nafasi,
Mimi bado ni naibu, nyinyi
ndio maraisi,
Kutukanana matusi, dini
tunaiharibu.
Khamisi Juma Sibura,
S.L.P. 164,
Majengo - Shinyanga
Bismillahi naanza, kwa jina
la Mola wetu,
Islamu kuwaasa, uwongo si
mila yetu,
Sikukuu kuiacha, ni yao
wala si yetu,
Aprili moja siku, Islamu
si ya kwetu.
Wajinga walianza, kuwaongopea
watu,
Sikukuu kuanzisha, eti nini
ya wapumbavu,
Siku huadhimishwa, kuwadanganya
watu,
Aprili moja siku, Islamu
si ya kwetu.
Matukio huanzishwa, uongo
si kweli katu,
Gazetini huandikwa, ili
kuwapasha watu,
Habari zisohakika, ili kupumbaza
watu,
Aprili moja siku, Islamu
si ya kwetu.
Mtume amekataza, uwongo kila
mtu,
Isipokuwa ameacha, katika
sehemu tatu,
Na hizo hakuzitaja, ziazimishwe
na watu,
Aprili moja siku, Islamu
si ya kwetu.
Kwanza ameutaja, kwa kupatanisha
watu,
Uwongo waweza kuja, ili
kuvuruga watu,
Mfarakano si tija, haitaki
dini yetu,
Aprili moja siku, Islamu
si ya kwetu.
Pili amesisitiza, kwa mume
na mke mtu,
Mume apataliwaza, mke uwongo
mtupu,
Apate kufarijika, kwa yake
masumbufu,
Aprili moja siku, Islamu
si ya kwetu.
Tatu, imekubalika, kwenye
vita vya mtutu,
Ili waje salimika, wasipungue
wenzetu,
Waweze kuendeleza, mapambano
dini yetu,
Aprili moja siku, Islamu
si ya kwetu.
Hapa mwisho nimefika, endelea
sithubutu,
Ujumbe kufikisha, Islamu
ndugu zangu,
Sikubali kuitika, furahia
sikukuu,
Aprili moja siku, Islamu
si ya kwetu.
Ramadhani H. Bakari,
Kisiju - Pwani.
|
|