TAHARIRI
Madhumuni ya Shahada
MAANA ya shahada ni kuwa
hapana Mola ila Allah na Muhammad (s.a.w.) ni Mjumbe wa Allah. Neno 'Allah'
katika Shahada linamaanisha Mungu, Ambaye ni Bwana, Muumba, Mlishaji, Mruzuku,
ambaye husikiliza maombi yetu na huyajibu, na ambaye anastahiki ibada yetu.
Pale usemapo, La ilaha illallah, inamaanisha kwanza, kwamba umetambua
na kukiri kuwa ulimwengu haukutokea bila ya uwezo wa kuumba wa Mwenyezi
Mungu, na wala si kweli kuwa una miungu wengi. Hakika una Mungu mmoja tu,
naye ni Muadilifu, na hamna yeyote mwenye uwezo wa kiungu isipokuwa Yeye
tu. Pili, lingine unalokiri katika Shahada ni kwamba Mungu Huyu Huyu ambaye
ndiye Mungu wako pia ndiye Mungu wa ulimwengu wote. Vyote unavyovimiliki
na vyote vilivyomo ulimwenguni ni Vyake Yeye. Yeye ndiye Muumba, Naye ndiye
Mruzuku. Uhai na umauti vyote vimo chini ya mamlaka yake. Dhiki na faraja
vinatokea kwa tawfiq Yake. Chochote akipatacho mtu amepewa na Yeye.
Chochote kinachomtoka mtu, kwa hakika humtoka kwa amri Yake. Yeye Peke
Yake ndiye wa kuogopwa. Yeye Peke yake ndiye wa kuombwa na kutegemewa kukidhi
mahitaji yetu. Yeye Pekee ndiye wa kuabudiwa. Sisi sote si watumwa wala
watumishi wa yeyote isipokuwa Yeye, Naye Ndiye Pekee Bwana na Mtawala wetu.
Jukumu letu halisi ni kukubali amri Zake na kikamilifu kufuata na kutii
Sharia Yake.
Hii ndio ahadi unayofunga
na Allah mara tu baada ya kutamka La ilaha illallah, na kwa kufanya
hivyo unaufanya ulimwengu mzima shahidi juu yako. Ukiivunja ahadi hii,
mikono na miguu yako, kila unywele wako, na kila chembe ya ardhi na mbingu
ambavyo mbele zao uliweka ahadi, vitatoa ushahidi dhidi yako katika mahakama
ya Allah ambako utakuwa kizimbani katika hali ya udhalili mno kiasi ambacho
hutakuwa na hata mmoja wa kukutetea. Hutakuwa na wakili wala mwanasheria
wa kukusaidia katika kesi yako.
Kwa hakika mawakili na
wanasheria ambao katika mahakama za ulimwengu huu wanaifanyia istihzai
na kuipotosha sharia kwa ajili ya maslahi ya kilimwengu, wao wenyewe katika
mahakama ya Allah watasimama katika dhila kama wewe. Mahakama hiyo si ya
kukuachia kwa ajili ya mbinu, udanganyifu au hila. Unaweza kuwaficha hatia
zako polisi wa dunia, lakini katu huwezi kuwaficha chochote polisi wa Allah.
Polisi wa dunia hupokea hongo na rushwa kinyume na polisi wa Allah. Mashahidi
wa duniani wanaweza kutoa ushahidi wa uongo, lakini sio mashahidi wa Allah,
kwani ni waaminifu sana mno kabisa. Watawala wa ulimwengu wanaweza kufanya
dhulma, lakini Allah ni Mtawala Muadilifu Asiyefanya dhulma. Na tena hamna
kuepa wala kutoroka katika jela ya Allah ambapo huwafunga wahalifu. Ni
ujinga mkubwa na kwa hakika ni upumbavu mkubwa kuliko wote kumfanyia Allah
ahadi ya uongo. Unapoweka ahadi hii, kwanza fikiri vizuri sana, kisha itekeleze
kikamilifu, kwani hukulazimishwa shingo upande utamke shahada. Kwani maneno
matupu hayana manufaa yoyote.
Bonyeza hapa
kushriki mjadala au
kutoa maoni juu ya habari hizi na masuala mengineyo ya Kiislamu kwenye
Baraza
ya Wasomaji
Kutoa
maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza
hapa
Au
Andika barua
kwa: webmaster@islamtz.org