KUTOKA MAGAZETI YA ZAMANI
 
Mashairi
 
Wakubwa tukusanyike

Edita mwingi wajina, japo pembeni niweke,
Kwangaya bure kununa, mambo haya yaepuke,
Baruwa nilivyoona, cheo wakipigateke,
Wakubwa tukusanyike, watoto tuwaokowe.

Watoto tuwaokowe, wakubwa tukusanyike,
Kutunga kwao mayowe, mnadi jina waweke,
Kutunga kwao mayowe, mradi jina waweke,
Wakubwa tukusanyike, watoto tuwaokowe.

Kapiteni Wakangara, kwangaya wachamakeke,
Ulikuwa jingabora, nguo zako ujivike,
Waiacha hadi bora, yakike ujipachike,
Wakubwa tukusanyike, watoto tuwaokowe.

Wapopote wema wenu, mwisho mje muumbuke,
Kulalia na uvungu, kwanza ngoja niwacheke,
Kweli jama haki yenu, roho ni za pekee,
Wakubwa tukusanyike, watoto tuwaokowe.

Mzee Mkanyageni, hodari upekepeke,
Utaingia motoni, kupenda taji uvike,
Jongoo ni Bininyani, mpango kura uvike,
Wakubwa tukusanyike, watoto tuwaokowe.

Beti saba nimefika, kalamu budi niweke,
Kisondoka ninacheka, swala kugeuzwa mate,
Mkwawa hana mashaka, miguu akupachike,
Wakubwa tukusanyike, watoto tuwaokowe.

Mohamed Juma A. Kisondoka
Kibindu-Kwamarungu - Uziguwa - Box.



Muolee mzazi, ajuwae sheria

Wendapo kuoa mke, chungua mambo matatu,
La kwanza wazazi wake, tabia iwe ya utu,
Wasiwe wapeke peke, mwana kumvunja utu,
Muoe mwana wa watu, ajue sheria zake.

Ajue sheria zake, muoe mwana wa watu,
Wazazi wapekepeke, hawana sheria kitu,
Kaka utamwacha mke, japo upende si kitu,
Muoe mwana wa watu, ajue sheria zake.

Tizama wazazi wake, wajue mambo ya utu,
Mkigombana na mke, wazazi wafanye utu,
Wewe pamoja na mke, wawaiteni watu,
Muoe mwana wa watu, ajue sheria zake.

Tizama fadhila zake, nakwambia mwanakwetu,
Kuvamia wanawake, viumbe usithubutu,
Mtizame mwendo wake, kichwa kisiwe kurutu,
Muoe mwana wa watu, ajue sheria zake.

Ukioa mwanamke, Halima aitwe Fatu,
Mjaribu mwenendo wake, tabia kama ya watu,
Hata na wazazi wake, waseme yaliyofitu,
Muoe mwana wa watu, ajue sheria zake.

Tamati hapa niweke, kalamu nijenge utu,
Waume na wanawake, tusiubague utu,
Yule na wazazi wake, tuwaombee balatu,
Muoe mwana wa watu, ajue sheria zake.

R.A. Mwanahewa (Mzee Simba)
Box 223,
Mbeya.


Sheria ya Jamhuri imenitoa Ubalozini - Tumbo
 

Mwafrika, Jumatatu Septemba 17, 1962
 

BWANA Kassanga Tumbo, Rais wa PDP alisema katika mkutano uliofanywa katika Jumba la Arnautoglu juzi kwa sheria ya Jamhuri inayomfanya Rais wa Tanganyika awe sawa na dikteta, ni sababu mojawapo iliyomfanya ajiuzulu Ubalozi.

Aliongeza kusema kuwa hakuweza kuvumilia kuwatendea raia mabo yasiyofaa. "Mimi sijasema uongo", alitamka, na nitaongoza chama changu kwa vitendo wala sio kwa methali.

Bwana Tumbo alisema kuwa yeye alipinga kwa nguvu zake zote ile sheria ya uraia. Lakini ilipitishwa kwa sababu alikosa kura za kutosha.

Alijitetea kwa nini ametumia jukwaa la TRAU katika mkutano alipotangaza kwamba anajiuzulu kutoka TANU na kuwa Rais wa PDP, Bw. Tumbo alisema alitumia jukwaa hilo ili kuwaaga watu wala hakuhutubia mambo ya siasa.

Mapema, Bw. Lifa Chipaka, mweka hazina wa chama hicho alisema kuwa serikali inalaumu chama chao kuwa kila wakati wanasahihisha tu baada ya kufanya vitendo.

"PDP iliishauri serikali isikope shilingi 12,000,000 za kujengea hoteli mjini Dar es Salaam, bali kila raia atoe shilingi 1 tu kwa sababu kukopakopa si kwema. Lakini serikali haikujibu".

Bw. Chipaka alisema kwamba serikali imeshindwa kutimiza ahadi zake aliposema hakutakuwa na ada za shule na kumbe hivi sasa ada zimepanda kufikia kipeo cha shilingi 960.

Bwana Chipaka alijigamba kwamba kila siku wanapata 100, na hivi sasa jumla yao ni zaidi ya 1,500.

Hotuba zikamalizika kwa kueleza kwamba matawi 10 chama yatafunguliwa hivi karibuni katika Tanganyika na tawi la kwanza likiwa Ilala mjini Dar es Salaam.


Mzungu waya kanywa mma akafanya rafu
 
Mwafrika Jumatatu, Septemba 17, 1962

YULE mzungu ambaye alijitolea kwa polisi mjini Mombasa akisema waya umemkaba na hana mbele wala nyumba, halafu akapatiwa msaada wa shilingi 100 kutoka katika 'mfuko wa Maskini' na Hakimu wa Mombasa alirejeshwa tena kortini Ijumaa akishitakiwa kufanya fujo baada ya kuuchapa mma.

Mzungu huyo, Patrick King, alifikishwa mbele ya Hakimu Mkuu wa Mombasa, Bw. R.J. Quin, siku ya Ijumaa akashitakiwa kwamba alifanya fujo katika Palace Hotel ya Mombasa.

Kortini hapo Ijumaa ilielezwa kwamba mshitakiwa baada ya kujitolea polisi na kusema kwamba alikuwa hana kitu, alifikishwa kortini na Hakimu akatoa ruhusa kwamba apatiwe shilingi 100 kutoka katika 'mfuko wa maskini' ili aendeshee maisha yake mpaka Septemba 20, Alhamisi ijayo ili aeleze ameingiwaje na waya kadiri hiyo.

Atarudi kortini

Jamaa baada ya kupewa mapesa hayo, baadaye akaja kukamatwa ameunyaka mma na kufanya rafu katika Palace Hotel.


Marealle ni balozi wa Tanganyika?
 

Mwafrika Juni 22, 1961

BWANA Thomas Marealle ambaye alikuwa Mangi Mkuu tangu mwaka 1952 mpaka alipoondolewa hivi mwaka jana baada ya Wachagga kujichagulia Rais, ameshatangazwa sana na uvumi ambao umeenea kila mahali mjini Moshi, Amerika na Tanganyika kwamba amechaguliwa kuwa Balozi wa Tanganyika.

"Kila mahali mjini pamejaa uvumi huu" amesema Bwana Marealle alipoonana na mwandishi wetu mjini Moshi "lakini sijui uvumi huu umetokana na nani, hali serikali ya Tanganyika haijanieleza lolote".

Bwana Marealle amesema kuwa amepata hata barua za pongezi kutoka kwa watu maarufu huko Amerika na Uingereza kuhusu jambo hilo. "Lakini naamini watu hao ni watu wenye uhakika, na wenye kuaminika, maana wengine wanafanya kazi karibu sana na ofisi ya makoloni, na hawawezi kusema uongo. Huenda uvumi huo umetokana na maofisa wa ofisi ya makoloni, akanena.

Vidokezi Moshi

Hapo mjini Moshi kila mtu alikuwa akisema kuwa Thomas Marealle amechaguliwa kuwa Balozi wa Tanganyika katika nchi ya Uingereza. Wengine wakasema kuwa amechaguliwa kuwa Mkurugenzi katika idara ya Uhamiaji.

Lakini yeye mwenyewe amekanusha kuwa hajapewa taarifa na serikali juu ya kuwa Mkurugenzi, wala kuwa Balozi, isipokuwa anashangaa sana kupata pongezi kabla ya kupata taarifa kutoka serikali ya Tanganyika akiambiwa kama ameajiriwa kuwa Balozi.

Mwenyewe hana habari

Bwana Marealle alikataa kusema kama ni kweli alipata kuomba kazi katika serikali kuwa Balozi au Mkurugenzi katika Idara ya Uhamiaji. Lakini akanena kuwa yeye yuko tayari ikiwa ataitwa kushika nafasi kama hiyo.


26 tu hawana kazi Unguja!
Ngurumo, Alhamisi, Mei 21, 1964
 
SHEIKH Abeid Amani Karume, Makamu wa Rais wa Kwanza wa Jamhuri ya Muungano wa Tanganyika na Unguja, kawasihi watu wa Unguja, kusahau kabisa mambo ya ubaguzi na kila tofauti iliyokuwa inaletwa na rangi ya ngozi, huyu ni Mwarabu na huyu ni Mwafrika. Hii wasahau. Watu wakae pamoja kwa amani wajenge nchi.

Sheikh Karume ambaye alikuwa anahutubia mkutano wa hadhara, ailsema kuwa serikali italinda haki ya kila mtu ili watu wapate uhuru wa kufanya kazi kuleta ustawi.

Akaeleza juu ya mali iliyochukuliwa na serikali: Nyote mwafahamu, alisema Karume, kwamba nyumba, ardhi, zimechukuliwa. Basi hoteli, mikahawa na mejengo ya namna nyingine nyingine yataanza kujengwa hivi punde.

Sheikh Karume akaendelea kusema, kulikuwa na watu wapatao elfu tisa hapa nchini ambao hawakuwa na kazi kabla ya kumpindua Sultani. Sasa? Akahoji, wapo watu 26 tu ambao hawana kazi. Akatangaza kuwa kati ya Juni mosi mwaka huu, mtu wa taifa lolote ambaye hana kazi atapata alawensi.


Azimio la Arusha litaendelea kuelezwa - Nyerere
Uhuru Jumatano, Agosti 23, 1967
RAIS Nyerere amesema jana kwamba yeye na viongozi wengine wa TANU na wa serikali wataendelea kulieleza Azimio la Arusha mpaka lieleweke na shabaha zake zitimizwe.

Mwalimu ambaye alikuwa akizungumza na Maofisa wakuu wa Jeshi la polisi wanaokutana mjini Tabora, alisema kwa kuwa hata imani za dini ambazo zililetwa kwa njia ya Mitume badi zinaendelezwa kila Ijumaa na Jumapili, ni dhahiri kwamba Azimio la Arusha ambalo lilipitishwa miezi michache iliyopita, bado linahitaji kuelezwa zaidi.

Mwalimu alisema kutokana na kutawaliwa kwa muda mrefu, watu walianza kutia hofu za kuweza kujitawala, na wale waliotawala walizoea tabia ya kutawala na kuifanya kuwa ni haki yao. Kutokana na hayo, wale waliotawaliwa walijipendekeza kwa watawala na kutaka watambuliwe kama watu. Hata waliopata elimu wengine waliitumia elimu yao ili waweze kukubaliwa na kujionyesha kwamba wao walikuwa tofauti na wenzao. Mwalimu alisema huo ulikuwa ni uogonjwa nakwamba bado upo.

Vile vile Rais alisema wengine waliopata elimu waliitumia kuwapa matumaini wenzao na kuonyesha kwamba hata wao wanaweza kuwa na hali kama za watu wengine.

Mwalimu alisema usawa wa binadamu ni wa maumbile na haupatikani kwa kuombwa. Usawa wa binadamu huonekana tu na kukubalika bila mtihani wowote.

Alisema kwamba katika mataifa yaliyotawaliwa na kujipatia uhuru, yako mengine ambayo yanataka kupewa mtihani kupata haki ya usawa. Lakini pia, yapo mataifa ambayo hayahitaji mtihani, nayo huendelea kufanya shughuli zao na kujiona ni sawa na mataifa mengine.

Akizungumza juu ya maonevu katika Afrika, alisemaz; "hatuwezi kuitoa Afrika Mashariki hali ya kuonewa na kunyanyaswa kwa kupata Waafrika wachache wanaofanana na makabaila. Kontinenti letu litaheshimiwa kutokana na hali ya wananchi wote kwa jumla kwa kushirikiana katika kufanya kazi ya kuleta heshima hiyo", alisema Rais.

Akijibu maswali, Mwalimu alisema kwamba tamu ya kutawala ni uchumi. Na kwamba ugomvi kati ya nchi zinazojitawala na zile zilizokuwa zikitawala huzuka wakati nchi zile changa zinaposema kwamba kujitawala bila kushika uchumi, utawala huwa si kamili.


Yusi wa Frelimo sasa yachemka
 
VIJANA wa Youth ya chama cha watoro kutoka Msumbiji, Frelimo, watafanya maandamano kumgomea mweka hazina wa chama hicho, Bw. Mmole, sababu ni "mkoloni mweusi ambaye haja yake ni kushibisha tumbo lake".

Habari hizi zimeelezwa na taarifa kutoka Youth ya chama cha Frelimo ambayo imetiwa saini na makamu wa Katibu Mkuu wa Youth League.

Taarifa hiyo inaeleza kwamba maandamano hayo yatafanyiwa viongozi wote wa Frelimo kwa jumla.

Inaendelea. "Vijana wote wa Msumbiji, wake kwa waume, mnaombwa kuhudhuria katika ofisi yenu... ili kutayarisha maandamano... Tunamwomba Bw. Mmole atoe maelezo kamili ya kutia kwake saini ile taarifa iliyotoka Cairo na huku anajidai hajui chochote".

Taarifa hiyo inaendelea kueleza kwamba inasikitisha kwamba Halmashauri Kuu ya Frelimo haijatoa matamshi yoyote kuhusu kitendo cha Bw. Mmole mpaka hivi sasa.

Pia inaendelea kueleza kwamba wanatumaini kuwa shabaha ya Bw. Mmole ilikuwa kudumisha ukoloni katika Msumbiji - "jambo ambalo tunalipinga", yaeleza taarifa hiyo.

Juu RUDI


Bonyeza hapa
kushriki mjadala au kutoa maoni juu ya habari hizi na masuala mengineyo ya Kiislamu kwenye Baraza ya Wasomaji

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtz.org
 
An-nuur Home | Ukurasa wa Mwanzo | Islam Tanzania 
Links | Matoleo Yaliyopita | Sign our Guestbook