MASHAIRI
 
 
Jerusalem tuililie
 

Ya Rabi tunakuomba, salama utupatie,
Makosa tuliotenda, ya Illahi tughufirie,
Sasa saa imefika, salama tushuhudie,
Amani ni fursa adhim, Jerusalem tuililie.

Mafanikio tuone, Jerusalem itungarie,
Jerusalem ni nyumbani, sote tukasalimie,
Tumerithi kwa Nabii Ibrahimu (a.s.) utufaidikie,
Amani ni fursa adhim, Jerusalem tuililie.

Jerusalem ni Al-Quds, vitabu tuvijulie,
Imejengwa kinadhifu, Waislamu tujivunie,
Mji huu mtukufu, ya Illahi tubarikie,
Amani ni fursa adhim, Jerusalem tuililie.

Wakati wa sasa umewadia, Jerusalem itung'arie,
Rehma nyingi tuombe, na mema tujifanyie,
Tuwache mtafaruku, umoja tujivunie,
Amani ni fursa adhim, Jerusalem tuililie.

Masjid Al-Aqsa, ni adhim ziara tujifanyie,
Safari zinyepesi, Hajj Trust ituandalie,
Al-Quds ni aziz ziara, za kheri tujifanyie,
Amani ni fursa adhim, Jerusalem tuililie.

Kisa cha Miraj kitukufu, sote tukifatilie,
Safari ya Rasul Llah (s.w.), adhim tuizingatie,
Dini ya Kiislamu, kamilifu ibada tujifanyie,

Amani ni fursa adhim, Jerusalem tuililie.
Imani Tawhiid, na Taqwa sote tujihimize,
Kamba ya Ikhwani, imara wajibu tuishikilie,
Hii itajenga imani, na umoja itupatie,
Amani ni fursa adhim, Jerusalem tuililie.

Ikhwani wa Palestine, Yarabi uwajaalie,
Subra kubwa wapate, dhambi uwaghufurie,
Neema uwapatie, na Dar-Ul-Salaam uwajaalie,
Amani ni fursa adhim, Jerusalem tuililie.

Shairi si fani yangu, watalaam mnisahishie,
Hili ni langu la kwanza, hivyo munisaidie,
Makosa niliofanya, ya Illahi nighurufie,
Amani ni fursa adhim, Jerusalem tuililie.

Dr. Amur Abdullah Amur,
Dar es Salaam.


Kuweka kali halali?
Kwa jina la Maualana, ya Illahi ya Rabuka,
Ninamshukuru sana, kwa uwezo alonipa,
Nguvu kanijaalia,ya shairi kuandika,
Kuweka kali halali, amri katoa nani.

Kwa kweli ninashangazwa, na vijana wa kisasa,
Mambo wanayavamia, bila hata kuchunguza,
Mwisho wanakurupuka, na kuanza kutangaza,
Kuweka kali halali, amri katoa nani.

Kabla hatujatangaza, yatupasa kuchunguza,
Kwa vitabu kuvisoma, na watu kuwauliza,
Majibu ukiyapata, sasa kaa na chunguza,
Kuweka kali halali, amri katoa nani.

Mola katofautisha, binadamu na wanyama,
Akili katujaalia, tofauti na wanyama,
Mambo kujichunguzia, kabla hatujayafanya,
Kuweka kali halali, amri katoa nani.

Kufanya hivyo ni bora, kuliko kusemezana,
Tutajenga umma bora, bila hata kuzozana,
Tutamrisha Mola , na Islamu jamia,
Kuweka kali halali, amri katoa nani.

Bibi Aisha kasema, Mtume alifundisha,
Laana itawapata, wanawake hapa hapa,
Nyuso zao kukwaruza, na nywele kubadilika,
Kuweka kali halali, amri katoa nani.

Sasa inaonekana, tayari imewapata,
Kwani wamekengeuka, nywele mpya kubandika,
Wamkosoa Muumba, kwa hiba aliowapa,
Kuweka kali halali, amri katoa nani.

Mimi wananishangaza, wanaopenda kuweka,
Amri wanakiuka, aloiweka Rabuka,
Eti wanadai kwamba, waume zao wapenda,
Kuweka kali halali, amri katoa nani.

Harufu mbaya hutoa, jua linapowapiga,
Madhara mengi hupata, kwa vidonda kuwatoka,
Na mainzi kuwafuata, kama wabeba mizoga,
Kuweka kali halali, amri katoa nani.

Tamati na tamatia, ujumbe huu sikia,
Kalamu naiachia, ujumbe kukufikia,
Sasa kazi ninawapa, kuanza kufuatilia,
Kuweka kali halali, amri katoa nani.

Jabiri Bakari wa Kibasira,
MSAUD (MTP) Form III,
Survey, Dar es Salaam.



Nguo fupi (swali)
1. Hili latuhuzunisha, nguo fupi mitaani,
Tena zina kerehesha, nizionapo mwilini,
Nguo zisisitirisha, aibu siyo kifani,
Wetu vigogo nchini, kwanini mwakaa kimya?

2. Nguo zinahuzunisha, mwajitia matatani,
Waume kutamanisha, zinachangia kuzini,
Jamii zatukanisha, zawatia utumwani,
Wetu vigogo nchini, Kwanini mwakaa kimya?

3. Nguo hadhi zawashusha, sawa kama punguani,
Unyama kudhihirisha, nyuso haya hazioni,
Mavazi haya yachosha, kila muda twalaani,
Wetu vigogo nchini, Kwanini mwakaa kimya?

4. Na ukweli waonyesha, wasivyo kuwa makini,
Uchi wajitembezesha, afadhali punguani,
Kwanini mwajidumisha, na kujishusha thamani,
Wetu vigogo nchini, kwa nini mwakaa kimya?

5. Kwa nini mwajiuzisha, kusiko taadhimani,
Nyie mwajishughulisha, kujitoa heshimani,
Vichupi mwajivalisha kuzagaa hadharani,
Wetu vigogo nchini, kwanini mwakaa kimya?

6. Ubakaji kuzidisha, jamii matatizoni,
Na lisilo pendezesha, kwanini kulithamini,
Kwenu nyie mwajikosha, msiwekwe hatiani,
Wetu vigogo nchini, kwanini mwakaa kimya?

7. Sio kuwa na watisha, tu ninauthamini,
Ndo maana nawajulisha, miili isitirini,
Heshima mtapandishwa, vaa vimini chumbani,
Wetu vigogo nchini, kwa nini mwakaa kimya?

8. Nyie zawafurahisha, nguo fupi mapajani,
Kwao nyie mwajikosha, msiwekwe lawamani,
Twaomba kuwasitisha, mwaogopa kitugani,
Wetu vigogo nchini, kwanini mwakaa kimya?

9. Twashauri kupitisha, sheria zilo makini,
Sio kuwachelewesha, kwani wanawapa nini,
Hapa ninahitimisha, nguo fupi kumuni,
Wetu vigogo nchini, kwanini mwakaa kimya?

Abdull Rawph B. Ally
P.O. Box 157,
Hai-Moshi


Tufurahike waumini mwaka mpya kutujia

1. Bismillahi Rahamani, kwa jina lake Jalia,
Maliki wa duniani, na akhera yote pia,
Sifa zake kila shani, nashindwa kuelezea,
Tufurahike waumini, mwaka mpya kutujia.

2. Ni mwaka wa Kiislamu, idadi twahesabia,
Hesabu ya Kiislamu, mwanzo ilipoanzia,
Moja nne tarakimu, mbili ziro kufatia,
Tufurahike waumini, mwaka mpya kutujia.

3. Alipohama rasuli, madina kuelekea,
Kwa idhiniya Jalali, dini ipate enea,
Hakujali hata mali, na anasa za dunia,
Tufurahike waumini, mwaka mpya kutujia.

4. Twamtolea pongezi, kwa moyo alioutoa,
Kwa uwezo wa Mwenyezi, amri aliitikia,
Kuitekeleza kazi, nuru ipate enea,
Tufurahike waumini, mwaka mpya kutujia.

5. Masahaba nao pia,, salamu twawatolea,
Kwa moyo walioutoa, mtume kumsaidia,
Safarini kuelekea, katika mwaka hijria,
Tufurahike waumini, mwaka mpya kutujia,.

6. Kushukuru ni lazima, kwa yule ulimjia,
Kwa kuuwahi mzima, na uhai kubakia,
Wangapi wameshazama, kaburini wametua,
Tufurahike waumini, mwaka mpya kutujia.

7. Ndugu yenu Sulemani, kalamu naiachia,
Nasubiri gazetini, shairi litapoenea,
Shime ndugu waumini, nasaha kuzingatia,
Tufurahike waumini, mwaka mpya kutujia.

Suleiman Mohamed Abdalla
P.O. Box 5252,
Dar es Salaam


Kiti Moto (1)

Bismillahr-Rahmani; Allah Mola jalia;
Leo naishika peni, na mdomo kuinua,
Yamekithiri jijini, maudhi yamezidia,
Kitimoto hadharani, ni wapi twaelekea?

2. Kitimoto mabuchani, dhahiri yaning'inia,
Mabango barabarani, alama kuashiria,
Kuwa huko kuliani, kitimoto kimejaa,
Kitimoto hadharani, Luanda nimechukia.

3. Kitimoto mitaani, hufugwa kama ngamia,
Wanaranda majaani, kama kuku mezagaa,
Ni kero mchikichini, mishikaki jichomea,
Kitimoto hadharani, kwa nini twavumilia?

4. Kitimo hasa nani, anayekifurahia,
Anayewapa leseni, kero kutuongezea,
Amekataza manani, yeye wapi ametoa,
Kitimoto hadharani, kuuza ati yafaa??

5. Kitimo mitaani, tume itatuambia,
Hivi kwa sheria gani, leseni yawapatia,
Nchi isiyokuwa na dini, nguruwe yakumbatia!!!
Kitimoto hadharani, ni hapo ninapoanzia!

6. Kitimo tangu lini, ruhsa kuning'inia?
Au ni kigogo gani, moto anayechochea,
Anachokitaka nini, midomo tukiinua?
Kitimoto hadharani, Tukianza kukemea?

7. Mauaji ya jijini, ndivyo yalivyoanzia,
Paroko yake maoni, Dola ikamwitikia,
Mwembechai magomeni, serikali imeua,
Kitimoto hadharani, we haya!! malizia!!!

8.Kitimoto mabuchani, jiji mwatuchafulia,
Keenja kama huoni, haifai nyamazia,
Madhara yake pomoni, na maradhi mengi pia,
Kitimoto hadharani, balaa mwatutakia.

9. Kitimoto asilani, hatutakivumilia,
mazingira hatarini, mengi hima kiondoa,
Tunamuudhi Manani, nini tutamuambia,
Kitimoto hadharani, wapi tunaelekea.

10. Kitimoto hamuoni, masheikh mkakemea,
Kimara barabarani, makongo kwingine pia,
Kimya chenu cha nini, mabaya kunyamazia,
Kitimoto hadharani, masheikh shime kemea.

11. Kitimoto kipingeni, ikulu, bungeni pia,
Tulaani hadharani, unyama uharamia,
Wa kuzitoa leseni, nguruwe kutuuzia,
Kitimoto hadharani, kwa pamoja twakemea.

K.S. Luanda (Nolo)
Dar es Salaam



Cheo ni Dhamana Na. 1

1. Kila mara utambuwe, kuwa cheo ni dhamana,
Hicho kisikuzuzuwe, kujiona wa maana,
Wakumbuke uwajuwe, ambao leo hawana,
Cheo ni dhamana.

2. ushikapo madaraka, mjumbe ama Mbunge,
heshima yako yataka, kwa wananchi uchunge,
Isije kuharibika, mawazo nao uchange,

Cheo ni dhamana.

3. Cheo kiko kama maji, huingia na kutoka,
Kitapotoka hakiji, mwingine atakishika,
MUNGU ndie mtoaji, humpa anayetaka,
Cheo ni dhamana.

4. MBUNGE kuwa mkweli, msiwe waongo-ongo,
Mnapoliliwa hali, toweni wenu mchango,
Msitafute muhali, wala kuleta maringo,
Cheo ni dhamana.

5. Tamati KUCHAGULIWA, angalia uendako,
KURA msipopigiwa, utapata maumbuko,
Na ukweli utajuwa, punguza MARINGO yako,
Cheo ni dhamana.

Yahya O. Barshid (Yob)
Madaraka Hote
Morogoro.
 

Juu RUDI


Bonyeza hapa
kushriki mjadala au kutoa maoni juu ya habari hizi na masuala mengineyo ya Kiislamu kwenye Baraza ya Wasomaji

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtz.org
 
An-nuur Home | Ukurasa wa Mwanzo | Islam Tanzania 
Links | Matoleo Yaliyopita | Sign our Guestbook