MASHAIRI
 
 

Kuweka kali halali? (Sapoti)

Bismillahir naanza, kwa jina lake jaalia,
Nataka kuwaeleza, yale yalotangulia,
Mwenzetu katueleza, Mungu alomjalia,
Kuweka kali haramu, kwa amri yake Mola.

Amri ni yake Mola, Jabiri nakuambia,
Mola kaiharamisha, na Mtumewe pia,
Laana wameahidiwa, wale walokaidia,
Kuweka kali haramu, kwa amri yake Mola.

Wanashangaza hakika, wale wanaojisifia,
Eti wao wanataka, mume kumfurahisha,
Huku linaharibika, umbo lao asilia,
Kuweka kali haramu, kwa amri yake Mola.

Laana ikikupata, nani takusalimisha,
Faida utayopata, hakuna wakumshirikisha,
Madonda utayapata, nani atakuponesha,
Kuweka kali haramu, kwa amri yake Mola.

Mola katutunukia, umbo linalopendeza,
Na nywele akatujalia, ili kichwa kukijaza,
Wala hakutuambia, kali kuitumbukiza,
Kuweka kali haramu, kwa amri yake Mola.

Hijab inawatoka, kali wanapojitia,
Kote kote watataka, kali kujionyeshea,
Madhara yatawafikia, si yakujijutia,
Kuweka kali haramu, kwa amri yake Mola.

Mungu ametuambia, yale aliyokataza,
Naye akatuambia, sheria zenye kuongoza,
Nakuweka pia, Mungu ametukataza,
Kuweka kali haramu, kwa amri yake Mola.

Tamati natamatia, ujumbe huu siku,
Jabiri kumsaidia, yale alohubiria,
Dini kuizingatia, kwa mujibu wa sheria,
Kuweka kali haramu, kwa amri yake Mola.

Fatma Saleh,
Kibasila Sec. School,
P.O. Box 20378,
Dar es Salaam.



Wamefika kwa Hakimu?

Nuun, Walkalamu, sisitizo maalum,
Nakumbusha ile damu, ilomwagwa ki haramu,
Ni kina cha dhalimu, kuuwa Islamu,
Wale walomwaga damu, wamefika kwa hakimu?

Amani kweli ni tamu, tena haitaki hamu,
Amani, dhuluma sumu, huifanya isidumu,
Amani sitege bomu, itakua ni adimu,
Wale walomwaga damu, wamefika kwa hakimu?

Nasema kwa baragumu, nifike Dar es Salaam,
Waikulu na Makamu, sikieni mfahamu,
Kufukia majukumu, huo si utalaamu,
Wale walomwaga damu, wamefika kwa hakimu?

Kukumbusha kwa kalamu, malenga yanilazimu,
Sera hii ni muhimu, dhuluma iseje dumu,
Uhai wa binadamu, polisi wa uheshimu,
Wale walomwaga damu, wamefika kwa hakimu?

Mmepewa majukumu, siyo ya kutudhulumu,
Msifanye kichwa ngumu, kupindisha gurudumu,
Katiba muiheshimu, itengemae kaumu,
Wale walomwaga damu, wamefika kwa hakimu?

Raia kuwadhulumu, mwatega nchini bomu,
Msije mkalaumu, Usama kumshutumu,
Mkae mkifahamu, wenyewe metega bomu,
Wale walomwaga damu, wamefika kwa hakimu?

Litakapo fumuka bomu, maisha itagharimu,
Hatapona Muhashamu, wala alo mkarimu,
Itakuwa ni karamu, yakutaja marehemu,
Wale walomwaga damu, wamefika kwa hakimu?

Yadola hii nidhamu, yapanda mbegu yasumu,
Iweje siwe vigumu, kumwaga za watu damu?
Tena yafanya karamu, kupongeza udhalimu?
Wale walomwaga damu, wamefika kwa hakimu?

Nuun chini kalamu, YOB jihadi muhimu,
Nuun zangu salamu, Sabala, Nolo jihimu,
Nuun letu jukumu, kutetea Islamu,
Nuun Walkalamu, nimefika kwenye qhatamu.

Yusuf A. Juma,
Dar es Salaam.



Bakwata si taasisi ni chombo cha Dola

Tumejionea kweli, Bakwata si taasisi,
Kwani hudhoofisha hali, kwa dini kuwa nyepesi,
Yakiukwa maadili, Qur’ani kuiasi,
Bakwata si taasisi, ni chombo cha serikali.

Ni chombo cha serikali, Bakwata si taasisi,
Tunayo mambo mawili, nukau tukidadisi,
La kwanza Idd kusali, ingekuwa Jumamosi,
Bakwata si taasisi, ni chombo cha serikali.

Mauaji kikatili, Mwembechai ni mkosi,
Haikutoa kauli, ama suala kufosi,
Na wala kulijadili, lau dua Ikhilasi,
Bakwata si taasisi, ni chombo cha serikali.

Tulifanya muhimili, kama chombo mkutasi,
Matatizo kukabili, kusimamia kesi,
Tunafanya ujahili, kuyapongeza maasi,
Bakwata si taasisi, ni chombo cha serikali.

Bakwata ni chetu chombo, kilichoshika hatamu,
Ingeshika yake fimbo, kutetea Isilamu,
Ilishikilia tumbo, kuubwaga Uislamu,
Bakwata si taasisi, ni chombo cha serikali.

Chombo cha Waislamu, weupe pia weusi,
Chakuongoza kaumu, twakipamba na lebasi,
Sasa chageuka sumu, ni shetani Ibilisi,
Bakwata si taasisi, ni chombo cha serikali.

Lazima tujilaumu, kwa makundi na vikosi,
Na tuchagueni timu, tupunguze hii kasi,
Viondolewe haramu, vile tunavyo vihisi,
Bakwata si taasisi, ni chombo cha serikali.

Tuchunguzeni ujinga, baadhi kutosubutu,
Bakwata walivyopanga, Idd mfungo tatu,
Na hali tukielewa, hatufungi siku mbili,
Bakwata si taasisi, ni chombo cha serikali.

Kamati ya Wanawake wa Kiislamu,
Tawi la Gongo la Mboto,
Dar es Salaam.



Wake kudai talaka (swali)

Habari zinasikika, kupitia gazetini,
Wake kudai talaka, madai mahakamani,
Hivi kweli tutafika, hasa sisi waumini,
Wake kudai talaka, sheria au ubabe?

Mahakama kitwaghuti, kuamuwa waumini,
Hamuoni tafauti,  tunajitowa Manani,
Wakati hautupiti, sasa tujikwamueni,
Wake kudai talaka, sheria au ubabe?

Ndoa zetu madhubuti, sheria za vitabuni,
Amri hiyo thabiti, tangu enzi za zamani,
Na ndani ya Taurati, imenenwa usizini,
Wake kudai talaka, sheria au ubabe?

Wake kwenda kwa pilati, talaka kuzibaini,
Huwa kwetu misibati, kama sisi tuna dini,
Sawa wale Wagalatia, hawana matumaini,
Wake kudai talaka, sheria au ubabe?

Nimefanya utafiti, sababu zake ni duni,
Kama sale hawapati, wanaanzisha uhuni,
Na ngoma ya benibati, ruhusa mukiwahini,
Wake kudai talaka, sheria au ubabe?

Temeke na katikati, kwingine kote nchini,
Kila mwenye hisabati, ndoa kitu cha thamani,
Tuacheni usharati, mabalaa hamuoni,
Wake kudai talaka, sheria au ubabe?

Sisi wanaharakati, sasa tukae makini,
Dini iwe katikati, kwa sheria hukumuni,
Tusipitwe na wakati, itakuwa mtihani,
Wake kudai talaka, sheria au ubabe?

Hapa mimi ni tamati, enyi wake waumini,
Mkae mjizatiti, ndoa zenu heshimuni,
Na muzifatie shuruti, waume zetu tiini,
Wake kudai talaka, sheria au ubabe?

Zuberi Mohammed Mwinyi (Amir),
S.L.P. 61428,
Dar es Salaam.



Swala kufunga shingoni

Leo nashika kalamu, ili niwaulizeni,
Munijibu Islamu,  siwaulizeni misheni,
Masheikh na Maimamu, talamidhi darasani,
Kufunga swala shingoni, mwafata Imamu gani?

Mwafata Imamu gani, nawauliza kaumu,
Au ni Mtume gani, hayo ameyahukumu,
Mubaini aya gani, kwenye kitabu adhimu,
Kufunga swala shingoni, mwafata Imamu gani?

Siyo ninawalaumu, walosoma Arabuni,
Bali nimepata hamu, nielewe kwa makini,
Ni kauli ya Imamu, kufunga swala shingoni,
Kufunga swala shingoni, mwafata Imamu gani?

Kugawanyika kaumu, kwa mote Misikitini,
Kama hatuna elimu, jambo hili kitu gani?
Mwisho tuende Jahimu, kwenye nari abadan,
Kufunga swala shingoni, mwafata Imamu gani?

Selemani na Salimu, komesheni ushindani,
Kwa barua hata simu, mueneze mikoani,
Aliosema Karimu, humo kwenye Qur’ani,
Kufunga swala shingoni, mwafata Imamu gani?

Kwa matangazo adhimu, yaliyotoka zamani,
Kwa yeyote Islamu, swala ifungwe tumboni,
Leo twaona jukumu, vipi mwafunga shingoni?
Kufunga swala shingoni, mwafata Imamu gani?

Yameanza humu humu, au nchi za kigeni?
Ni kweli yana muhimu, ni mbinu za Marekani,
Wao wameshika zamu, nia yao farakani,
Kufunga swala shingoni, mwafata Imamu gani?

Kama yametoka Rumu, ni vizuri mbaini,
Ikiwa Darisalaamu, au Pemba mkoani,
Au ni Mombasa Lamu, ushahidi elezeni,
Kufunga swala shingoni, mwafata Imamu gani?

Mimi si mwenda wazimu, nina akili kichwani,
Kama nimewadhulumu, nawaomba samahani,
Nia yangu ni elimu, Injili na Kuruani,
Kufunga swala shingoni, mwafata Imamu gani?

Kaditama ninazamu, nakwenda zangu chuoni,
Nawangojea Ghulamu, walio Bara na Pwani,
Wanijibu kielimu, yatulie akilini,
Kufunga swala shingoni, mwafata Imamu gani?
 

--

Juu RUDI


Bonyeza hapa
kushriki mjadala au kutoa maoni juu ya habari hizi na masuala mengineyo ya Kiislamu kwenye Baraza ya Wasomaji

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtz.org
 
An-nuur Home | Ukurasa wa Mwanzo | Islam Tanzania 
Links | Matoleo Yaliyopita | Sign our Guestbook