MASHAIRI
 
 

Cheka na langu shairi

Cheka na langu shairi, siasa zitafakari,
Uzichunguze habari, sera nyingi ni za shari,
Ubabe uko dhahiri, hadharani si kwa siri,
Cheka na langu shairi, tumo katika hatari.

Cheka na langu shairi, tulia utafakari,
Dhulma imekithiri, si wakati wa zumari,
Acha karata, golori, bao lifunge kufuri,
Cheka na langu shairi, tumo katika hatari.

Cheka na langu shairi, akilini ufikiri,
Vipi haki isafiri, wakati huna habari,
Wewe kweli ni mahiri, wa kujipa uhodari,
Cheka na langu shairi, tumo katika hatari.

Cheka na langu shairi, nyimbo miziki ghururi,
Utaleweshwa chakari, ushindwe kutafakari,
Hutoweza kufikiri, kuzipembua habari,
Cheka na langu shairi, tumo katika hatari.

Cheka langu shairi, pande tupige viburi,
Tuchukue tahadhari, tuchore na mstari,
Watambue si vizuri, ubabe na ukahari,
Cheka na langu shairi, tumo katika hatari.

Cheka na langu shairi, unafiki si mzuri,
Ukatumiwa kwa siri, kuchota zetu habari,
Ufanyayo ya hatari, kutumikia kafiri,
Cheka na langu shairi, tumo katika hatari.

Cheka na langu shairi, yangu maneno sukari,
Usifanye uhodari, kusema kila habari,
Zingine ufanye siri, ziweke uzisitiri,
Cheka na langu shairi, tumo katika hatari.

Idd Kikong’ona,
Morogoro.


Haki

Sineni nao wazee, namba vijana mliko,
Leyo niwadokezee, akili zifanye shiko,
Kila siku mutetee, vyenu visende kusiko,
Uwatapo haki yako, nani akuokotee?

Akuokotee nani, uwatapo haki yako,
Kutwa wajifanza duni, hewala tamko lako,
Huwo ni uhayawani, chunga sana bongo lako,
Uwatapo haki yako, nani akuokotee?

Huwa haiombwi haki, leyo mufanye zinduka,
Hutwaliwa kwa mikiki, ya juu hwendewa huko,
Bora wambwe balamaki, kuata ni dhara kwako,
Uwatapo haki yako, nani akuokotee?

Tetea kwa kulla hali, sihofu misukosuko,
Namba kwa mwene akili, aso na mawazo koko,
Kuporwa usikubali, kubali ufe kwa chako,
Uwatapo haki yako, nani akuokotee?

Mtu hakiyo afite, afite kwene mfuko,
Asiitike umwite, aondoke kwa katiko,
Bora teke mkung’ute, ende kefu aendapo,
Uwatapo haki yako, nani akuokotee?

Ni amri ya Sattari, M’mi si langu tamko,
Kutwaa siyo dosari, haki kwa huku twendako,
Kaditamati shairi, nakoma hili andiko,
Uwatapo haki yako, nani akuokotee?

“Kuhani Mkuu”,
Iddi M. Mwassa (Pilato),
S.L.B. 15789,
Dar es Salaam.



Acheni mkorogo
 

Bismillahi baswiyru, mbora wa walimwengu,
Vibaya kumkufuru, Muumba wa saba mbingu,
Nyingine sifa bashiru, si mwingine bali Mungu,
Acheni kujichubua, tamaduni yapotea.

Tamaduni yapotea, acheni kujichubua,
Ngozi zenu mwasumbua, kwa yenu hiyo tabia,
Weupe jitafutia, mudhaniwe Waasia,
Acheni kujichubua, tamaduni yapotea.

Shindanoni Namibia, nani asoshuhudia?
Ushindi jitafutia, wengi walijichubua,
Mweusi alichukua, mkorogo walilia,
Acheni kujichubua, tamaduni yapotea.

Rangi nyeusi ni yetu, Mola katujaalia,
Yeye kapendeza kwetu,  asili tambulisha,
Tunaupoteza utu, tusipojivunia,
Acheni kujichubua, tamaduni yapotea.

Weupe mukishapata, madharae mwayaona,
Ajali ikiwakuta, ni vigumu kuwashona,
Tena zaidi matata, nyuzi ngozi inachana,
Acheni kujichubua, tamaduni yapotea.

Ndugu zangu kwaherini, kalamu naweka chini,
Shairi mulishikeni, tena lizingatieni,
Yalosemwa ni yakini, amini usiamini,
Acheni kujichubua, tamaduni yapotea.

Said Mkama,
Box 65,
Mtwara.


Kufunga swala shingoni (jibu)
 

Assalaamu alaykum, ewe ndugu Isilamu,
Leo nina kubwa hamu, kukupa jibu adhimu,
Kwa kauli ya karimu, Mola wa yote kaumu,
Kufunga swala si nguzo, ni Sunna twatekeleza.

Kufunga swala shingoni, au mikono achia,
Au kufunga tumboni, kifua hujakosea,
Jiondoe mashakani, fanya ulilozowea,
Kufunga swala si nguzo, ni Sunna twatekeleza.

Usemapo neno swala, yapo yake ya lazimu,
Kwanza iwe na twahara, na wakati ufahamu,
Jambo jingine sitara, na Qibla ukufahamu,
Kufunga swala si nguzo, ni Sunna twatekeleza.

Swala ina zake nguzo, kumi na saba bayana,
Kati ya zote hizo, kufunga swala hamna,
Usijezuka mzozo, na watu kufarakana,
Kufunga swala si nguzo, ni Sunna twatekeleza.

Mtume mfano mwema, kiigizo cha dunia,
Mikono hakuachama, kifuani kashikia,
Ndugu yangu muadhama, Mtume fuatilia,
Kufunga swala si nguzo, ni Sunna twatekeleza.

Kuna mengi malumbano, mijini na vijijini,
Wengine waseme tumbo, na wengine kifuani,
Iondoke minong’ono, sira irejeeni,
Kufunga swala si nguzo, ni Sunna twatekeleza.

Tamati nimefikia, naweka yangu kalamu,
Jambo hili zingatia, ndugu yangu Isilamu,
Kufunga swala sikia, ni jambo lisolazimu,
 Ni  Sunna ya Muhammadia, si ya Shekhe wala Imamu.

Zuhura Uwesu Mashaka,
P.O. Box 55105,
Dar es Saalam.


Yafaa? Na. 1
 

Enyi wajuzi wa mambo, werevu ulowajaa,
Watofautisha shombo, la samaki na dagaa,
Ninawauliza jambo, munambe kama yafaa,
Kumsaliya yafaa, mja mfu asosali?

Watongozi tongoweni, tujuwe dowa na waa,
Kwa mja muasi dini, kusali alokataa,
Haya nambeni yakini, kumuombeya duwaa,
Kumsaliya yafaa, mja mfu asosali?

Sikuwaumba majini, na binadamu lwaa,
Kasema niabuduni, mnena haya Shufaa,
Mja anapo jihini, kusali aseme kaa,
Kumsaliya yafaa, mja mfu asosali?

Kaishi kwenye duniya, toka kuzaliwa ng’aa,
Kala na kujilaliya, waa kaona bidaa,
Yaswih akijifiya, kumsaliya jamaa?
Kumsaliya yafaa, mja mfu asosali?

N’jibuni “shaziliya”, msipoteze wasaa,
Nawadhehebu la “Shiya”, ka’tu msije bung’aa,
Nambeni “Ahamadiya”, mfaa huyu si kinyaa!
Kumsaliya yafaa, mja mfu asosali?

Wa Kadiriya dhehebu, nyuma msije zubaa,
Mtu mchapa sharabu, kunwa bia na chang’aa,
Afapo naye wajibu, kumsaliya jamaa?
Kumsaliya yafaa, mja mfu asosali?

Kalamu haiandiki, naibwaga tini pwaa,
Waja mlosoma fiq, hususan Ulamaa,
Haya kamateni biki, munipe hii fatwaa,
Kumsaliya yafaa, mja mfu asosali?

“Kuhani Mkuu”,
Iddi M. Mwassa (Pilato),
P.O. Box 15789,
Dar es Salaam.
--

Juu RUDI


Bonyeza hapa
kushriki mjadala au kutoa maoni juu ya habari hizi na masuala mengineyo ya Kiislamu kwenye Baraza ya Wasomaji

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtz.org
 
An-nuur Home | Ukurasa wa Mwanzo | Islam Tanzania 
Links | Matoleo Yaliyopita | Sign our Guestbook