Na Elia Batendi
NIMEKUWA nikifuatilia kwa makini makala zote nane (8) za Bw. Muhibu Said kuhusiana na hoja ya "Je, Yehova na Allah ni miungu tofauti?" Katika makala hizo, Bw. Muhibu ameelezea kwa kirefu sifa za Yehova na Allah kuwa ni moja na hakuna hata mmoja wao aliyepungukiwa na sifa hizo, na hivyo kuonekana kuwa Yehova na Allah ni Mungu mmoja aliyejifunua kwa Manabii kwa majina mbalimbali. Hata hivyo, Bw. Muhibu ametuacha na kiu ya kujua mengi kwani hoja nyingi za msingi ameziacha bila majibu.
BW. MUHIBU amefanya kazi kubwa sana ya kumjibu mtu aliyemwita "mtaalamu wa magonjwa ya kina mama Muhimbili". Amefanya kazi kubwa kwa sababu kazi ya kuandika na kutafuta rejea katika vitabu vya dini ni kubwa na nzito inayohitaji muda wa kutosha. Katika makala zake Bw. Muhibu amezitaja sifa za Yehova na Allah kuwa ni moja na hivyo ni Mungu mmoja, sifa hizo ni:
Uuumbaji Mw. 1:1, Qur. 6:100-102
Kuwepo kabla ya vitu vyote Isa. 41:4, Qur. 57:1-3.
Upweke Isa. 44:6-8, Qur. 6:162-163.
Kutokuwa na nafsi Isa. 45:21-23, Qur. 5:116.
Kutobadilikabadilika Zab. 102:24-27, Qur. 33:62
Kutochoka Isa. 40:28, Qur. 50:38.
Kutokufa Za. 102:24-27, Qur. 28:88.
Ukuu Kumb. 10:19, Qur. 31:30.
Uweza Ay. 37:23, Qur. 57:1-2.
Kutofanana na kitu Kumb. 33:26, Qur. 42:11.
Kutoonekana Kumb. 4:12, Qur. 6:102-103.
Sifa hizi na nyingine nyingi ambazo Mungu Yehova na Allah wanazo na hivyo kuwa ni Mungu mmoja aliyejifunua kwa Manabii kwa majina mbalimbali, zimeelezewa vizuri na Bw. Muhibu. Kitu ambacho Bw. Muhibu hakukielezea wazi na hivyo kunifanya mimi na wengine waliokuwa wanafuatilia hoja hizo na kutufanya tuamini kuwa ametuacha na kiu ni kutoelezea kwa uwazi kwa nini miungu hawa wanapingana pamoja na kwamba wana sifa moja.
Aidha, Bw. Muhibu anatakiwa avunje hoja za huyo "mtaalamu wa magonjwa ya wanawake" kuwa kufanana kwa Yehova na Allah katika zao, siyo hila (Qur. 3:54) na jinsi inavyoelezwa katika Isaya 14:14, "Nitaapa kupita vimo vya mawingu NITAFANANA naye aliye juu". Hoja zinazotakiwa kuvunjwa ni kama ifuatavyo ili Yehova na Allah aonekane ni Mungu mmoja asiyepingana:
Majina ya Yehova kama vile Baba (Yer. 3:19), Bwana wa Majeshi (Zab. 24:10), Mungu wa Israel (Isa. 1:24) na kadhalika yangekuwemo katika majina 99 ya Allah kwa kuwa ni Mungu mmoja. Mungu Yehova mji wake uliotukuka ni Yerusalem (Zab. 48:8, Isa. 60:14) siyo kwa muda tu hata baada ya kiama (Uf. 21:2), mji wa Allah uliotukuka ni Maka (Qur. 27:91). Mungu Yehova anawapenda Israel (Yer. 31:3) na atawatupilia mbali iwapo misingi ya dunia itaweza kugunduliwa (Yer. 31:37). Mungu Allah anasema Mayahudi ndio maadui wabaya kuliko wote (Qur. 5:82). Yehova amekataza uhusiano na washirikina, ameagiza mahala wanapofanyia ibada pabomolewe, pavunjwe-vunjwe (Kut. 34:10-14) Allah ameagiza mahala hapo pafanyiwe ibada ya kusai (Qur. 2:158). Yehova hufanya maagano yake kwa damu. Alifanya agano na Ibrahim akamwagiza achinje njiwa (Kut. 15:7-10) ili kumhakikishia Ibrahim kuwa uzao wake utarithi nchi ya Kanaani katika tukio hilo Mungu Allah anawafufua njiwa hao kuonyesha uwezo wake wa kufufua na wala siyo agano. Mungu Yehova naamuru kuchinja mnyama wa Pasaka na damu ipakwe katika mlango wa kila mwana Israel iwe ni alama aya kukombolewa (Kut. 12:13). Mungu Allah anasema alimpa Musa ishara tisa tu (Qur. 17:101) tukio la damu halitajwi. Mungu Yehova anasema yalikuwa ni mapenzi yake Yesu auawe na damu yake iwe ondoleo la dhambi (Isa. 53:10). Mungu Allah anasema hawakumuua (Qur. 4:157).
Orodha ya hoja ambazo Bw. Muhibu anatakiwa kuzijibu ili kuondoa shaka kwamba Yehova na Allah si Mungu mmoja zinaendelea kama ifuatavyo: Mungu Yehova anakataza kuapa kwa uongo (Wal. 19:12) hata kwa neno dogo la upuuzi (Mat. 12:36) Mungu Allah hatatushika kwa sababu viapo vyetu vya upuuzi (Qur. 2:225 na 5:89). Yehova anatuvumilia sana (Zab. 86:15) na hutunyeshea mvua wema na wabaya (Mat. 5:45). Mungu Allah huwatuma mashetani kwa makafiri ili kuwachochea mabaya, (Qur. 19:83). Yehova anakataza uhusiano wetu na majini (Wal. 17:7) Allah alituma kundi la majini kwa Nabii Muhammad wasikilize Qur'an na baadhi yao wameamiani (Qur. 46:29 na 72: 1-2).
Kwa kweli pamoja na Bw. Muhibu kuelezea kwa ufasaha sifa za Yehova na Allah kuwa ni moja na hivyo kuonekana ni Mungu mmoja, lakini bado hoja hizi za Mungu mmoja anayepingana hazijajibiwa. Kwa kuwa Bw. Muhibu ameonyesha ufahamu wa dini ni bora kwanza afafanue ni vipi miungu hawa wanapingana, kuliko kutumia muda mwingi kuzungumzia uungu wa Yesu au kumshutumu Mtume Paulo. Suala la Yesu mwana wa Mungu ni jepesi na liko wazi. Katika Qur'an 19:35 tunasoma. Anapolitaka jambo huliambia tu kuwa nalo likawa. Lakini Mwenyezi Mungu alitamka kupitia kinywa cha Nabii Daudi (Zab. 2:7) kuwa Yesu ni mwanae, Je, haiwezi kuwa? Pia kwa kinywa cha Nabii Hosea 11:1. Nilimwita mwanangu kutoka Misri na utabiri huo kutimia katika Mat. 2:15. Twasoma kuwa akakaa (Yesu) huko mpaka Herode alipokufa. Jambo hili lilifanyika ili neno alilosema Bwana kwa njia ya Nabii litimie. Nilimwita mwanangu kutoka Misri". (Hos. 11:1). Kama Mungu hutamka neno liwe na huwa (Qur. 19:35) basi ametamka Yesu ni mwanae. Na moja ya sababu Yesu kuhukumiwa kifo ni kule kukiri kwake kuwa ni mwana wa Mungu baada ya kuwekwa chini ya kiapo na Kuhani Mkuu aseme kweli. Twasoma kuwa "Kuhani Mkuu akamuuliza tena. Je, wewe ndiye Masiha mwana wa Mungu mtukufu?" Yesu akajibu "Naam mimi ndiye... ndipo Kuhani Mkuu akararua joho lake (Marko 14:60-65). Wayahudi walikimbilia kuokota mawe (Yoh. 10:31) na kurarua majoho pindi Yesu anaposema ni mwana wa Mungu, hata hivyo Waislamu wao hupendelea hoja zaidi kuliko kuokota mawe.
Bw. Muhibu alitakiwa ajibu hoja za Yehova na Allah zilizotajwa hapo juu kuliko kukimbilia kumsakama Mtume Paulo kuwa ndiye aliyeanzisha Ukristo. Hakika Ukristo ulianza pale Yesu alipotamka kwamba juu ya mwamba wa Petro atajenga Kanisa lake (Mat. 16:18) nadhani inafahamika Kanisa ni nani, pia Yesu alipoagiza tubatizwe (Mat. 28:19) na kwamba Wakristo wataondolewa kwenye masinagogi (Misikiti) Yoh. 16:1-3 haya siyo maneno ya Paulo.
Bw. Muhibu anapoteza muda mwingi kuhangaika na Paulo kuwa ndiye aliyewafanya Wakristo wamwabudu Yesu kama Mungu. Twasoma kuwa Mwana ataheshimika kama Baba Yoh. 5:23 haya siyo maneno ya Paulo. Paulo hakuanza kumwita Yesu Mungu, Yesu ameitwa hivyo zamani na wakati wa uumbaji yeye ndiye aliyekuwa stadi wa kazi (Mithali 8:30) na Mungu mwenye nguvu (Isa. 9:6), maneno haya siyo ya Paulo.
Badala ya Bw. Muhibu kupoteza muda mwingi kuhangaika na Paulo, atuondolee shaka ni vipi Yehova na Mungu Allah aseme Mayahudi ndio maadui wakubwa (Qur. 5:82) na mambo mengine yanayofanana na hayo yenye kupingana.
Bw. Muhibu atumie tena muda wake kutuelimisha tupate kuamini bila shaka yoyote kuwa Yehova na Allah ni Mungu mmoja badala ya kupoteza muda mwingi kwa Paulo.
--
|
|