MASHAIRI
 

Issa Ponda hana kosa
 

Atafutwa mchochezi, mvurugaji amani,
Asha kwa mfano ndezi, kwa moto vichakani,
Iwe yao moja kazi, kumtia hatiani,
Katika upelelezi, ashakwae hana  kosa.

Ashakwae hana kosa, si mvugura amani,
Hivyo ni vyakwao visa, lengo tumelibaini,
Ukistaajabu Musa, waona ya Firauni,
Katika upelelezi, ashakwae hana  kosa.

Kunajambo talinena, lisikize ka makini,
Mwenye  kosa wasi hana, mvurugaji amani,
Atembea kila kona, na silaha mabegani,
Katika upelelezi, ashakwae hana  kosa.

Amewaua hadhirina, bila chembe ya imani,
Kuumba uwezo hana, katutia misibani,
Mchochezi na fitina, mwamsaka mtu gani,
Katika upelelezi, ashakwae kaonewa.

Mengine usitaraji, mwenye kosa fafanua,
Kama kweli mshakaji, haki ukitumia,
Mwenye kosa muuaji, amani katuvurugia,
Mvurugaji amani, raia wema kauwa.

Muuaji huyo mtu, amezizusha hasama,
Ameua ndugu zetu, mfano kama wanyama,
Kutendeka hiki kitu, hatusahau daima,
Sisi lilobaki kwetu, kura zetu kuwanyima,
Mvurugaji wa amani, silaha alotumia.

Bi. B.A. Mohamed,
S.L.P. 4,
Pangani,
Tanga.


Acha kujidhalilisha

Bismillahir naanza, kwa jina lake Rabuka,
Tena kanipa uweza, kusoma na kuandika,
Nia ni kuwaeleza, wasia wangu hakika,
Acha kujidhalilisha, ewe dada Islamu.

Islamu wa kisasa, kwa kweli wanishangaza,
Waichukua mikasa, nakupita itangaza,
Waicheza kwasa kwasa, njiani bila kuwaza,
Acha kujidhalilisha, ewe dada Islamu.

Amekuwa hayawani, hujuwi kikudhurucho,
Kila onacho njiani, wakitaka uwe nacho,
Yakushinde miwani, yakaapo kwenye jicho,
Acha kujidhalilisha, ewe dada Islamu.

Yarabi katuumbia, sura za kila namna,
Sie twajiharibia, twajiweka kwa namna,
Ngoziye kuikoboa, nazo nyuso kuzichuna,
Acha kujidhalilisha, ewe dada Islamu.

Hivi huna hata haya, kukataa bara lako,
Vipi wale wa Ulaya, wakitaka kuja kwako,
Wakimbilia Ulaya, na nywele kama ukoko,
Acha kujidhalilisha, ewe dada Islamu.

Mashindano uremboni, ndiyo hayo mwayaweza,
Utakuta gazetini, uchi mmejilegeza,
Hata huko mashuleni, nao pia wajikaza,
Acha kujidhalilisha, ewe dada Islamu.
 

Acheni mfananisho, kati yako na kondoo,
Yaja siku ya kitisho, ukate ndugu na koo,
Kikutoke na kijasho, hiyo siku ya kitisho,
Acha kujidhalilisha, ewe dada Islamu.

Nane beti namaliza, kalamu naweka chini,
Namshukuru muweza, kuniweka akilini,
Kanijalia uweza, unifae maishani,
Acha kujifananisha, kati yako na wanyama.

Asha Juma,
Msamala Muslim Seminary Sec. Sch.,
S.L.P. 985,
Songea.



Baraza la Maulidi

Hivi ni kigezo gani, kinachotumika hasa,
Mialiko ya wageni, kwenye hafla za sasa,
Mambo haya ya zamani, au yanaanza sasa,
Kumualika Sumaye, ni kosa kubwa kabisa.

Sumaye kuwa mgeni, tena huja kuwaasa,
Masheikh waumini, wote kupigwa msasa,
Ukafiri hamuoni, mbona mnafanya visa,
Waumini wote ndugu, haya ndio mafundisho?

Hemed mjaa fani, nanyi Masheikh wa sasa,
Hafla hizi za dini, wapi nyinyi mmenasa,
Mtabeba mgongoni, mafurushi ya makosa,
Waumini wote ndugu, haya ndio mafundisho?

Mabakwata tizameni, mnayo mengi makosa,
Serikali si yadini, ukafiri ndio hasa,
Mwawaalika wa nini, mbona nyinyi mwajitosa,
Waumini wote ndugu, haya ndio mafundisho?

Mengi tasema mbeleni, leo nimeyatomasa,
Mnayofanya jamani, njaa ua ututusa,
Tafakarini undani, pepo tusije ikosa,
Kumualika Sumaye, ni kosa kubwa kabisa.

Zuberi Mohamed Mwinyi (Amir),
S.L.P. 61428,
Dar es Salaam.

--
Juu RUDI


Bonyeza hapa
kushriki mjadala au kutoa maoni juu ya habari hizi na masuala mengineyo ya Kiislamu kwenye Baraza ya Wasomaji

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtz.org
 
An-nuur Home | Ukurasa wa Mwanzo | Islam Tanzania 
Links | Matoleo Yaliyopita | Sign our Guestbook