Ya Temeke na Ubungo
Wako wapi wakufunzi, wenye
elimu na bongo,
Watanzuwe hizi tanzi, zenye
kurudisha lengo,
Awe mmoja muhunzi, arande
kwenye ulingo,
Ya Temeke na Ubungo, lengo
twarudishwa wapi?
Tunarudishwa kwa juzi, kwenye
kimoja kitengo,
Liwe moja hili shanzi, agawe
yeye unyango,
Kama mpo watetezi, mwajuwa
hii mipango?
Ya Temeke na Ubungo, lengo
twarudishwa wapi?
Haja kidumu kimoja, ndani
ya mingi milango,
Ajisifiye usoja, ndiye bingwa
kwenye tungo,
Awe peke yake meja, wengine
wote waongo,
Ya Temeke na Ubungo, lengo
twarudishwa wapi?
Kwa hizi ndogo chaguzi, baba
kajazwa usongo,
Ananyang’anya kwa wazi,
wanyonge twakata shingo,
Keshaanza udakuzi, kuwatia
watu chongo,
Ya Temeke na Ubungo, lengo
twarudishwa wapi?
Ifikapo zamu yake, kunyang’anywa
lile tango,
Agaridhia atoke, kiti akae
Tinyango,
Hatosukuma mateke, makombora
na vigongo,
Ya Temeke na Ubungo, lengo
twarudishwa wapi?
Wajuzi wenye elimu, kina
Soselo na Shango,
Fanyeni kila jukumu, liondoke
hili zongo,
Ugonjwa huu kudumu, tunageuzwa
kaango,
Ya Temeke na Ubungo, lengo
twarudishwa wapi?
S.C. Gonga,
S.L.P. 15068,
Dar es Salaam.
Kuweka kali halali? (Sapoti)
Bismillahir naanza, kwa jina
lake jalia,
Nataka kuwaeleza, yale yalotangulia,
Mwenzetu katueleza, Mungu
alomjalia,
Kuweka kali haramu, kwa
amri yake Mola.
Amri ni yake Mola, Jabiri
nakuambia,
Mola kaiharamisha, na Mtumewe
pia,
Laana wameahidiwa, wale
walokaidia,
Kuweka kali haramu, kwa
amri yake Mola.
Wanashangaza hakika, wale
wanaojisifia,
Eti wao wanataka, mume kumfurahishia,
Huku linaharibika, umbo
lao asilia,
Kuweka kali haramu, kwa
amri yake Mola.
Laana ikikupata, nani takusalimisha,
Faida utayopata, hakuna
wakumshirikisha,
Madonda utayapata, nani
atakuponesha,
Kuweka kali haramu, kwa
amri yake Mola.
Mola katutunukia, umbo linalopendeza,
Na nywele akatujalia, ili
kichwa kukijaza,
Wala hakutuambia, kali kuitumbukiza,
Kuweka kali haramu, kwa
amri yake Mola.
Hijab inawatoka, kali wanapojitia,
Kote kote watataka, kali
kujionyeshea,
Madhara yatawafikia, si
yakujijutia,
Kuweka kali haramu, kwa
amri yake Mola.
Mungu ametuambia, yale aliyokataza,
Naye akatuambia, sheria
zenye kuongoza,
Nakuweka pia, Mungu ametukataza,
Kuweka kali haramu, kwa
amri yake Mola.
Tamati natamatia, ujumbe
huu siku,
Jabiri kumsaidia, yale alohubiria,
Dini kuizingatia, kwa mujibu
wa sheria,
Kuweka kali haramu, kwa
amri yake Mola.
Fatma Saleh,
Kibasila Sec. School,
P.O. Box 20378,
Dar es Salaam.
Wake kudai talaka (swali
la msisitizo)
Habari zinasikika, kupitia
gazetini,
Wake kudai talaka, madai
mahakamani,
Hivi kweli tutafika, hasa
sisi waumini,
Wake kudai talaka, sheria
au ubabe?
Mahakama kitwaghuti, kuamuwa
waumini,
Hamuoni tafauti, tunajitowa
Manani,
Wakati hautupiti, sasa tujikwamueni,
Wake kudai talaka, sheria
au ubabe?
Ndoa zetu madhubuti, sheria
za vitabuni,
Amri hiyo thabiti, tangu
enzi za zamani,
Na ndani ya Taurati, imenenwa
usizini,
Wake kudai talaka, sheria
au ubabe?
Wake kwenda kwa pilati, talaka
kuzibaini,
Huwa kwetu misibati, kama
sisi tuna dini,
Sawa wale Wagalatia, hawana
matumaini,
Wake kudai talaka, sheria
au ubabe?
Nimefanya utafiti, sababu
zake ni duni,
Kama sale hawapati, wanaanzisha
uhuni,
Na ngoma ya benibati, ruhusa
mukiwahini,
Wake kudai talaka, sheria
au ubabe?
Temeke na katikati, kwingine
kote nchini,
Kila mwenye hisabati, ndoa
kitu cha thamani,
Tuacheni usharati, mabalaa
hamuoni,
Wake kudai talaka, sheria
au ubabe?
Sisi wanaharakati, sasa tukae
makini,
Dini iwe katikati, kwa sheria
hukumuni,
Tusipitwe na wakati, itakuwa
mtihani,
Wake kudai talaka, sheria
au ubabe?
Hapa mimi ni tamati, enyi
wake waumini,
Mkae mjizatiti, ndoa zenu
heshimuni,
Na muzifatie shuruti, waume
zetu tiini,
Wake kudai talaka, sheria
au ubabe?
Zuberi Mohammed Mwinyi
(Amir),
S.L.P. 61428,
Dar es Salaam.
|
|