Hali ya Uislamu Sambaani


NIMEPATA kuhudhuria maadhimisho ya kumbukumbu ya kuzaliwa kwa Mtume (s.a.w.) sehemu tofauti na nyakati tofauti miaka ya nyuma sehemu hizi ambapo nilishuhudia maelfu kwa maelfu ya Waislamu wakisikiliza nasaha mbalimbali, kumsalia na kumsifu Mtume (s.a.w.).

Mikusanyiko ya namna hii ni kigezo cha kuweza kujua wingi wa Waislamu katika eneo husika kwa kuwa kila mtu hujihimu kuhudhuria. Dosari moja kubwa niliyopata kuiona ni pale nyakati za swala zinapoingia, kwani ni kikundi kidogo tu kinachojishughulisha na ibada ya swala. Tatizo la Waislamu wengi kutoswali lipo karibu kila mahali lakini limezidi kupita kiasi huko, mbaya zaidi ni pale unapoona hata walimu wa madrasa au wanafunzi wao wa siku nyingi wanavyokuwa wazito kuswali.

Jinsi watu wanavyohamasishana kutoa michango kwa ajili ya maulidi na heka heka zinavyokuwa siku ya sherehe na maadhimisho yenyewe, basi mtu mwenye elimu ndogo kuhusu Uislamu huweza kuamini moja kwa moja kwamba huenda hii ndiyo ibada kubwa kuliko zote.

Suala la kuswali hususan swala tano huonekana ni gumu lenye kuhitaji nguvu za ziada kulifanya, ni jambo la kawaida kuona watu wamekaa vibarazani wakiteta hili na lile au kucheza bao huku muda wa vipindi vya swala ukiwapita.

Ijapokuwa unaweza kuamini kwa haraka haraka kutokana na mandhari inavyoonekana kutokana na Msikiti kuonekana kila baada ya kitambo kidogo, utakuta karibu kila kijiji kuna Msikiti na darsa lakini kama havitumiki kuwajenga kiimani na kimaadili watu wanaoishi jirani navyo inakuwa haipendezi na itakuwa ni kinyume cha mafundisho ya Mtume (s.w.) juu ya taasisi hizi mbili. Idadi ya wanaohudhuria humo ni ndogo kupita kiasi kama nilivyopata fursa ya kutembelea Lushoto mjini wakati wa mshuko wa swala ya Ijumaa katika Msikiti wa Chake Chake.

Nilipatwa na simanzi baada ya kuona vile waumini walivyokuwa wachache pamoja na kwamba Misikiti miwili wa Polisi na ule wa Bakwata ilifungwa ili kuipa nguvu ile ya Chake Chake na Dochi ambapo ipo kama maili mbili hivi kutoka mmoja hadi mwingine. Watu wingi wanaendelea kuonekana wakiendelea na uchuuzi wa vitu mbalimbali katika gulio la mjini na majiani kana kwamba hawajui nini dini yao inawataka wafanye au siyo Waislamu kabisa.

Nimegundua kuwa vipo vijisababu vinavyowapelekea wengi wetu kwenda kinyume na mafundisho safi ya dini yetu, mojawapo ni kutotaka kujifunza Uislamu, na wale waliojifunza juzuu mbili ama tatu hivi inashindikana kuwasaidia kutokana na njia ngumu sana walizotumia kujifundishia. Nimepita pita hata kukaa madrasa nimekaa muda mwingi tu, nilichokiona ni jinsi vijana walivyojitahidi kuhifadhi Qur'an na kukariri hadithi za Mtume (s.a.w.).

Tatizo ni kwamba tafsiri ya vile walivyovihifadhi hawafundishwi sawa sawa hivyo kuwapelekea kushindwa kuvifanyia kazi kinachowapelekea kuishi kama mtu ambaye hajajifunza kitu. Kijana wa namna hii itamwia kwake vigumu kuishi Kiislamu ambapo huweza kudakwa kirahisi na tamaduni za kileo, mila, desturi na taratibu nyingine za kitwaghuti.

Baadhi ya Waislamu wameonekana kuritadi huku wanawake wakiongoza, kwani hushawishika kirahisi hadi kuchumbiwa na wasiofuata maadili ya dini au kuwekwa vimada na makafiri wa kiume na wale waliokosa yote hujikuta wakijipatia watoto nje ya ndoa.

Athari nyingine ni watu kuingia kwenye shirki aidha bila kujua au wengine kushiriki kutokana na mazingira yalivyochafuka na imani za kichawi au kutofahamu vema chanzo cha matatizo na magonjwa fulani fulani. Mila na desturi za kikabila na kienyeji zimepewa nafasi kubwa sana mpaka kupelekea kuchanganywa na dini katika baadhi ya sehemu, hivyo kuonekana kama ni dini mpya hivi.

Kwa wasomaji wa ANNUUR matoleo ya siku zilizopita iliwahi kuchapishwa barua kutoka Mkumbara wilayani Korogwe kuelezea miiko waliyopewa wakulima wakazi wa kijijini hapo wakitakiwa wasiende mashambani mwao kutokana na dawa iliyofanywa na mganga mmoja wa kienyeji ili kuondoa baa la wadudu waharibifu waliolikumba eneo lao.

Ukiacha hilo zipo desturi nyingine nyingi kama tambiko tofauti ambazo wakati mwingine wanaojiita walimu na Maustadh huombwa kuleta dua na baadaye kujumuika na wengine waliohudhuria kumtafuna kondoo au mbuzi wa kafara. Mbali na tambiko za namna namna zipo zingine za maombi ya mvua au "mgwia shama" kama inavyofahamika na wakazi wengi. Maziko na ndoa huambatana na taratibu zingine za kimila kama vile unywaji wa pombe, hali kadhalika waganga hualikwa mazikoni au wakati wa kuosha maiti na ndugu wa marehemu ikihisiwa kuwa kifo cha marehemu kimeletwa na mkono wa mtu kama kurogwa hivi au shakiizi kwa wale wanaojua au maapizi kwa kinamama maarufu kama vyungu. Kuna wakati hata maiti hufukuliwa na kuzikwa upya kwa maelekezo ya waganga, haya yote hufanyika sambamba na viongozi wa kidini wasomi wazuri tu lakini mabubu kwa kuwa hawawezi kuyakemea.

Aidha, walio wengi huamini kuwa kupiga ramli na kutazamia ni shughuli ya kiutaalamu kama vile daktari anavyomfanyia uchunguzi mgonjwa. Hii ni kwa sababu wanaotazamia na kupiga ramli wamejinasibisha na Uislamu wakijipamba kwa vyeo vya Sheikh, Ustaadh na maalim hivyo kuendelea kuswalisha, kudarasisha na kulingania, baadaye majumbani mwao hushughulikia watu kwa matatizo mbalimbali ya kurogwa kama wanavyoelekezana, wakiambizana ana zongo, kisimo na kadhalika au marehemu fulani hakufa bali amechukuliwa msukule. Hali kama hizi zimekuwa ni kikwazo kikubwa kwa kuwa tunaotegemea wawe mfano bora ndio wanakuwa wapotoshaji wakubwa hivyo waumini wa kawaida kufikia kuwa wazito kukubali wanapokumbushwa waepuke haya kwa kuwa yanakwenda kinyume na taratibu za Allah (s.w.).
 
--
Juu RUDI


Bonyeza hapa
kushriki mjadala au kutoa maoni juu ya habari hizi na masuala mengineyo ya Kiislamu kwenye Baraza ya Wasomaji

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtz.org
 
An-nuur Home | Ukurasa wa Mwanzo | Islam Tanzania 
Links | Matoleo Yaliyopita | Sign our Guestbook