Dini anayoihitaji mwanaadamu


KUTOKANA na umbile lake, mwanaadamu daima hutamini kuishi maisha ya furaha na amani yenye maana na yenye kufikia lengo. Kwa hiyo, kinadharia mwanaadamu angelipenda kufuata dini (njia ya maisha) itakayo muhakikishia kufikia lengo la kuumbwa kwake kwa furaha na amani. Swali muhimu kwa mwanaadamu ni kubaini ni ipi katika dini nne - Uislamu, Ukafiri, Ushrikina na Utawa - atakayoichagua na kuifuata ili aweze kuishi hapa duniani kwa furaha na amani.

Sifa za Dini sahihi anayoihitaji mwanaadamu

Dini sahihi itakayomuwezesha mwanaadamu kuishi kwa furaha na amani katika maisha ya hapa duniani na akhera hainabudi kuwa na sifa zifuatazo:

(a) Dini sahihi ni lazima ieleze ukweli juu ya maumbile

Dini sahihi ni lazima itoe taarifa za ukweli juu ya mwanaadamu na maumbile yote yaliyomzunguka. Imfahamishe mwanaadamu juu ya Muumba wake na vyote vilivyomzunguuka, imfahamishe lengo lake la maisha na lengo la kuwepo viumbe vyote vilivyomzunguuka vilivyo hai na visivyo hai. Pia imfahamishe ni ipi nafasi yake au hadhi yake hapa ulimwenguni na ni vipi ataweza kufikia lengo lake la maisha na kubakia katika hadhi yake. Pia imfahamishe kwa usahihi ni pi hatima yake baada ya maisha ya hapa duniani.

(b) Kanuni na Sharia zinazofuatwa na dini sahihi ni lazima ziende sambamba na kanuni na sheria zinazofuatwa na maumbile yote

Dini sahihi ni lazima imuundie mwanaadamu mwenendo wa maisha unaolingana na mwenendo unaofuatwa na maumbile yote ikiwa ni pamoja na mwili wake ili kuenda sambamba na maumbile na kuepukana na migongano ya aina yoyote.

(c) Dini sahihi ni lazima iwe na uwezo wa kutosheleza mahitaji yote ya mwanaadamu ya kimwili na kiroho (hisiya)

Dini sahihi pamoja na kumuelekeza mwanaadamu namna bora ya kuunawirisha mwili wake na kumuweka katika Siha nzuri, haina budi pia kumuelekeza kutosheleza hisia zake. Kwa kawaida mwanaadamu katika maisha yake anakuwa katika hali na hisia tofauti tofauti wakati mwingine mwanaadamu huwa katika furaha kubwa, kupata ushindi mkubwa katika jambo fulani, huwa katika madaraka makubwa, huwa tajiri, n.k. Dini sahihi ni lazima imuelekeze mwanaadamu namna ya kuishi kulingana na lengo atakapokuwa katika hali kama hizi kwa manufaa ya mwanaadamu wote.

Pia ni kawaida kuwa wakati mwingine mwanaadamu huwa katika hali ya huzuni, kusononeka, uchungu, majonzi, matatizo, wasi wasi, n.k. Dini sahihi ni lazima imuelekeze mwanaadamu kwa usahihi namna atakavyokabiliana na hali kama hizo na kubakia katika lengo lake.

(d) Dini sahihi hainabudi kuwa njia ya maisha iliyokamilika

Dini sahihi ni lazima imuwekee mwanaadamu utaratibu maisha utakao muwezesha kuindea kwa ufanisi kila kipengele cha maisha yake ya kibinafsi na kijamii katika nyanja zote za kiafya, kiuchumi, kisiasa, kiutamaduni, kisheria na kieleimu n.k.

(e) Dini sahihi hainabudi kuwa na taasisi (Ibada) maalum za kumbakisha mwanaadamu katika lengo lake na hadhi yake

Mwanaadamu anatokana na muungano wa mwili na roho. Mwili una sifa za kinyama na roho ina sifa za kiutu. Roho ikitawala mwili mwanaadamu huwa na mwenendo wa kiutu unaozaa mapenzi, huruma, ustawi, furaha na amani katika jamii. Matashi ya kimwili yakiutawala utu, mwanaadamu huwa na mwenendo wa kinyama, na hasa mbaya zaidi kuliko ule wa wanayama unaozaa chuki, udhalimu, majivuno, kiburi, vurugu na kuharibika kwa jamii. Kawaida mwanaadamu huchukia kufanyiwa matendo ya kinyama na hupenda kufanyiwa matendo ya kiutu. Kwa hiyo, dini sahihi inayostahiki kuwa chaguo la mwanaadamu ni lazima iweke utaratibu wa uhakika wa kuinua utu wa mwanaadamu na kumbakisha katika lengo lake na hadhi yake hapa duniani.

(f) Dini sahihi hainabudi kuwa dini ya walimwengu wote wa nyakati zote

Binaadamu asili yao ni moja, lengo la maisha yao ni moja na wote wanahitaji kuishi kwa furaha na amani. hivyo dini sahihi hainabudi kuwa dini inayowahusu wanaadamu wote wa uliwmengu mzima kuanzia wa mwanzo mpaka wa mwisho. Dini hiyo hainabudi kutokuwa na mipaka ya mahali (jiografia) au wakati. Pia dini sahihi haitakuwa kwa jina la mtu, au la mahali au la kihistoria.

(g) Dini sahihi hainabudi kumhakikishia mwanaadamu kupata haki zake zote

Dini sahihi inayowastahiki walimwengu wote wa nyakati zote hainabudi kuhakikisha kuwa kila mmoja anapata haki zake sawa za kibinafsi na kijamii bila ya upendeleo au ubaguzi wa aina yoyote. Dini, kabila, taifa, rangi au hadhi havitazingatiwa na dini sahihi katika kumpatia kila mtu haki yake anayostahiki. Dini sahihi haina budi kuwa na utaratibu wa kusimamia na kuchunga haki ya kila mtu na kuwahukumu na kuwaadhibi wakosa kwa usawa ili kuiweka jamii kwenye furaha na amani ya kweli katika maisha. Dini sahihi hainabudu kuwa na sharia ambazo zinamgusa kila mtu kwa usawa.

Kwa nini mwanaadamu hawezi kuunda Dini sahihi

Ukizingatia kwa kina sifa za dini sahihi inayostahiki kuwa chaguo la mwanaadamu, utaona kuwa dini hiyo haiwezi kuwa mojawapo katika ya zile dini alizoziunda mwanaadamu ukafiri au Ushirikina au utawa. Swali la msingi linalotukabili ni "Kwa nini mwanadamu hawezi kuunda dini yenye sifa hizo?" Swali hili limeshajibiwa katika kurasa za nyuma pale utlipojibu swali, "Kwanini mwanaadamu anahitajia mwongozo kutoka kwa Mwenyezi Mungu Mungu (s.w.) kwa muhtasari hawezi mwanaadamu kuunda dini sahihi kwa sababu zifuatazo:

(a) Mwanaadamu anaathiriwa na matashi yake

Mwanaadamu pamoja na kutunukiwa vipawa vya akili na utambuzi wa hali ya juu, bado fikra zake na uamuzi wake unaathiriwa sana na matashi ya nafsi yake. Akipenda kitu hupitisha uamuzi wa upendeleo pasina haki. Na akichukia kitu hupitisha uamuzi wa uonevu. Hivyo kutokana na udhaifu huu ukichukua jukumu la kuunda dini ataweka utaratibu utakaomopendelea yeye na wale walio karibu naye na kuwakandamiza wale wasio na uhusiano wa karibu naye.

(b) Nyenzo anazozitumia Mwanaadamu katika kujipatia elimu ni dhaifu

Kipawa kingine alichotunukiwa mwanaadamu kinachomuwezesha kuwa mtawala wa ulimwengu na vilivyomo ni elimu. Lakini elimu aliyonayo ni finyu sana kiasi kwamba haimuwezeshi kuunda njia ya maisha itakayokuwa na sifa zilizotajwa. Elimu aliyonayo ni finyu kwa sababu ya ufinyu wa nyenzo anazozitumia katika kujipatia elimu. Nyenzo anazozitumia ni akili na milango ya fahamu, uchunguzi na majaribio ya kisayansi na uzoefu unatokana na historia. Kutokana na ufinyu na udhaifu wa nyenzo anazozitumia katika kujielimisha, mwanaadamu hawezi kufahamu mambo ya msingi wa maisha yake mpaka afahamishwe na Muumba wake. Kama nyenzo hizi anazozitumia katika kujielimisha hazijaweza kumfahamisha uhakika wa roho yake, atawezaje kuunda njia sahihi ya maisha. Qur'a inatutanabahisha juu ya ufinyu wa elimu tuliyonayo kama ifuatavyo:

"Na wanakuuliza habari ya roho; Sema, Roho ni jambo lililohusika na Mola wangu. Nanyi hamkupewa katika elimu ila kidogo kabisa." (17:85).

Kutokana na sababu hizi za msingi, mwanaadamu kamwe hana uwezo wa kuunda Dini sahihi. Njia yoyote ya maisha itakayoundwa na mwanaadamu itakuwa ni yenye kumpotosha mwanaadamu na kumuangamiza kwani itakuwa imejengwa katika msingi ya dhana na uzushi tu kama Allah (s.w.) anavyotutanabahisha:

"Na ukiwatii wengi katika (hawa waliomo ulimwenguni watakupoteza na njia ya Mwenyezi Mungu. Hawafuati ila dhana tu, na hawakuwa ila wenye kuzua (tu basi)". (6:116).

Mwenye kustahiki kumuundia mwanaadamu njia sahihi ya maisha yake ni Muumba wake, Mwenye ujuzi na Hekima, aliyemuumba yeye na vyote vilivyomzunguuka kwa lengo maalum.

Kwanini Uislamu ni Dini Sahihi?

Uislamu ndio dini sahihi inayostahiki kuwa chaguo la kila mtu mwenye akili timamu kwa sababu zifuatazo:

Kwanza: Uislamu ni dini ya Mweyezi Mungu (s.w.) aliyemuumba Mwanaadamu kwa lengo maalum. Ni Muumba pekee anayejua mahitaji halisi ya Mwanaadamu na ni yeye pekee anayejua njia sahihi ya kumfikisha mwanaadamu kwenye lengo lake la maisha. Mwenyezi Mungu anasisitiza:

"Ni juu yetu (kubainisha) njia (sahihi)" (92:12)

Hakika dini mbele ya Mwenyezi Mungu ni Uislamu (3:19).

Pili: Uislamu ndio dini pekee inayotosheleza kwa ukamilifu vipengele vyote vya sifa za dini sahihi kama ifuatavyo:

(a) Uislamu unaeleza ukweli juu ya Maumbile na nafasi ya mwanaadamu hapa Ulimwenguni

Uislamu unatufahamisha kuwa ulimwengu huu pamoja na vyote vilivyomo umeumbwa na Mwenyezi Mungu (s.w.), kwa lengo maalum. Katika Qur'an tunafahamishwa kuwa lengo la kuumbwa mwanaadamu ni kumuabudu Mwenyezi Mungu. Rejea Qur'an (51:56). Pia tunafahamishwa kuwa lengo la kuumbwa viumbe vyote vya mbinguni na ardhini ni kwa ajili ya kumtumikia mwanaadamu. (Rejea Qur'an, (2:29).

Aidha tunafahamishwa katika Qur'an kuwa mwanaadamu hapa ulimwenguni ana Hadhiya ukhalifa wa Mwenyezi Mungu. Kuwa khalifa wa Mwenyezi Mungu ni kusimamisha ufalme wa Mwenyezi Mungu kwa kufuata mwongozo wake na kutarajia Radhi zake. Pia Uislamu unatufahamisha kuwa mwanaadamu atakuwa na maisha ya akhera ambapo atalipwa kutokana na matendo yake hapa duniani. Wale walioufuata dini ya Mwenyezi Mungu (s.w.) na kuishi kulingana na lengo la kuumbwa kwao watakuwa na maisha ya furaha na amani huko peponi. Na wale waliofuata dini walizounda wanaadamu wakashindwa kufikia lengo la maisha yao, watapewa adhabu kali huko motoni.

(b) Kanuni na Sharia za Uislamu zinakwenda sambamba na kanuni na Sharia za maumbile yote

Kufuata Uislamu ni kutii kwa unyenyekevu sharia na taratibu alizoziweka Mwenyezi Mungu katika kuendesha maisha ya kila siku ya kibinafsi na kijamii. Pia kutokana na Sayansi tunafahamu kuwa ili maumbile yote yabakie katika hali yake ya kawaida, ikiwa ni pamoja na miili yetu, wanyama, mimea na viumbe vingine vilivyo hai na visivyo hai vimedhibitiwa na kanuni na sharia za maumbile za kibailogia, kifizikia na kikemia. Aliyeziweka sharia hizi ni Mwenyezi Mungu Muumba. Hivyo mwanaadamu atakapokuwa mtii wa kanuni na sharia za Mwenyezi Mungu atakuwa ameamua kwenda sambamba na maumbile yote.

Tunafahamishwa katika Qur'an kuwa viumbe vyote, isipokuwa binaadamu vinafuata Uislamu bila ya hiari:

"Je, wanataka dini isiyokuwa ya Mwenyezi Mungu (dini ya Kiislamu) na hali kila kilichomo mbinguni na ardhini kinamtii yeye kipende kisipende? Na kwake watareshwa wote". (3:83).

Katika aya nyingine Mwenyezi Mungu (s.w.) anatufahamisha kwamba Uislamu ndio njia ya maisha pekee inayokwenda sambamba na umbile la binaadamu, umbile la mbingu na ardhi na viumbe vyote vilivyomo:

"Basi uelekeze uso wako katika dini iliyo sawasawa. Ndilo umbile Mwenyezi Mungu alilowaumbia watu. Hakuna mabadiliko katika maumbile ya viumbe vya Mwenyezi Mungu. Hiyo ndio dini iliyo ya haki, lakini watu wengi hawajui." (30:30).

(c) Uislamu ni Dini inayotosheleza mahitaji yote ya binaadamu ya kimwili na kihisia

Uislamu unamuhimiza mwanaadamu kukinawirisha kiwiliwili chake na kukiweka katika siha nzuri kwa kula na kunywa vilivyo vizuri, kufanya mazoezi ya viungo, kujikinga na maradhi na kujitibu, kujinadhifisha nguo na mwili.

Sambamba na kuurutubisha mwili, Uislamu unamuelekeza mtu ni vipi afanye anapokuwa katika hali na hisia tafati tafauti, ambazo bila mwongozo zinaweza kumhilikisha. Kwa upande mmoja Uislamu unamuelekeza mwanaadamu anapokuwa katika hali ya furaha kama kuwa katika utajiri mkubwa, katika madaraka makubwa n.k., asitakabari bali amshukuru aliyemtunukia neema hizo kwa kuzitumia kwa faida ya watu wote katika jamii.

Kwa upande mwingine Uislamu unamuelekeza mwanaadamu anapokuwa katika hali ya majonzi, huzuni, matatizo, na katika hali nyingine kama hizo, afanye Subira na kumtegemea Mwenyezi Mungu kama tunavyokumbushwa katika aya zifuatazo:

"Na tutakuitieni katika msukosuko wa hofu na njaa na upungufu wa mali na watu na matunda. Na wapahse habari njema wanaosubiri. Ambao uwafikapo msiba husema, Hakika sisi ni wa Mwenyezi Mungu na kwake yeye tutarejea:

Hao juu yao zitakuwa baraka zitokazo kwa Mola wao na rehema, na ndio wenye kuongoka." (2:155-157).

(d) Uislamu ni njia kamili ya maisha

Uislamu ni dini pekee inayojibuysisha na fani zote za maisha. Uislamu haugawi maisha ya dini na dunia bali umemuelekeza mwanaadamu namna bora ya kukiendea kila kipengele cha maisha yake ya kibinafsi, kifamilia, kiuchumi kisiasa, na maisha yote ya kijamii na kumuwekea mipaka itakayombakisha katika lengo lake la maisha. Kwa maana nyingine Uislamu hauhitaji kuazima lolote kutoka kwenye dini nyingine linalohusiana na uendeshaji wa maisha ya kila siku katika kila fani.

(e) Uislamu umeweka Ibada maalum kwa lengo la kumjenga Mwanaadamu kimaadili

Pamoja na Mwenyezi Mungu (s.w.) kumpa mwanaadamu mwongozo unaomuwezesha kukiendea kila kipengele chake cha maisha kwa usahihi kulingana na lengo, amemuamrisha kutekeleza Ibada maalum kwa lengo la kumjenga kimaadili na kumbakisha katika hadhi yake ya ukhalifa. Ibada hizi ni nguozo tano za Uislamu - kutoa Shahada mbili, kusimamisha Swala, kutoa Zakat, Kufunga Ramadhani na Kuhiji Makka kwa wenye uwezo.

Kutoiaja na umuhimu wake, ibada hizi za faradhi zimeambatanishwa na ibada za sunnah ili kuzikamilisha ibada za faradhi pale zilipoteleza kwa upungufu. Mwanaadamu kamwe hawezi kuwa na maadili yanayostahiki bila ya kuteleza hizi kwa ukamilifu wake.

(f) Uislamu ni Dini ya Walimwengu wote wa nyakati zote

Uislamu ni dini ya kijitiisha na kujinyenyekesha kwa Mwenyezi Mungu (s.w.) kila mwenye kuamini Mwenyezi Mungu na kujitiisha kwake kwa kufuata barabara mwongozo wake katika kukiendea kila kipengele cha maisha huwa ni Muislamu bila ya kujali ukoo wake, taifa lake, hadhi yake au wakati wa historia. Uislamu ni dini iliyofundishwa na Mitume wote kuanzia kwa Adam (a.s.) kama tunavyojifunza katika aya zifuatazo:

"Amekupeni sharia ya Dini ile ile aliyomuusia Nuhu na tuliyokufunulia wewe na tuliyowausia Ibrahim na Musa na Isa, kwamba simamisheni dini wala msifarikiane kwayo, ni ngumu kwa wenye kushirikisha (dini hii) unayowaitia. Mwenyezi Mungu humchagua kwake amtakaye na humuongoza kwake aelekeaye." (42:13).

"Na ipiganieni Diniya Mwenyezi Mungu kama inavyostahiki (kuopiganiwa). Yeye amekuchagueni (muwe umma ulio bora). Wala hakuweka juu yenu mambo mazito katika dini. (Nayo dini hii) ni Mila ya baba yenu Ibrahim. Yeye (Mwenyezi Mungu) alikuiteni Waislamu tangu huko mwanzo katika vitabu vya zamani) na katika (Qur'an) hii pia (mumeitwa kwa jina hilo) ili awe Mtume shahidi juu yenu na nyinyi muwe shahidi juu ya watu (waliotangulia). Basi simamisheni swala na toeni zaka na shikamaneni pamoja kwa ajili ya Mwenyezi Mungu. yeye ndiye Mola wenu. Mola mwema alioje na msaidizi mwema alioje."

(g) Uislamu ni Dini ya kusimamisha Haki na Usawa

Miongoni mwa mambo makubwa yanayovuruga amani ulimwenguni ni kuwepo kwa dhulma katika jamii. Na dhulma haiondoki mpaka Haki isimamishwe. Dini zote zilizoundwa na wanadamu ziko pale kustawisha dhulma katika jamii - matajiri na wenye hadhi huwakandamiza raia maskini na wanyonge. Uislamu ndio dini pekee inayoweza kumkomboa mwanaadamu kutokana na dhulma za aina zote. Usimamishaji wa haki umekuwa miongoni mwa masharti makubwa manne ya kusimama Uislamu kama tunavyojifunza katika Suratul-Asr:

"Naapa kwa zama ("Asr), kuwa binaadamu yuko katika hasara. Isipokuwa wale walioamini na wakafanya vitendo vizuri na wakausiana (kusimamisha) haki na wakausiana (kushikamana) na subira". (103:1-3).

Aya hizi kwa ufupi zinatufahamisha kuwa Uislamu utasimama kwa mtu binafsi na kwa jamii kwa ujumla iwapo mambo manne yatatekelezwa yote kwa pamoja na kwa ukamilifu; Mambo hayo ni:

i) Kuamini inavyostahiki

ii) Kufanya vitendo vizuri

iii) Kuusiana kusimamisha Haki

iv) Kuusiana kusimamisha subira.

"Yeye (Mwenyezi Mungu) ndiye aliyemleta Mtume wake kwa uongofu na Dini ya Haki ili aijaalie kushinda dini zote ijapokuwa watachukia washirikina." (9:33 na 61:9).

Tunajifunza kutokana na aya hii kuwa Uislamu ni dini ya Haki kwa maana ya kuwa ni dini yya Mwenyezi Mungu mwenye haki pekee ya kumuundia mwanaadamu dini. Pia tunajifunza kuwa Uislamu ndio dini pekee inayoweza kusimamisha haki katika jamii. Katika aya nyingine Mwenyezi Mungu anafahamisha kama ifuatavyo:

Na kwa (ajili ya kuleta) hakiki (ulimwenguni ndio) tumeteremsha (Qur'an), na kwa haki imeteremka. Na hatukukuleta ila uwe mtoaji wa khabari njema na muonyaji (17:105).
 
--
Juu RUDI


Bonyeza hapa
kushriki mjadala au kutoa maoni juu ya habari hizi na masuala mengineyo ya Kiislamu kwenye Baraza ya Wasomaji

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtz.org
 
An-nuur Home | Ukurasa wa Mwanzo | Islam Tanzania 
Links | Matoleo Yaliyopita | Sign our Guestbook