Mashairi


Enyi waramba viatu!

Enyi waramba viatu, vibaraka ulamaa,
Nyoyo zimejaa kutu, uchu na nyingi tamaa,
Unyama kusema utu, kulinda yasiyofaa,
Tenda hizo zenu tenda, tenda tumezing'amua.

Tenda zenu tenda, tenda tumezing'amua,
Mchukie mkipenda, mnune na kujiua,
Hata kama mkikonda, pande tunawaengua,
Sasa tushagutuka, enyi waramba viatu.

Enyi waramba viatu, vibandiko mlovaa,
Mjifanyao wenzetu, kusali nasi jamaa,
Kumbe muadi zetu, wabaya mwatuhadaa,
Tenda hizo zenu tenda, tenda tumezing'amua.

Tenda hizo zenu tenda, tenda tumezing'amua,
Vibaraza kuviunda, kuzuga kutuzuzua,
Mmebaki njia panda, hatuji tumegundua,
Sasa tumshagutuka, enyi waramba viatu.

Enyi waramba viatu, vikao mnaoandaa,
Hizo mbinu sasa butu, ukweli zimechakaa,
Bure hampati kitu, hadhara twazikataa,
Tenda hizo zetu tenda, tenda tumezing'amua.

Tenda hizo zenu tenda, tenda tumezing'amua,
Ni punde mlituponda, na sumu kutumwagia,
Havijapona vidonda, mwarudi na kutujia,
Sasa tumeshagutuka, enyi waramba viatu.

Enyi waramba viatu, tena hatutopumbaa,
Umoja na mbwa mwitu, hatuji tunaambaa,
Ujinga hatuthubutu, kuzugwa kama vichaa,
Tenda hizo zenu tenda, tenda tumezing'amua.
 

Idd Kikong'ona,
Morogoro.


Sheikh Mbukuzi

Ya Illahi Ya Satari, Ya Illahi Ya Azizi,
Ya Illahi Ya Qahari, tunakuomba Mwenyezi,
Mpe maisha mazuri, ya furaha na mbawazi,
Shekhe wetu Mbukuzi, Amiri wa Maimamu.

Amiri wa Maimamu, Shekhe wetu Mbukuzi,
Ya Illahi Ya Karimu, mwenye nguvu na ujuzi,
Muondolee magumu, vikwazo na pingamizi,
Shekhe wetu Mbukuzi, Amiri wa Maimamu.

Mbukuzi ni Amiri, abishae mpuuzi,
Hakutwaa kiburi, amepewa hii kazi,
Kwa madhumuni mazuri, kwenye Shura Kiongozi,
Shekhe wetu, Mbukuzi, Amiri wa Maimamu.

Uislamu ni kweli, Kitabu chasema wazi,
Afatae neno hili, huonwa mtu bazazi,
Kweli anaebadili, kwa urongo ndo mjuzi,
Sema kweli Mbukuzi, Amiri wa Maimamu.

Mwisho wa langu shairi, ama yote simalizi,
Tunakuombea kheri, akili na utambuzi,
Katika dhidi subiri, kesho ukapande ngazi,
Shekhe wetu Mbukuzi, Amiri wa Maimamu.

(Mshairi Bora)
Amiri A.S. Andanenga (Sauti ya Kiza),
S.L.P. 4775, Kinondoni Shamba,
Dar es Salaam.



Tulihami pango letu

Siafu wakaitana, kwa pamoja kujadili,
Sababu ya kukutana, kiongozi akakuli,
Mabanati na mabwana, twajifanyaje vivuli?
Magumu tuyakabili, tulihami pango letu.

Tulihami pango letu, magumu kuyakabili,
Ili tugombee chetu, kwa kila hali na mali,
Kwa vipi urithi wetu, kwa kila hali na mali,
Magumu tuyakabili, tugomboe pango letu.

Joka lindani ya pango, Mungu alotufadhili,
Limetatiza mlango, kwa kuzinga mizingili,
Tuukubali mpango, wa kukabili kitali,
Magumu tuyakabili, tugomboe pango letu.

Mkutano kwa umoja, hoja ukaikubali,
Kwa kuungwa ile hoja, joka likaona kweli,
Mara siafu wakija, kifo kitamkutuli,
Likaona afadhali, liende kwenye misitu.

Joka pango kaliacha, kwa kuhofu pilipili,
Siafu usiku kucha, mawazo wakibadili,
Joka limeshajificha, mafichoni huko mbali,
Magumu walikabili, wakatwaa pango lao.

Kama siafu waweza, wabaya kuyabadili,
Kuja yanayopendeza, nao wadudu dhalili,
Vipi! Sisi twajikwaza, watu tulo na akili!
Magumu tuyakabili, tuipate haki yetu.

Hima twende tusilale, msumeno pande mbili,
Nyuma unga unga mbele, gogo hutengwa kuwili,
Ishasemwa na wa kale, "haki" bei yake ghali,
Gharama tuikabili, tuipate haki yetu.

Si haki kudhulumiwa, kudhulumu si halali,
Usiridhi kuibiwa, kuiba usikubali,
Bali chako kutopewa, kakitwae bilikuli,
Tamati katika hili, tuchukuwe "haki" yetu.

(Mshairi Bora)
Amiri A.S. Andanenga (Sauti ya Kiza)
S.L.P. 4775, Kinondoni Shamba,
Dar es Salaam.

--
JuuRUDI



 
 


Bonyeza hapa
kushriki mjadala au kutoa maoni juu ya habari hizi na masuala mengineyo ya Kiislamu kwenye Baraza ya Wasomaji


 



   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtz.org


An-nuur Home | Ukurasa wa Mwanzo | Islam Tanzania
Links | Matoleo Yaliyopita | Sign our Guestbook