Nyerere alituandaa kuipindua Serikali ya Amin - Museven
 

RAIS Yoweri Museven wa Uganda amesema harakati za kuipindua serikali ya Uganda wakati wa Idd Amin ziliendeshwa kutoka Tanzania mnamo miaka ya sabini mwanzoni.

Rais Museven alisema harakati hizo zilianza muda mfupi baada ya Amin kuipindua serikali ya Milton Obote mwaka 1971.

Akizungumza katika mazishi ya hayati Mwalimu Julius Nyerere Jumamosi iliyopita, Rais huyo alisema wao waliandaliwa na Mwalimu Nyerere wakati huo wakiwa vijana wadogo wakisoma Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Rais Museven alikuwa akielezea wasifu wa Mwalimu Nyerere katika siasa za ukombozi barani Afrika.

Alisema Mwalimu hakuwa mstari wa mbele katika kupinga ukoloni tu bali alikuwa tayari kusaidia harakati za kupinga ukandamizaji hata katika nchi zilizokuwa huru.

Akizungumza kwa lugha ya Kiswahili huku akisikilizwa na maelfu ya watu walioshiriki mazishi hayo, Museven alisema walikuwa wakikutana na Mwalimu mara kadhaa kupanga mbinu za kuing'oa serikali ya Amin kabla ya vita ya Kagera.

Alisema kulikuwa na makundi mawili hapa nchini yaliyokuwa yakikutana na Mwalimu nyakati tofauti kwa ajili hiyo, moja likiwa la kwao vijana waliokuwa na miaka 20 na lile lililokuwa likiongozwa na Milton Obote.

Rais Museven aliuambia umati huo uliofurika Butiama yakuwa Mwalimu Nyerere alikuwa akikutana nao mara kwa mara bila kujali umri wao hatua ambayo haikuwa ikiwafurahisha Maafisa wa Idara ya Usalama ambao walikuwa upande wa Obote katika harakati hizo.

Serikali ya Amin ilipinduliwa mwaka 1979 baada ya majeshi ya Tanzania yakisaidiwa na waasi wa serikali hiyo kuendesha mapambano ndani ya ardhi ya Uganda.

Akitangaza vita na serikali ya Amin, Rais wa wakati huo hayati Mwalimu Julius Nyerere alisema majeshi ya Uganda yalivamia mkoa wa Kagera nchini Tanzania na kudai kuwa eneo walilovamia ni sehemu ya Uganda.

Mwalimu alisema kufuatia uvamizi huo, Tanzania ilikuwa ikiingia vitani huku ikiwa na uwezo, sababu na nia ya kumpiga Amin na kwamba isingekuwa tayari kuitikia wito wa suluhu kutoka kwa marafiki zake.

Kabla ya vita vya Kagera Rais Amin wa Uganda alikuwa akituhumu Serikali ya Mwalimu Nyerere kuwa ilikuwa ikiwapa hifadhi na mafunzo ya kijeshi waasi wa Serikali yake ambao alidai mara kwa mara walikuwa wakifanya uvamizi kutokea mpaka wa nchi hiyo na Tanzania.

Mwaka 1972 majeshi ya Tanzania na Uganda chini ya utawala wa Amin yalipata kurushiana risasi maeneo ya mpaka wa nchi hizo.

Baadhi ya walioongoza serikali ya Uganda baada ya kupinduliwa Amin ni pamoja na Meja Jenerali Tito Okello, Yusuf Kironde Lule na Godfrey Binaisa.

Hatimaye utawala huo ulirejea tena kwa Bwana Milton Apolo Obote ambaye aliendesha mauaji makubwa kabla ya kupinduliwa na Rais wa sasa Bwana Yoweri Kaguta Museven.
--
Juu RUDI


Bonyeza hapa
kushriki mjadala au kutoa maoni juu ya habari hizi na masuala mengineyo ya Kiislamu kwenye Baraza ya Wasomaji

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtz.org
 
An-nuur Home | Ukurasa wa Mwanzo | Islam Tanzania 
Links | Matoleo Yaliyopita | Sign our Guestbook