Ujamaa!
Ya kale tulosomewa, tukingali
darasani,
Mahubiri ya usawa, jinsia
na zote dini,
Bongo zetu zikalewa, maneno
tukaamini,
Hukumbuka nikacheka, hekaya
za Ujamaa!
Ilani ilinadiwa, kwisha kwenda
mkolini,
Hayuko wa kuonewa, wala
kujihisi duni,
Tumebakia wazawa, tushike
vyema sukani,
Hukumbuka nikacheka, hekaya
za Ujamaa!
Arusha kulikaliwa, Azimio
kusaini,
Ubepari kuondowa, ujamaa
kuamini,
Wenye mali wakaporwa, mashamba
na marosheni,
Hukumbuka nikacheka, hekaya
za Ujamaa!
Lengo wote tuwe sawa, wasiwepo
wa kukhini,
Kusoma na kutibiwa, na madaraka
ya ndani,
Dira tukaichukuwa, Uchina
na Urusini,
Hukumbuka nikacheka, hekaya
za Ujamaa!
Ujenzi umelemewa, ujamaa
uko chini,
Lengo halikufikiwa, tumetehemu
njiani,
Si mambo ya kuambiwa, inaona
kila mboni,
Hukumbuka nikacheka, hekaya
za Ujamaa!
Shule zinalaumiwa, kufunza
elimu duni,
“Wajamaa” tunachekwa, wala
haya hatuoni,
Wana wa watu “wakubwa”,
wanasomeshwa Londoni,
Hukumbuka nikacheka, hekaya
za Ujamaa!
Hata tunakotibiwa, dawa hazipatikani,
Muhimbili yakimbiwa, watu
wenda “Uropani”,
Hakika tumezidiwa, kwa maoni
ya kichwani,
Hukumbuka nikacheka, hekaya
za Ujamaa!
Wajifunze wasofunzwa, uungu
wanotamani,
Kutaka kuabudiwa, kwa maoni
ya kichwani,
Kina Mao wameachwa, watu
hawaulizani,
Hukumbuka nikacheka, hekaya
za Ujamaa!
Kaditamati makiwa, ujamaa
kitu duni,
Hadharani umetupwa, wala
hatuna huzuni,
Mwenye kufaa kuigwa, ni
mjumbe wa Manani,
Hukumbuka nikacheka, hekaya
za Ujamaa!
Jihad Saballa,
Box 347,
Shinyanga.
Leo ninaunguruma, Kiko mithili
ya simba,
Uwanjani nasimama, nasema
tukaze kamba,
Sikizeni nchi nzima, Bara,
Unguja na Pemba,
'Mmm' 'mmm' amkeni, oneni
hii dhuluma.
Nanguruma asubuhi, enyi macho
mlofumba,
Oneni Muembe chai, wameuwa
kwa kutamba,
Kwa hasira kama chui,
pongezi wakajigamba,
'Mmm' 'mmm' amkeni, oneni
hii dhuluma.
Leo ninaunguruma, nasema
tukaze kamba,
Umekubuhu unyama, utu hawendi
sambamba,
Haki tupinge hujuma, tusibaki
ombaomba,
'Mmm' 'mmm' amkeni, oneni
hii dhuluma.
Oneni hii dhuluma, simaneno
ya kupamba,
Paroko alituchoma, kupitia
kwa Makamba,
Watoto akina mama, wakapigwa
na kuvimba,
'Mmm' 'mmm' amkeni, oneni
hii dhuluma.
Leo ninaunguruma, nasema
tukaze kamba,
Ikulu tuliyatuma, madai
haki kuyumba,
Haki ipewe heshima, dhuluma
yavunja nyumba,
'Mmm' 'mmm' amkeni, oneni
hii dhuluma.
Kimya hiki cha dola, cha
haki ama kasumba,
Ushindweje utawala, kuwafikisha
kizimba,
Walopiga kama swala, Chuki
shaba ikachimba,
'Mmm' 'mmm' amkeni, oneni
hii dhuluma.
Hapa mwisho kaditama, ujumbe
tukaze kamba,
Pamoja tukisimama, utafutika
umwamba,
Twende tusirudi nyuma, zetu
haki wameramba,
'Mmm' 'mmm' amkeni, oneni
hii dhuluma.
Idd Kikong'ona,
Morogoro.
|
|