Waislamu Chechnya wajizatiti kuihami Grozny
 

MAMIA ya askari wa Kirusi wameuliwa na wapiganaji wa Kichechnya, wiki hii.

Katika mapigano makali yanayoendelea, Warusi wanataka kuutwaa mji wa Grozny.

Kwa mujibu wa shirika la habari liitwalo Agence France -Press (AFP) majeshi ya Urusi yalipoteza magari 70 ya kijeshi kwenye mapambano makali yaliyotokea katika miji ya Argun na Alkhan-Yurt.

Miji hiyo ipo kilometa chache kutoka mji wa Grozny.

Kwa mujibu wa maelezo ya kamanda wa majeshi ya Chechnya, Jenerali Alsambek Arsayev, miji ya Noibyora na Novogroznensky ambayo ilidaiwa kutekwa na Warusi bado ipo mikononi mwa Wachechen.

Wapiganaji wa Chechnya wapo katika siku ya sita wakijaribu kuyazuia majeshi ya Urusi kuingia Grozny.

Historia ya ukoloni na udhalimu wa Urusi kwa Chechnya unaanzia karne ya 18. Mwaka 1785 Wachechen wakiongozwa na Mansur Usherma alianzisha mapambano dhidi ya ukoloni huo.

Kufikia mwaka 1854 ambapo Warusi walikuwa wamewaua takriban Wachechen wote wenye uwezo wa kupigana.

Hata hivyo, kati ya 1859 na 1944 mapambano ya mara kwa mara yalikuwa yakiibuka Wachechen wakipigania uhuru wao.

Matukio hayo yalikuwa yakijibiwa kwa ukatili wa kutisha ambapo viongozi walikuwa wakiuliwa na watu wengi kuhamishiwa Siberia.

Mwaka 1944, ulimwengu ulishuhudia mauaji ya maangamizi ambapo Waislamu wa Chechnya walitolewa katika miji yao na kutupwa Siberia na Asia ya kati.

Wachechen wapatao 700 katika kijiji cha Khaibakh ambao walikataa kuhama walitiwa katika tanuri na kuchomwa moto.

Inakisiwa kuwa kati ya 35% na 50% ya Wachechnya waliuliwa katika zoezi hilo la kung'olewa katika miji yao.

Baada ya kuanguka kwa ukomunisti Chechenya ilijitangazia uhuru Novemba 27, 1990. Oktoba 27, 1991 walifanya uchaguzi wa kidemokrasia uliokuwa na waangalizi wa kimataifa.

Johar Dudayev alipata 90% ya kura na hivyo kuchaguliwa kuwa Rais. Urusi haikutambua uhuru huo wa Chechnya.

Desemba 11, 1994 Urusi ilituma jeshi lenye askari 40,000 mamia ya vifaru, ndege, mamia ya helkopta, kuwapiga Waislamu Chechnya.

Miji na vijiji viliangamizwa na Waislamu wapatao 50,000 kuuliwa katika mapambano yaliyochukua miezi 15.

Mauaji, mateso na kuharibu mali zimekuwa baadhi ya mbinu zinazotumiwa na Warusi dhidi ya Waislamu wa Chechnya ili wasalimu amri.

Waislamu hawa wa Chechnya wanakabiliwa na yote haya kwa ile azma yao ya kutaka kujitawala.

Ulimwengu umepiga kimya wakati Wachechen wakiuliwa na miji yao kuangamizwa. Inadaiwa hilo ni tatizo la ndani ya Urusi.

--
Juu RUDI


Bonyeza hapa
kushriki mjadala au kutoa maoni juu ya habari hizi na masuala mengineyo ya Kiislamu kwenye Baraza ya Wasomaji

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtz.org
 
An-nuur Home | Ukurasa wa Mwanzo | Islam Tanzania 
Links | Matoleo Yaliyopita | Sign our Guestbook