MASHAIRI
 

Kinanuka!

   Kuna udini udini lo! kinchi kinanuka,
   Kuuawa waumini, tena bila mashitaka,
   Kupigwa Misikitini, na kejeli kadhalika,
   Mhu! kinanuka kinchi, chuki udini udini.
 
   Inanuka nuka, mbaya harufu nchini,
   Raia tunavyongeka, kama vile wahaini,
   Vipigo tunapigika, na kusweka gerezani,
   Mhu! kinanuka kinchi, chuki udini udini.
 
   Kuna udini udini lo! kinchi kinanuka,
   Katiba ni matendoni, nadharia ni dhihaka,
   Twauawa masikini, sheria wazifunika,
   Mhu! kinanuka kinchi, chuki udini udini.
 
   Paroko alitamka, bado ushahidi gani,
   Kamanda alohusika, amri kampa nani,
   Na bunduki wakashika, wakalenga vifuani,
   Mhu! kinanuka kinchi, chuki udini udini.
 
   Kuna udini udini, lo! kinchi kinanuka,
   Walouwa kulikoni, washindwe kushitakika,
   Sirikali muna nini, uzito kuwajibika,
   Mhu! kinanuka kinchi, chuki udini udini.
 
   Huku kudharaulika, Ikulu hadi bungeni,
   Kutuona takataka, wachochezi na wahuni,
   Ndipo tunanung’unika, haki mtatupa lini,
   Mhu! kinanuka kinchi, chuki udini udini.
 
   Hebu nanyi tazameni, usukani muloshika,
   Iweje sawa kwa nini, wale walokizika,
   Walouwa hadharani, sheria walokizika,
   Mhu! kinanuka kinchi, chuki udini udini.
 
   Idd Kikong’oa,
   Morogoro.



Dini na siasa

   Fikira nazikusanya, kujibu hili shairi,
   Yarabi hisani fanya, uishushe yako nuri,
   Jamii niweze onya, kwa haya yaloshamiri,
   Ni vita vya kifikra, lazima tuviepuke.
 
   Lazima tuwe makini, laa sivyo tutapotea,
   Kwa vita vilo nchini, ni mtihani tambua,
   Makusudi wamebuni, wale wenye chafu nia,
   Ni vita vya kifikra, lazima tuviepuke.
 
   Huwezi kuiepuka, siasa ndani ya dini,
   Ni Rabi aloviweka, viwe pamoja yakini,
   Vipi leo tunataka, kuvigawa twepukeni,
   Ni vita vya kifikra, lazima tuviepuke.
 
   Fikra hizi jamani, kweli zimepandikizwa,
   Kuivunja yetu dini, ni mila yetu kuchakazwa,
   Sijui wafanye nini, hali wao washawezwa,
   Ni vita vya kifikra, lazima tuviepuke.
 
   Hii ni njama jamani, ilokaliwa vikao,
   Ni lazima tujueni, watu wayataka yao,
   Tutakuwa matatani, tukiwafuata wao,
   Ni vita vya kifikra, lazima tuviepuke.
 
   Hao wanaotangaza, tukiwa Misikitini,
   Siasa haitoweza, kuchanganyika na dini,
   Lengo ni kutupambaza, tusitoke utumwani,
   Ni vita vya kifikra, lazima tuviepuke.
 
   Kila kiumbe jamani, lazima kiwe na dini,
   Na humo ndani ya dini, siasa haikosekani,
   Yatwambia Qurani, kitabu chake Manani,
   Ni vita vya kifikra, lazima tuviepuke.
 
   Tamati naishilia, tufuate ya Jalia,
   Tupuuze yanongia, yanopotosha jamia,
   Fikira za kupotoa, tusije zifuatia,
   Ni vita vya kifikra, lazima tuviepuke.
 
   Rukia Othman,
   Dar es Salaam.

--
Juu RUDI


Bonyeza hapa
kushriki mjadala au kutoa maoni juu ya habari hizi na masuala mengineyo ya Kiislamu kwenye Baraza ya Wasomaji

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtz.org
 
An-nuur Home | Ukurasa wa Mwanzo | Islam Tanzania 
Links | Matoleo Yaliyopita | Sign our Guestbook