BARUA



Tujitoe muhanga kuinusuru Tanzania

Ndugu Mhariri

NIMEPATA uchungu mkubwa kusikia na kuona jinsi serikali inavyowadhalilisha wananchi haswa wale walalahoi.

Wazee wetu walijitoa muhanga kupambana na serikali ya kikoloni kwa matarajio kuwa watoto wao tutaishi maisha bora yasiyo na hofu wala bughudha ila upendo, amani na utulivu. Walifikia hatua hiyo baada ya kuona kuwa serikali ya kikoloni inawadhalilisha na kuwabagua kwa misingi ya dini.

Pato la nchi lililochangiwa na wananchi wote lilipelekwa kuanzisha na kuendesha mashule ya Kikristo ambayo vijana wa Kiislamu iliwalazimu kubatizwa ili wapate elimu.

Watawala walitumia sehemu kubwa sana ya pato la taifa kwa shughuli zao za kifahari huku walalahoi wakibaki bila hata huduma muhimu za jamii ilhali wao ndio wazalishaji.

Hali ile au zaidi ndiyo inayotukabili hivi sasa kwani matabaka yameota mizizi kwa misingi ile ile ya dini na vyeo.

Mashule na mahospitali ambayo yalijengwa kwa fedha za wananchi wote japo yaliitwa ya Kikristo, hivi sasa serikali imeyakabidhi tena mikononi mwa Kanisa.

Serikali imejenga uhusiano wa karibu na mataifa na mashirika ya Kikristo ili kuwapa Wakristo misaada mbalimbali ya kijamii na kimaendeleo. Jambo hili ni tofauti sana kwa Waislamu ambapo mataifa na mashirika ya Kiislamu huzuiwa kabisa au kupewa masharti makali kutoa huduma hapa nchini.

Watawala wamekuwa watumiaji wabaya wa mapato ya taifa ambayo ni kOdi za wananchi, huku wananchi wanakosa hata zile huduma muhimu za maisha.

Mahospitali na mashule ya wananchi yametelekezwa na kufanywa ya gharama kubwa wasizoweza kuzilipa japo huduma zenyewe ni duni mno. Wakati watoto wa watawala wanasoma katika mashule ya kimataifa ndani na nje ya nchi, serikali bila kujali jukumu lake la kuwasaidia watoto wa wananchi wanaokosa elimu kwa kushindwa gharama. Inaendesha kampeni ya nyumba hadi nyumba kuwakamata na kuwashitaki walalahoi walioshindwa kuwasomesha watoto wao kwa kukosa ada.

Jambo la kusikitisha zaidi ni kuwa serikali inawakamata na kuwarundika katika majengo ya shule za msingi wananchi ambao hawana uwezo wa kupata hata chakula na malazi, wengi wao wakiwa ni walemavu. Wananchi hao wamefikia hatua hiyo kutokana na sera za serikali kushindwa kutumia rasilimali za asili zilizojaa Tanzania.

Mwisho napenda kuwakumbusha Watanzania wenzangu kuwa, kazi waliyokusudiakuifanya baba zetu wakati wa mkoloni iko mbele yetu na ni lazima tuikabili kwa manufaa ya kizazi kijacho.

Mwanafunzi
Kimundia A. Kimundia,
Ugweno,
Moshi.



Hatupati gazeti la AN-NUUR Mtwara

Ndugu Mhariri

NITASHUKURU sana endapo nitapata nafasi katika gazeti lako ili niweze kutoa maoni yangu.

Ni ukweli usiofichika kwamba gazeti hili ni shule tosha kwa Muislamu anayefahamu dini yake na yule asiyefahamu huweza kujifunza mengi kupitia gazeti hili.

Aidha, baadhi ya faida ambazo hupatikana humo gazetini ni pamoja na kumuwezesha msomaji kufahamu habari za lishe, sheria, Qur'an, uonevu ndani na nje ya nchi dhidi ya Waislamu na jinsi ya kupigania na kusambaza dini hii ya kweli mbele ya Mola ili tupate faida hapa duniani na kesho akhera.

Chombo muhimu kinachozingatiwa na msomaji anufaike ni wakati. Yaani gazeti lipatikane kila Ijumaa.

Lakini hapa Mtwara mjini imekuwa kinyume. Kwa maana ya kwamba hatulipati kila Ijumaa badala yake zaweza kupita hata wiki mbili hatujapata na tulipowahoji MIDECE (Mtwara Islamic Development Centre) ambao ndio wakala walisema: " Tatizo ni usafiri, kwani wanategemea basi".

Cha ajabu mabasi huja huku kila siku kuanzia Juni mwaka jana hadi leo.

Hivyo, nakuomba Mhariri kitafutwe chanzo cha udhaifu huu na kipatiwe ufumbuzi mara moja ili umma wa Kiislamu uendelee kupata neema hii nono.

Kuonewa Mkungu,
S.L.P 528,
Mkunwa,
Mtwara.


Sekondari ya Pugu kupewa Wakatoliki?

Ndugu Mhariri

NAOMBA unipe nafasi katika gazeti lako ili nitoe maoni yangu.

Kwenye taarifa ya habari ya Radio One saa mbili kasoro robo na saa nne usiku Januari 12, mwaka huu walitangaza kuwa shule ya sekondari ya Pugu wataifanya ya Kikatoliki, jambo hili limejenga hisia kuwa serikali inaegemea upande mmoja kwenye elimu.

Siku za nyuma nilisikia hata chuo cha Kilimo cha Nyegezi Mwanza watapewa Wakristo. Je, tuelewe vipi serikali yetu?

Haji R. Langa,
P. O. Box 13407,
Arusha.


Kisiju tumefufuka

Ndugu Mhariri

KWANZA tunawapongeza wanawake wa Dar es Salaam kwa kuitikia wito uliyotolewa kupitia gazeti hili na Bwana Salum Hamis wa Nasibugani wa kuwataka wanawake na taasisi zote za ulinganiaji kuja Kisiju kuleta uamsho.

Baada ya wanawake chini ya uongozi wa Ukht Safia Ismail (Nyauyaga) kufanya kazi nzito ya kuwaelimisha wanawake wa Kisiju, hali imeanza kubadilika na kuonesha matumaini ya kufufuka Uislamu huku Kisiju.

Tunaomba tuzidi kutembelewa.

Bakari Omar,
Kisiju.


Sheikh Mkuu unatupeleka wapi?

Ndugu Mhariri

NIMESOMA gazeti la Nipashe la Januari 10, mwaka huu ukurasa wa tatu kichwa cha habari: "Waislamu waaswa kuvumiliana. Sheikh huko Dodoma alisema: "Hakuna uhuru usiokuwa na mipaka, hivyo aliwataka Waislamu kuheshimu mipaka iliyowekwa ikiwa ni pamoja na kutii sheria za nchi.

Kwa kweli Sheikh ulipofikia panatisha. Tunakushangaa unapotuhimiza amani na kutii sheria za kitwaghuti, wakati Rais anasema mauaji ya Mwembechai hawezi kuunda tume ya kuchunguza mauaji. Je, hawa ndio wakuwavumilia?

Muddatthir Sulaiman,
Morogoro.


Meliniam University!

Ndugu Mhariri

TUNAFURAHI sana kusikia BAKWATA nao sasa wanapanga mikakati ya kuwaendeleza Waislamu kwa kuanzisha Chuo Kikuu, kwa kauli wana lengo la kuwaendeleza Waislamu nasi tunaunga mkono.

Lakini jina la Chuo ndiyo linatupa wasiwasi sisi Waislamu kwa sababu jina lenyewe linatukuza na kuitangaza kalenda ya Kikristo.

Kwa hiyo tunawaomba wahusika tafuteni jina lingine hata Hijra au Anno Hijiry linafaa kwa sababu ndiyo kalenda ya Waislamu na Chuo Kikuu ni cha Waislamu kuliko Milenia ambayo ni Kalenda ya Wakristo sisi Wasilamu tunapinga kalenda hiyo kwa nguvu zetu zote.

Waislamu,
Kisiju.
 

--
JuuRUDI


Bonyeza hapa
kushriki mjadala au kutoa maoni juu ya habari hizi na masuala mengineyo ya Kiislamu kwenye Baraza ya Wasomaji

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtz.org

 
An-nuur Home | Ukurasa wa Mwanzo | Islam Tanzania
Links | Matoleo Yaliyopita | Sign our Guestbook