In-nalillahi Wainanailain raajiuun
Lakini kosa letu nini?
AN-NUUR Na. 157, Julai 10 - 16, 1998
EE Mwenyezi Mungu kama tumekukosea; kuwakosea wananchi wenzetu au kuikosea serikali hii kiasi cha kustahili adhabu hii, hakika wewe ni mwingi wa kusamehe; Ya Allah! Kwako tunashitaki udhaifu wetu. Nguvu zetu na udhalilifu wetu katika macho ya watu. Ewe Mwingi wa rehema na huruma kuliko wote mwenye huruma. Wewe ndiwe Bwana wa wanyonge na Wewe Ndiwe Bwana wetu. Ni katika jamii za aina gani umehiyari tuishi waja wako! Jamii isiyo na huruma bali iliyotayari kudai damu na nyama ya watu hali ikikenuwa meno. Jamii isiyojali hata ile haki ya kuishi, uliyompa kila kiumbe!
Ya Allah, wenzetu wanafyekwa gerezani japo hawajahukumiwa kwa kosa lolote. Agizo lako kwamba tusidhulumu limeruka patupu katika jamii hii. Ya Rabbi hakika wewe si mwenye kuwadhulumu waja wako; lakini sisi tumekuwa ni wenye kudhulumiana!
Tumedhulumu nafsi zetu kwa kushindwa kuwatetea wanaoteseka Keko na Segerea mpaka wamelazimika kujitetea wenyewe kwa kugoma kula! Ya Rabbi tunaomba utunusuru na ghadhabu zako au kutokuwa radhi na sisi. Hapana nguvu wala uwezo ila kutoka kwako.
Ya Rabbi kupitia kwa Mtume wako umetuagiza tumsaidie anayedhulumiwa na anayedhulumu.
Tumekuwa tukijali nafsi zetu na kuwasahau waja wako wanaoteseka kwa kusema kwao kwamba mja wako Issa (a.s.) si Mungu. Tunaswali na kukamua tasbihi tukitaraji pepo yako huku tukiwasahau waja wako wanaonyimwa dhamana na matibabu!
Tunakula na kunawiri huku hatuna habari kwamba wenzetu wanakondeana Keko kwa kukosa kula tena chakula ambacho kimepatikana baada ya wake zao kuhangaika sana!
Kwanini wasihangaike wakati umma wa Kiislamu umewatelekeza. Kila mtu anajali mke wake na watoto wake! Kwanini wasigome kula; silaha gani nyingine wanayo wakati Masheikh, wazee na Waislamu wote kwa ujumla hawamsaidii dhalimu kwa kumkemea!
Ya Rabbi pamoja na udhaifu wetu na kujidhulumu nafsi zetu kwa kutowatetea wanaodhulumiwa, lakini umetueleza pia kupitia kwa Mtume wako kwamba "Lau watu wangeaminiwa kwa madai yao tu, baadhi ya watu wangedai damu na mali ya watu wengine".
Ni mwezi wa nne sasa wenzetu wanateswa gerezani bila madai dhidi yao kuthibitishwa. Tunahisi kuzidhulumu nafsi zetu kwa kutowahami wenzetu; lakini tunaushuhudia pia udhalimu huu wa kuteswa wenzetu kabla ya kuthibiti kosa lao.
Kama haya yanayotusibu yametokana na mikono yetu,Yarabi tunusuru na utuoneshe tulipokosea. Ama kama tunateswa bure bure tu pasi na haki Ya Rabbi tumiminie subra, na utujaalie Istiqama katika njia yako. Wanaotufanyia haya ni waja wako na Wewe Ndiwe Mwenye Nguvu na Mamlaka juu yao.
Makafiri na washirikiana wa Makka waliwatesa Waislamu kwa kila aina ya mateso. Wengine wakiwabanika juani, wakiwachoma kwa vyuma vya moto, kuwapiga na kuwaua kwa njia za kutisha. Wako waliofungwa miguu yao kwenye farasi wawili kisha wakavutwa kuelekea pande tofauti wakachanika pande mbili.
Mateso yalivyozidi Mtume (s.a.w.) aliwaelekeza Waislamu wahamie Uhabeshi kwani huko palikuwa na Mfalme ambaye si mwenye kumdhulumu mtu.
Miongoni mwa ujumbe Waislamu waliomfikishia Mfalme Najash ni pamoja na kumfahamisha kwamba Yesu si Mungu bali ni Mtume wa Mwenyezi Mungu aliyezaliwa kwa miujiza kupitia kwa Mama Mariamu.
Waislamu hao wakiwemo Ruqaya bint wa Mtume (s.a.w.) waliachwa waishi kwa salama na amani huku wakieneza imani yao.
Najash serikali yake ilikuwa ya kidini ya Kikristo. Haikuwa isiyo na dini kama yetu. Najash hakutangaza kwamba serikali yake haina dini ila watu wake wana dini! Ilikuwa ya Kikristo kwa nadharia na vitendo. Lakini hakuwafunga hao Waislamu wakimbizi.
Hakuwahukumu kwamba wanakashifu dini yake kisha akawaweka ndani bila ya kuwapa dhamana!
Hakuwaweka ndani akawanyima matibabu.
Hawa ndio Wakristo tulioelezwa katika historia
kwamba kwa kumjua kwao Mungu hawakumdhulumu mtu.
MUDA mfupi baada ya Bw. Magezi kunyakuliwa kundi kubwa zaidi la askari wakiwemo wale wa kutuliza ghasia (FFU) walifika Mwembe Chai na kulizingira eneo la msikiti hali iliyowafanya Waumini waliokuwa wakifanya ibada msikitini washindwe kutoka kwa kuogopa kushambuliwa.
Usiku ulipoingia askari zaidi waliongezwa na eneo lote la Mwembe Chai na maeneo ya jirani yakazingirwa. Wananchi wengi walikosa uhuru wa kuendelea na shughuli zao kwenye maeneo hayo na wapita njia ambao wengi walikuwa hawana taarifa ya kilichokuwa kinaendelea walijikuta wakikamatwa.
Ilipofika usiku wa manene TANESCO (Shirika la umeme) waliamrishwa kukata umeme katika nguzo iliyokuwa na 'line' ya kuingizia umeme msikitini. Baada ya kukamilika kwa zoezi hili eneo lote la msikiti liligubikwa na giza totoro. Wakati waumini waliozuiliwa ndani ya msikiti wakiwa hawaonani kwa kiza, askari waliwamiminia mabomu mengi ya moshi unaopalia kooni, kutoa machozi na kuwasha mwili na hivyo kuwafanya wachanganyikiwe zaidi.
Huku waumini bado wakiwa katika hali ya kuchanganyikiwa muda mfupi baadaye walivamiwa na maaskari waliokuwa wamefanikiwa kuvunja milango ya msikiti, wakapigwa, wakakanyagwa na kuburutwa kabla ya kuchukuliwa na kupelekwa kituoni. Katika operesheni hiyo waumini wengi walipata majeraha makubwa.
Askari walipokuwa wamezingira msikiti, Waislamu walioshikwa na uchungu ambao hawakuwa ndani ya msikiti walipinga tendo la serikali kuzingira msikiti kwa kurusha mawe, na kuwasha mioto barabarani kuchoma moto magari,. Mambo haya ya litokea sawiya, cha ajabu ni kwamba badala ya askari kwenda kuwakamata wanaochoma magari na kuyajeruhi kwa mawe, waling'ang'ania kuzingira msikiti ambao waliokuwemo walikuja kuswali. Ndio maana waliokamatwa wengi walikuwa vikongwe na watoto na watu wazima. Dhana kuwa waliochoma magari na kuharibu mali ndio waliokimbilia msikitini sio sahihi kabisa. msikiti ulikuwa umefungwa na ulizingirwa na polisi hivyo uwezekano wa kukimbilia msikitini kwa walioinyoshea misuli FFU haukuwepo. Wale waumini waliopigwa mabomu, waliopigwa virungu, magumi mateke na kuburuzwa kwenye makarandika ya polisi na kusombwa kituoni na hatimae kufunguliwa mashtaka hawakuwa na hatia yoyote zaidi ya kwenda kuswali.
Usiku wa maonevu ulipita na asubuhi yake Ijumaa tarehe 13/2/98 Waislamu wengi waliopata habari hizi za kusikitisha waliswali swala ya Ijumaa Mwembe chai kupata usahihi wa jambo lenyewe.
Aidha, kabla ya swala ya Ijumaa Februari 13, 1998, kutokana na viongozi wote wa Msikiti kusambataratishwa na polisi jana yake hapakuwa na dalili kuwa swala ya Ijumaa ingekuwepo hadi saa 3 asubuhi Msikiti ulikuwa mtupu.
Kwa mujibu wa maelezo ya baadhi ya watu wanaoswali Msikiti huo, kikundi kidogo cha vijana kiliamua kumfuata Katibu wa Kamati ya Kutetea Haki za Waislamu, Sheikh Ponda Issa Ponda.
Inaelezwa kuwa kikundi hicho cha vijana pamoja na kumpatia Katibu taarifa za hali iliyotuka jana yake (usiku wa Alhamisi), pia lilimuomba afanye utaratibu wa kupata Imamu na msoma Khutba ili kuwezesha kufanyika swala ya Ijumaa ambayo ilikuwa mashakani siku hiyo.
Baada ya taarifa hiyo, vijana hao wakiandamana na Katibu huyo pamoja na Imamu aliyepatikana walichukuzana hadi Msikitini hapo.
Uwezekano wa kuswaliwa Ijumaa Msikitini hapo siku hiyo ulianza kuonekana baada ya kufika Sheikh Ponda ambapo kufikia saa sita mchana Msikiti ulifurika watu wengi.
Sheikh Ponda na kamati yake ya kutetea haki za Waislamu ilipo huishwa kwa mara ya pili baada ya mwaka 1993 wakati wa mabucha ya nguruwe masuala ya waliokamatwa na masuala mengine ya namna hii.
|
Links | Matoleo Yaliyopita | Sign our Guestbook |