UKOSEFU WA HUDUMA MUHIMU NCHINI

Wachachafyeni watawala

BILA kutikiswa viti vya enzi, wananchi wasiote kupata haki zao za msingi na huduma stahiki.

Muda wa kuwa njia za kwenda Ikulu na Bungeni zimeonekana 'nyeupe' viongozi wataendelea kujali maslahi yao binafsi.

Hayo ni maoni ya baadhi ya wananchi wakitathmini tatizo sugu la maji na hatua zinazochukuliwa na serikali.

"Wanasiasa hawa lao ni kukaa madarakani tu hawana habari na shida za wananchi. Na kama hatutatikisa viti vyao wakaviona vya moto, tutaendelea kunywa maji machafu na kupata kipindupindu", amesema Bw. Daud Kengia.

Akizungumzia tatizo la maji eneo analotoka Ubungo amesema, maji bombani hutoka mara moja baada ya wiki mbili. Na yakitoka ni kwa muda usiozidi masaa mawili.

"Maji ya mashimo yasiyo salama ndiyo tunayotumia. "Taifodi" imekuwa sehemu ya maisha yetu", amesema Bw. Kengia na kuongeza, juhudi zao kulifuatilia tatizo hilo zimekwaa kisiki. Amesema si viongozi wa mamlaka ya maji wala wa serikai wanaoonesha kujali shida yao.

"Agenda ya wanasiasa ni kukaa madarakani na maadhali hatuwabughudhi, hawawajali kuwa hatuna maji", amesema Mama Mlay na kuwataka wananchi wasijiangamize kwa uungwana wao.

"Upole wetu ndio ujinga wetu na adui yetu mkubwa . Tutakosaje maji wiki tatu bila ya dharura inayokubalika na viongozi wetu wanalala buheri...", amesema mama huyo wa Ubungo ambaye amedai kuwa wao kutoka maji ni dharura inayotokea kila baada ya wiki mbili au tatu. Amesema wamedumu na hali hiyo kwa zaidi ya miaka mitatu.

Mama Mlay amesema bila ya wananchi kusimama imara na kuwatikisa watawala wanaotwaa kodi bila ya kutoa huduma ya maji, wataendelea kunywa maji machafu na kumalizwa na 'taifodi' na kipindupindu.

Akizungumzia suala hilo Bw. Ibrahim amesema Mwalimu Nyerere kaacha urithi hatari. "Kiongozi ni mwenzetu hata kama anaiangamiza nchi. Kiongozi ni mchapakazi hata kama uchumi unadorora. Kiongozi anayejali wananchi hata kama wananchi wenyewe wanakufa kwa kipindupindu kwa kukosa huduma ya maji safi na salama", amesema na kuongeza na "huyo njia yake ya kwenda Ikulu ama Bungeni ni nyeupe. Ana hakika ya kura hata kama kuwepo kwake madarakani hakuna msaada wowote kwa wananchi".

Akizungumzia kemeo la Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni kuwa watu ni wachafu ndio maana kuna kipindupindu, Bw. Halfan alimtaka alete maji kwanza ndio awasute wananchi.

"Wananchi wanalazimika kutumia maji machafu kwenye mabwawa huku kodi wanalipa, halafu wanashutumiwa wachafu nani wa kubeba lawama awali?" alihoji.

Alisema kuondoa kejeli hizi ni lazima wananchi wajitokeze na wawe madhubuti kudai haki zao. "Mpaka waone viti vyao vinakaribia kuporomoka, ndio watawajali, lakini mkinung'unikia vyumbani hawajali. Ni lazima kila inapobidi wananchi watoke kwa sauti moja wadai haki zao", alisisitiza.

Maeneo kadhaa jijini kwa muda mrefu sasa yamekuwa na tatizo kubwa la maji. Wananchi wamekuwa wakichimba visima visivyo salama na hata kuchota maji madimbwini. Hali hiyo imeibua kipindupindu hasa katika wilaya ya Kinondoni.

Pamoja na tahadhari zinazotolewa kukabiliana na hali hiyo, wananchi wameitaka serikali itoe huduma ya maji kwanza.

Wamesema kipindupindu hakitamalizwa kwa kupiga marufuku uuzaji wa maandazi na mama ntilie. Huduma ya maji safi na salama ni muhimu na hilo ni jukumu la serikali inayotwaa kodi za wananchi.

--
JuuRUDI


Bonyeza hapa
kushriki mjadala au kutoa maoni juu ya habari hizi na masuala mengineyo ya Kiislamu kwenye Baraza ya Wasomaji

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtz.org

 
An-nuur Home | Ukurasa wa Mwanzo | Islam Tanzania
Links | Matoleo Yaliyopita | Sign our Guestbook