Dkt. Z.S.M Mochiwa
MTAALAM mmoja alipata kusema kuwa wingi wa lugha katika nchi changa ni miongoni mwa dalili za uchanga wa nchi hizo kimaendeleo. Tanzania ni miongoni mwa nchi hizo ambazo zina lugha nyingi. Wingi huu wa lugha unaleta umaskini mkubwa wa kimawasiliano. Watanzania walio wengi wana lugha za makabila yao. Lugha hizi ndizo zinazowapa pumzi yao ya kwanza ya kijamii. Kwa kuzijua lugha hizi Watanzania husharabu adabu za kwao, taratibu za makusano katika jamii zao. Kwa kutokana na lugha hizi, Watanzania hupata kujua mahusiano yao na wale wanaowazunguka. Kwa ufupi lugha hizi ndizo za malezi yao. Lugha hizi za kikabila zinakisiwa kuwa zaidi ya mia moja na ishirini.
Tanzania ina lugha mbili za makuzi. Lugha hizi ni zile zinazohitajika ndani ya mfumo wa elimu. Hali ilivyo sasa ni kwamba Kiswahili ndicho kinachokuzia mbongo za vijana katika shule zote za msingi nchini. Wanafunzi wa shule hizo hukusana na walimu wao kwa njia ya Kiswahili.
Kwa maana hiyo anapoingia shule ya msingi, mtoto hunyang'anywa lugha ya kikabila aliyozoea na kulazimishwa kutumia Kiswahili. Hili ni badiliko ambalo, kama nilivyopata kusema kwingineko, hutenganisha uzoevu uliopatikana wakati wa malezi na ule utakaopatikana katika makuzi ya kwanza, ya shule ya msingi. Aidha, kutokana na badilio la lugha, dhana mbalimbali zilizopatikana kwenye lugha hiyo ya malezi huweza kupotea au kuparaganyika.
Kwa bahati nasibu tu, Kiswahili, lugha ya kwanza ya makuzi, kina nasaba kubwa na lugha nyingi za makabila. Ubantu wake unakifanya Kiswahili kiwe na msamiati na sarufi ambayo hukaribiana sana na lugha hizo.
Inasemekana kuwa zaidi ya asilimia hamsini ya msamiati wa Kiswahili una asili ya Kibantu. Kweli hii ya kihistoria imekuwa chimbuko la wepesi kwa watu wanozungumza lugha yoyote ya Kibantu kukidaka na kukisharabu Kiswahili. Kwa msingi huu, badiliko la kumlazimisha mwanafunzi kuacha lugha ya kikabila na kutumia Kiswahili halileti misukukosuko mingi ya kisaikolojia.
Mara nyingi baada ya mwaka au miaka miwili mwanafunzi hukimiliki Kiswahili kwa kiwango cha kumwezesha kukitumia kwa kuchanuzia masihara au kweli ya uzoevu wake. Hivyo, katika kipindi kifupi, Kiswahili humwia mwanafunzi chombo thabiti cha kupokelea na cha kuchanuzia maarifa, taarifa na hisia zake. Ikisemwa vinginevyo, mwanafunzi hupata uwezo wa kusuka semi zake na wa kusukua, yaani kuelewa kikamilifu, semi za wenzake, zikiwa ni pamoja na za walimu wake.
Baada ya kujenga msingi thabiti wa ufahamu wake wa Kiswahili mwanafunzi huyo hunyang'anywa na kukabidhiwa Kiingereza kuwa lugha yake ya kujifunzia. Badiliko hili linamjia baada ya kuwa kajifunza Kiingereza katika shule ya msingi kwa jumla ya saa zisizozidi mia nane (800) (rej. Mochiwa 1991). Watalaam na/au viongozi wa Tanzania wameridhika kabisa kuwa baada ya kufundishwa Kiingereza na walimu hawa waliopo hapa nchini kuanzia darasa la tatu hadi la saba, kwa idadi hiyo ya saa na kwa vifaa hivi tulivyonavyo, Kiingereza hicho kitafundishika na kitakuwa chombo cha kusukia na kusukulia maarifa ya shule za sekondari.
Kwamba mwega wa badiliko hili ni muujiza wa Mwenyezi Mungu, huthibitika kwa njia mbili. Kwa utaalam uliopo, haiwezekani kuisharabu lugha ya malezi bila ya kutumia saa 18,000. Hii ina maana kuwa, kabla ya kuingia shule mwanafunzi alitumia miaka mitano au sita ya kwanza ya maisha yake kwa kujifunza lugha ya mama yake ambayo ndiyo ya malezi yake. Muda huo ndio uliomwezesha kujenga msingi thatibi wa sarufi ya lugha hiyo. Watu wote waliokuwa wamemzunguka walikuwa wakizungumza lugha anayojifunza. Isitoshe, katika kipindi hicho, mtoto hakuwa na shughuli nyingi alizopangiwa ambazo zilihitaji makini ya akili yake. Kwa kifupi mtoto hakuwa na ratiba nyingine rasmi za kumshughulisha kiakili.
Pili, usharabu wa lugha ya Kiingereza, ambayo inakusudiwa kuwa ya makuzi katika kiwango cha sekondari, hutegemea kufundishana. Hii ina maana kuwa usharabu unatokana na mtoto kuwa mwanafunzi wa mwalimu fulani. Ubaya wa utaratibu huu wa usharabu wa lugha ya Kiingereza ni ule uwezekano wa kuathiriwa na kiwango duni cha mwalimu, zana duni za ufundishaji na ukosefu wa mchango wa mazingira katika kuimarisha stadi zinazofundishwa. Aidha, inapokumbukwa kuwa, kinapofundishwa, Kiingereza hakina matumizi ya papo kwa papo ndani wala nje ya darasa, jitihada zote za kukisharabu ni kama mchezo wa kuigiza. Mwanafunzi anapata jina la "Betty" na Mwalimu "Mr Winterbottom".
Kwa maneno mengine msemo wanaojifunza hauhitajiki kuendeshea maisha yao sasa hivi! Hapana shaka kuwa, usharabu huu haupati msukumo wa dhati wa kujitafutia nusura ambao kila mwanadamu anao. Mtoto aliitafuta lugha ya malezi ili aungane na familia yake. Kutokana na nasaba yake na lugha ya kikabila, Kiswahili kilikuwa chepesi kwa mtoto. Hivyo sivyo ilivyo kwa Kiingereza.
Ama uwezekano wa kuisharabu lugha ya Kiingereza hujiegesha katika mwaka kuwa kila Mtanzania ana kipawa cha lugha. Hatuhitaji kufanya utafiti kugundua kuwa wepesi wa kusharabu lugha ni kipawa kimojawapo ambacho mtoto anaweza kuzaliwa nacho. Vipawa vingine ni kama wepesi wa ufahamu wa hisabati, jiografia, historia, kemia, fizikia na kadhalika. Tunapokubali kuwa usharabu wa lugha hutegemea kipawa cha mwanafunzi na mwalimu wake, hatuwezi kutafuta muujiza uwamiminie wanafunzi lugha ya Kiingereza kwa muda wa saa mia nane.
Pamoja na ugumu wa usharabu unaowakabili, wanafunzi hulazimika, baada ya kuvuka kiwango cha elimu ya msingi, kutumia Kiingereza kupokelea changamoto za elimu ya sekondari na vyuo vya juu. Wanatazamiwa, hivyo hivyo kimiujiza wasuke fikra zao na hapo hapo wamudu kusukua fikra za walimu na za wenzao zilisosukwa kwa lugha hiyo ya Kiingereza. Wanafunzi hao wanatazamiwa wajenge ari ya kusoma vitabu vya kusasanya na kusasanyua yale waliyosoma. Kwa maana nyingine, Kiingereza kina dhima ya kukuza dhima za wanafunzi ili mwisho wa mchakato wao wa elimu waweze kuwa chimbuko la fikra angavu. Wahitimu hao wanatazamiwa kuwa na akili zilizochata badala ya zile zinazonata.
Kutokana na dhima hii kubwa ya serikali kuhakikisha kuwa Kiingereza kimo ndani ya maisha yetu kwa mtindo huu, Kiswahili kikaendelea kudumaa, kikabaki lugha ya kuuzia nyanya. Kiswahili kinaendelea kuwa lugha ya mambo yasiyo ya kitaaluma. Mtu, kwa imani iliyopo nchini, hawezi kuwa mtaalamu ikiwa harogonyi lugha isiyojulikana katika mazingira yake. Lakini pamoja na ufili-ubishi usio na hoja -ninadhani ndani ya jamii hii wako wengi wanajua kuwa muujiza tunaotazamia hauwezi kuwa. Pengine hii inatupatia fununu ya sababu ya nchi yetu kusita kuwaamini wahitimu wetu, kwani wanajua fika kuwa wamepata matatizo katika mchakato wao wa elimu. Aidha, hakika ya tatizo la mchakato wetu wa elimu kuzaa akili zinazonata tu yaani za kukariri kariri mambo linaonekana kuwa matokeo ya mbinu za nchi za Magharibi za kuhakikisha kuwa mifumo ya elimu ya nchi changa inaendelea kutoa wahitimu wasio na uwezo wa kufikiri. Mazrui anasema kuwa uongozi wa nchi changa haung'ang'anii Kiingereza kwa hiari yao. Nchi za Magharibi hutumia matumizi ya Kiingereza kudhoofisha elimu ili nchi changa ziwe mlimbi mkubwa wa kupatia wafanyakazi walungizi si wafanyakazi watangulizi.
Uamuzi wa kuleta badiliko la lugha ya kufundishia unatokana na umaizi wa mambo makuu matatu. Na ingawa yamejadiliwa, kuyataja kwake ni kujiweka tayari kuwa maandalizi na badiliko lenyewe. Jambo la kwanza lililojadiliwa ni kule kutokuelewa kwa usahihi tatizo la Watanzania ni nini katika elimu. La pili ni kutokuelewa lugha ni nini? Na la tatu ni kule kutofahamu kuwa zoezi la kusharabu lugha lina gharama kubwa ya wakati, mali na nguvu kazi. Kulielewa tatizo la elimu Tanzania, ni hatua muhimu katika kusawiri mbinu za utekelezaji wa sera mpya ya lugha ya elimu.
|
Links | Matoleo Yaliyopita | Sign our Guestbook |