MASHAIRI


Yangelizuka majungu

   Yeye wa tangu na tangu, mwanzo mwisho hana,
   Mmoja Mwenyezi Mungu, katu mshirika hana,
   Muumba nchi na mbingu, na vyote vilojazana,
   Kuzaa na kuzaliwa, Mwenyezi kaepukana.
 
   Mfanowe hana Mungu, kiumbe akafanana,
   Si watatu kwenye mbingu, baba, roho wala mwana,
   Yangalizuka majungu, sheria kufarakana,
   Kuzaa na kuzaliwa, Mwenyezi kaepukana.
 
   Halali, hachoki Mungu, hasahau Sub hana,
   Mjuzi wa mambo chungu, yote yalofichikana,
   Kwenye ardhi na mbingu, hanaye wa kushindana,
   Kuzaa na kuzaliwa, Mwenyezi kaepukana.
 
   Mlezi Mwenyezi Mungu, atulisha Maulana,
   Mtandazaji mawingu, mvua zanyesha mwanana,
   Minanasi na mikungu, miembe inashonana,
   Kuzaa na kuzaliwa, Mwenyezi kaepukana.
 
   Kaumba Mwenyezi Mungu, sura kutofuatana,
   China, Mwarabu, Mzungu, rangi zisizofanana,
   Kabila za ulimwengu, kilugha zinapishana,
   Kuzaa na kuzaliwa, Mwenyezi kaepukana.
 
   Razaku Mwenyezi Mungu, mgawaji kwa mapana,
   Atupa pweza na changu, bahari wazaliana,
   Michuzi yajaza chungu, samaki wanoneana,
   Kuzaa na kuzaliwa, Mwenyezi kaepukana.
 
   Muweza Mwenyezi Mungu, zake sifa nyingi sana,
   Nemaze kwako na kwangu, tele zimerundikana,
   Kuhesabu kwa mafungu, idadi yashindikana,
   Kuzaa na kuzaliwa, Mwenyezi kaepukana.
 
   Beti nazifunga pingu, mwisho ninatulizana,
   Nawapisha na wenzangu, sitaki kusema sana,
   Waseme sifa za Mungu, wende wazame kwa kina,
   Kuzaa na kuzaliwa, Mwenyezi kaepukana.
 
Idd Kikong?ona,
Morogoro.


1+1+1=1 (Sisitizo)

   Saa nyingine nacheka, hawa mabwana wawili,
   Viumbe wana mashaka, ya Mungu vitendawili,
   Haja yao wanataka, eti waipinge Injili!
   Ona walivyong?ang?ana, taka mchunguza Mungu!
 
   Kama huyu S. Luanda, na mwenzake Kikong?ona,
   Kutwa kucha wanawinda, uongo kuulizana,
   Na ukweli wanapinda, viumbe wamekutana,
   Ona walivyong?ang?ana, taka mchunguza Mungu!
 
   Moja wapo wasema, Mungu mfano wa mvule!
   Mbao tatu akipima, kuwa moja iwe pale,
   Kabisa amesimama, hana hofu mtu yule,
   Ona walivyong?ang?ana, taka mchunguza Mungu!
 
   Watu hawa ni masikini, mawazo yao hafifu,
   Kabisa tu hawamwoni, Yehova wa utukufu,
   Tena hawako makini, kumwelewa mtukufu,
   Ona walivyong?ang?ana, taka mchunguza Mungu!
 
   Kwanza hivyo ni kufuru, Yehova hachunguziki,
   Meng?ang?ana kama faru, kuambiwa hawataki,
   Ngoja tuwape uhuru, wapunguze hamaki,
   Ona walivyong?ang?ana, taka mchunguza Mungu!
 
   Jambo moja sikia, ninyi mnaong?ang?ana,
   Yehova akichukia, siku hiyo mtaona,
   Takimbia mkilia, hata pa kwenda hamna,
   Ona walivyong?ang?ana, taka mchunguza Mungu!
 
   Heri mngesonga mbele, kusema ya Mwembe chai,
   Na mambo ya chama kile, kukichania uhai,
   Kulikoni jambo lile, waungwana muko hoi,
   Ona walivyong?ang?ana, taka mchunguza Mungu!
 
Mwinjilisti,
B.E. Dettu,
S.L.P. 60474,
Dar es Salaam.


Kukichagua chafaa? (Jibu)

Sikiliza D tatu, majibu beti napanga,
Hiki si chama cha watu, vyema kukipiga chenga,
Tusikipe kura zetu, kiwe kinatangatanga,
Hiki si cha kuchagua, kina mama sikiliza.

Sasa tusemeni basi, ni mwiko kukichagua,
Tukifatuwe kwa kasi, miguu kukipindua,
Rukwa, Tabora, Masasi, na kote kukiumbua,
Hiki si cha kuchagua, sikiliza kina dada.

Hii ndiyo yake dawa, wanyonge kujikwamua,
Tusiseme sawasawa, vema tukakipatia,
Hali tutaziokowa, machungu yataishia,
Hiki si cha kuchagua, sikilizeni vijana.

Balaa tutazikinga, sasa nawapasulia,
Lindi, Kigoma na Tanga, Pwani Kilwa na Songea,
Mwanza, Arusha na Iringa, ikiwa mnachungua,
Hiki si cha kuchagua, sikilizeni wazee.

Ahadi zote ni hewa, kipi tulichoambuwa?
Yale tuliyoambiwa, mbona hatukutendewa,
Yafaa kikasusiwa, cheupe kukichaguwa,
Hiki si cha kuchagua, sikiliza wananchi.

Mbele sitoendelea, cha siku nyingi sikia,
Ndicho kinachotuua, madhara kinatutia,
Dikupa nawe Luanda, julisha Watanzania,
Hiki si cha kuchagua, sikiliza wananchi!

Mtoto Mtaun (Mtafiti),
S.L.P. 4
Kilwa - Kiwawa.

--
JuuRUDI


Bonyeza hapa
kushriki mjadala au kutoa maoni juu ya habari hizi na masuala mengineyo ya Kiislamu kwenye Baraza ya Wasomaji

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtz.org

 
An-nuur Home | Ukurasa wa Mwanzo | Islam Tanzania
Links | Matoleo Yaliyopita | Sign our Guestbook