MATATIZO ya kijamii hutokea pale ambapo jamii inaamini kuwa Kiingereza ni elimu na kuwa waliopata elimu (na hasa elimu hiyo inapokuwa katika Kiingereza) ni watu bora zaidi kuliko wale wasiopata elimu hiyo, na kuwa wao pekee ndiyo wenye ujuzi. Pale jamii inapoacha kuthamini mambo yake ya msingi na kudhani kuwa mambo ya kigeni tu ndiyo yenye maana.
Matatizo ya kitamaduni yanatokana na kushindwa kukita katika tamaduni za Kiafrika elimu, sayansi, na teknolojia za kigeni, na kufanya elimu, sayansi, na teknolojia hizo kuendelea kubaki nje ya tamaduni zetu kwa kuwa lugha zinazotumika kufundishia hazieleweki kwa wanafunzi na wananchi walio wengi. Matokeo ya hali hiyo ni kudumaa kwa tamaduni za Kiafrika kwa kuwa hazipati nafasi ya kuchangamana na tamaduni hizo za kigeni, tofauti na tamaduni za Ulaya zilivyopokea sayansi na teknolojia kutoka tamaduni za Wayunani na Wagiriki na kuzimiliki kikamilifu kiasi cha kutufanya sisi tuamini kuwa, kwa mfano Kiingereza ni lugha ya sayansi na teknolojia.
Matatizo ya kiuchumi huwepo pale ambapo inabidi siku zote tuendelee kutegemea matatizo ya nje kutupatia wataalamu, vitabu, na vifaa vya elimu. Mbali na hayo kusomesha vijana kwa kutumia Kiingereza ambayo ni lugha ya kigeni ni njia mojawapo ya kuwasisitiza kuwa elimu katika lugha yao haina thamani, ndiyo maana haitakiwi shuleni. Kwa maneno mengine, elimu ikitolewa kwa lugha ya kigeni kama Kiingereza, inawaandaa vijana kutumikia mataifa ya nje kuliko taifa lao wenyewe. Ipo mifano mingi ya wasomi wa Kiafrika na wa ulimwengu wa tatu ambao wamehamia katika nchi zilizoendelea na kutumikia jamii za nchi hizo badala ya wasomi hao zikiangaliwa kiuchumi kwa ngazi ya taifa ni hasara kubwa kwa mataifa yanayosomesha vijana hao kwa lugha za kigeni.
Matatizo ya kielimu yanayotokea hasa kwa wale wanafunzi ambao hawakielewi Kiingereza na wanalazimika kutumia kama lugha ya kujifunzia. Utafiti unaonesha kuwa zaidi ya asilmia 95% ya wanafunzi katika shule za sekondari nchini Tanzania hawaelewi Kiingereza (Mlama na Matteru 1977; Campbell and Qorro 1997), kwa hiyo wanashindwa kuelewa masomo yote yanayofundishwa kwa lugha hiyo. Hii ina maana kwamba ingawa serikali na wazazi wanajitahidi kupeleka watoto shule kwa malengo na madhumuni ya kuwapatia elimu, malengo na madhumuni hayo huwa hayatimii kwa kuwa baadhi ya waalimu na wengi wanafunzi hawaelewi lugha inayotumika kufundishia, yaani Kiingereza. Kwa maneno mengine, kutumia Kiingereza kufundishia kunapingana moja kwa moja na malengo na madhumuni ya elimu nchini Tanzania.
Aina ya mwisho katika matatizo niliyoyataja ni tatizo la kiakili. Hili
ni tatizo ambalo kwa sehemu kubwa halionekani ingawa athari zake zinaweza
kuwa kubwa zaidi. Mifano yake ni pale akili inapozugwa na kufungwa kuamini
mambo ambayo wanaotawala elimu watapenda kuyaamini. Au pale akili inapokuwa
imefungwa kiasi cha kutoweza kupambanua na kutambua mambo muhimu katika
maisha. Tatizo la kiakili linaweza kuwa katika sehemu mbili, yaani, kisaikolojia
(psychological) na uelewa (cognition). Katika makala haya nitajaribu kulifafanua
tatizo hili kwa undani zaidi kwa kuwa naamini kwamba ndilo tatizo lililozaa
yale mengine niliyoyataja.
Athari za tatizo la kiakili
Kisaikolojia (Msimamo na mtazamo)
Athari kubwa ya tatizo la kisaikolojia ni kutojiamini ambayo mifano yake ni kama vile kudhani kuwa:
Sisi Waafrika tuna upungufu mkubwa kama binadamu, kwa hiyo kuiga mambo ya wengine ndiyo kunakamilisha utu na ubinadamu wetu;
hatukuwa na elimu yoyote mpaka walipokuja wazungu kutuletea kutoka Ulaya;
utamaduni wetu una hitilafu kwa hiyo ni wa kuachwa na kuchukua utamaduni wa watu wengine;
lugha zetu hazina maana wala mchango wowote katika ulimwengu wa kisasa kwa hiyo kuziendeleza lugha hizo ni kurudi nyuma;
vyakula vyetu siyo bora kwa hiyo haviwezi kutupa siha inayohitajika mwilini;
elimu, sayansi na teknolojia ni mambo ya wazungu kwa hiyo ili tuvipate hatuna budi kuachana na mambo yetu na kuiga yote ya kwao ndipo tutapata maendeleo, na athari nyingine nyingi zitokanazo na kutojiamini.
Hali hii ya kutojiamini inafanya tunakosa pa kuanzia kwa kuwa imetufanya
tuyachukie mambo yetu yote; kwa maneno mengine tunaushuku utu na ubinadamu
wetu (self-negation). Yaani hatujiamini kama tu watu kamili, ambao tuna
mambo yetu ya msingi yanayodumisha na kuendeleza maisha yetu na uhai wetu.
Hali hii ya kutojiamini ni tatizo kubwa kwa kuwa ni kinyume kabisa na matakwa
ya maisha ya ulimwengu wa sasa kwamba kama binadamu wengine, nasi pia tuna
mchango mkubwa katika jamii ya binadamu duniani. Kwa hiyo ni lazima tujiamini
na tuchukue nafasi yetu katika ulimwengu ya kujiletea maendeleo yetu wenyewe.
Uelewa
Tatizo la uelewa (cognition) inahusiana na lile la kielimu lililozungumziwa
hapo awali. Tatizo hili linatokea kwa kuwa wanafunzi walio wengi hawaelewi
Kiingereza kwa hiyo wanashindwa kuelewa mada ya masomo yanayofundishwa,
matokeo yake ni kudumaa kwa uelewa wao kiakili. Kwa mfano tuanaglie maandishi
ya mwanafunzi katika ngazi mbalimbali ya elimu:
Vielelezo
Kielelezo cha kwanza
Kidato cha kwanza, somo la Biolojia. Mada: Osmosis.
OSMOSIS
Osmosis is the movement of the solvent from the solution of lower contatration to that of higher concatration throgh a simipermiable membrane.
Osmosis accurs when two solution of aliffenat contration allowed to pass to high concetration through a semi permiable me semi permiable mebrane is the one which allow same at the material to pass throgh it. Example: (i) membrane (ii) cell wall at plant edl etc.
Solvent is the liquid which is especially used for dissoving solute is water. Solute is any sustance whi one mixed with result to the farmation at solution that is it dissoleves is solved.
Solution: Is the resulting mixture obtained when solvet dissolve in solvent. Osmotic pressure is the force or obility fo the solvent a semipemiable membrane.
Maandishi haya mwanafunzi ameyanakili kutoka ubaoni, na inaonekana kuna maneno ameyanakili visivyo sahihi, kama maneno concentration, through, semipermiable na of a different concentration. Hali hii inatoa hisia kuwa mwanafunzi huyu haelewi au hana hakika na muundo wa maneno haya bali anaigiza herufi kutokana na jinsi anavyosoma hati ya mwalimu wake. Kwa hiyo mwalimu anapokosea kuandika neno wanafunzi hawana uwezo wa kutambua na kuuliza ili kuhakikisha usahihi wake. Vyovyote atakavyoandika mwalimu, wanafunzi hunakili hivyo hivyo. Wakati mwingine ni vigumu kujua kama ni makosa ya mwalimu au ya wanafunzi. Mifano ya makosa kama hayo ni mingi.
|
Links | Matoleo Yaliyopita | Sign our Guestbook |