UKIONDOA makofi yaliyopigwa na viongozi jukwaa kubwa, sehemu kubwa ya wananchi ilikuwa kimya Rais alipoingia uwanjani.
Akiwa amesimama sambamba na Mkuu wa Majeshi, Rais Benjamin Mkapa aliingia uwanjani katika gari la wazi la kijeshi huku mapikipiki kadhaa
yaliyokuwa pembezoni mwa gari hilo yakileta mbwembwe za hapa na pale.
Tofauti na uchangamfu uliozoeleka miaka ya nyuma wanapowasili viongozi wa kitaifa katika maadhimisho kama hayo, wananchi walionekana kuendelea na mazungumzo yao hata pale Rais alipowapungia mkono kuwasalimia.
Moyo wa uzalendo umeondoka, anasema mwalimu mmoja wa shule ya sekondari akitoa maoni kuhusu tukio hilo.
"Yawezekana wamekatishwa tamaa na mwenendo wa viongozi wao", amedai mwalimu huyo.
Sherehe za miaka 36 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar zilifanyika juzi sehemu mbalimbali nchini.
Jijini Dar es Salaam, Rais Benjamin Mkapa alikagua gwaride la vikosi vilivyowakilisha majeshi yote nchini.
Viongozi wote wa kitaifa walihudhuria sherehe hizo ambazo ni za kwanza kutohudhuriwa na waasisi wake wote.
Tanganyika na Zanzibar ziliungana Aprili 1964 ambapo Marais wa wakati huo, Mwalimu Nyerere na Mzee Abeid Aman Karume walitia saini kwa niaba ya nchi zao.
Hata hivyo, kumekuwa na malalamiko mengi kuhusiana na muungano huo kutoka pande zote ikidaiwa mkataba una utata na haukidhi matakwa ya wananchi.
Baadhi ya watu walioonesha dosari za Muungano ni pamoja na aliyekuwa Rais wa Zanzibar na Makamu wa Kwanza wa Rais wa serikali ya Muungano, Alhaj Aboud Jumbe.
Akihojiwa na waandishi wa habari mara baada ya sherehe hizo juzi, Mwenyekiti
wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba alisisitiza kurekebishwa kwa dosari zilizojitokeza
katika Muungano zirekebishwe ili kukidhi matakwa ya wananchi wa pande zote
mbili.
--
![]()
|
Links | Matoleo Yaliyopita | Sign our Guestbook |