Wanafiki wasipewe fursa Misikitini
QUR'AN inasema: Na wako (wanafiki) waliojenga Msikiti wa (kuleta) udhia na hutia nguvu ukafiri na kuwafarikisha walioamini na kuufanya mahali pa kuwangojea wale waliomfanyia vita Mwenyezi Mungu na Mtume wake zamani. Na bila shaka wataapa (waseme): "Hatukukusudia ila wema". Lakini Mwenyezi Mungu anashuhudia kuwa wao ni waongo. (9:107).
Ni imani yetu kwamba Waislamu wanapotoa fedha zao kujenga Misikiti, lengo waingie humo watu wanaopenda kujitakasa. Watu awapendao Allah. Watu wenye imani thabiti, wenye kuihami dini ya Allah.
Hakuna Muislamu anayetoa sadaka yake kujenga Msikiti ili uje kuwa kichaka cha wanafiki. Wanafiki ambao wawapo mgongoni Waislamu huwafitini Waislamu kwa makafiri bila kuhofu madhara ya kauli na fitna zao kwa waumini wenzao.
Uislamu ni kunaswihiana. Tunadhani Waislamu wanawajibu mkubwa kuhakikisha kuwa Misikiti haigeuzwi maficho ya kumpiga vita Mwenyezi Mungu, Mtume wake na waumini wake. Wala kuwa vituo vya mawasiliano kati ya wanaowadhulumu na kuwanyanyasa Waislamu na mawakala wao.
Na tukumbuke kuwa "wanaoamirisha (wanaosimamia na kufanikisha) Misikiti ya Mwenyezi Mungu ni wale wanaomwamini Mwenyezi Mungu na siku ya Mwisho, na kusimamisha sala na kutoa zaka na hawamuogopi yeyote ila Mwenyezi Mungu, basi hao ndio wanaotarajiwa kuwa miongoni mwa walioongoka. (9:18).
|
Links | Matoleo Yaliyopita | Sign our Guestbook |