UISLAMU unamuona mwanaadamu yoyote, akiwa wa nchi moja au wa nchi nyingine, akiwa mkazi wa jangwani au wa msituni, akiwa mfalme au raia, akiwa Muumini (Muislamu) au kafiri, kwa vyovyote vile atakavyokuwa, maadamu yeye ni mwanaadamu anastahiki kupata Haki za kimsingi za binaadamu. Haki za Kimsingi zinazohusu wanaadamu wote ni hizi zifuatazo:-
(a) Haki za Kuishi (maisha)
(b) Haki ya Usalama wa maisha
(c) Haki ya kuheshimu Usafi wa wanawake (Utoharifu).
(d) Haki ya kupata mahitaji ya lazima ya maisha.
(e) Haki ya Uhuru (Kila mtu kuwa huru)
(f) Haki ya Uadilifu katika hukumu (Right to justice)
(g) Haki ya Usawa.
(a) Haki ya Kuishi (Maisha)
Kila mtu pasina ubaguzi wa aina yoyote ana haki ya kuishi na kulindwa maisha yake. Kumuua mtu yeyote awaye ni kosa la jinai na muuaji ni lazima ahukumiwe kwa sheria ya Kiislamu. Makemeo ya Qur'an kuhusu kosa hili yanadhihirisha kwa uwazi ubaya wa kumuua mtu yoyote pasi na haki:
Kwa sababu ya hayo tukawaandikia wana wa Israil ya kwamba atakayemuua mtu bila ya yeye kuua mtu, au bila ya kufanya fisadi katika nchi; basi ni kama amewaua watu wote... (5:32).
"... Wala msimuue mtu ambaye Mwenyezi Mungu ameharamisha (kuuawa) ila ikiwa (imetokea) haki (ya kuuawa)..." (6:151).
Hukumu ya muuaji ni kuuawa kama inavyobainishwa katika Qur'an:
Wala msiue nafsi ambaye Mwenyezi Mungu ameiharamisha kuuawa isipokuwa kwa haki (Akahukumu hakimu wa Kiislamu kuwa mtu amestahiki kuuawa na akatoa amri ya kuuawa), nani mwenye kuuawa kwa kudhulumiwa, basi tumempa nguvu mrithi wake (juu ya muuaji huyo, akitaka ataomba kwa hakimu kuwa amuue au akitaka amtoze fidia au akitaka (amsamehe). (17:33).
(b) Haki ya Usalama wa Maisha
Kila mtu anayo haki ya kuokolewa au kupata ulinzi utakaomuweka katika hali ya usalama bila ya ubaguzi wa aina yoyote. Tunafahamishwa katika Qur'an kuwa:
"... Na mwenye kumwacha mtu hai (kumsaidia kuishi) ni kama amewaacha hai watu wote..." (5:32).
Kila mtu awe mgeni au raia ana haki ya kupata mahitajio muhimu ya maisha yatakayomuwezesha kuishi, na kila mtu anayo haki ya kupata hifadhi itakayomuhakikishia kuishi kwa usalama.
(c) Haki ya Kuheshimu Usafi wa wanawake
Ili kuhakikisha kuwa kila mwanamke anapata hifadhi ya kutoguswa na mwanaume yoyote awaye nje ya utaratibu wa ndoa. Kitendo cha zinaa au kishawishi chochote cha zinaa kimekatazwa katika Uislamu bila ya kujali kuwa kimefanywa na Muislamu au na asiye Muislamu, kimefanywa na raia au mgeni. Makemeo ya Qur'an juu ya kitendo hiki ni haya yafuatayo:
Wala msikaribie zinaa. Hakika hiyo ni uchafu na ni njia mbaya kabisa. (17:32).
Uzinifu katika Uislamu ni kosa la jinai na mzinifu yeyote anastahiki adhabu kali ya kupigwa viboko mia moja. (Qur'an, 24:2) au kupondwa mawe mpaka kufa bila ya ubaguzi wa aina yote.
(d) Haki ya kupata mahitaji ya lazima ya maisha
Katika Uislamu kila mtu ana haki ya kupata mahitaji ya lazima kama vile chakula, malazi, mavazi, matibabu, elimu, n.k. bila ubaguzi wowote ule uwe wa rangi, dini, kabila, au utaifa. Kwa wale wasio na uwezo wa kujikimu mahitaji hayo ni jukumu la wenye uwezo kuwasaidia:
"Na ambao katika mali zao iko sehemu maalumu. Kwa ajili ya aombaye na anayejizuilia kuomba (japo anahitaji)." (70:24-25).
Uislamu unatuamrisha kwamba, kama mtu anao uwezo na mtu mwingine akamuomba msaada au hata kama hajamuomba lakini anajua kuwa anahitaji msaada ni wajibu wake kumsaidia. Mwenyezi Mungu (s.w.) amepitisha riziki ya mja wake huyo kupitia kwa mwenye uwezo.
(e) Haki ya Uhuru
Ili kuhakikisha kuwa kila mtu anakuwa huru na hawi mtumwa wa mwingine kimabavu au kifikra, Uislamu umeliweka suala la mamlaka au utukufu kwa Mwenyezi Mungu (s.w.). Uislamu umeharamisha kitendo cha kumfaya mtu huru kuwa mtumwa au kumuuza kwenye masoko ya watumwa. Kuhusu habari hii Mtume Muhammad (s.a.w.) anatuambia kama yafuatavyo:
"Kuna watu wa aina tatu ambao Mimi mwenyewe nitasimama kuwashitaki katika Siku ya Hukumu (Siku ya Hesabu), miongoni mwa hao ni yule anayemfanya mtu huru kuwa mtumwa na kumuuza..." (Bukhari).
Maneno haya ya Mtume (s.a.w.) yanawahusu wanaadamu wote bila ya kujali utaifa wao, rangi zao, dini zao na kadhalika. Hata hivyo kumekuwa na propaganda kuwa Uislamu ndio ulioeneza utumwa na nchi za Magharibi ndizo zilizokuja kukomesha utumwa. Pamoja na madai kwamba ni nchi za Magharibi zilizokuja kukomesha utumwa baada ya nusu ya karne ya 19 lakini watu hao hao kabla ya wakati huo ndio walioivamia Afrika na kuwateka Waafrika waliokuwa huru, wakawafunga na kuwasafirisha kwenye makoloni yao mapya kama vile Amerika, Australia na New Zealand. Waafrika hawa waliotekwa na kufanywa watumwa walifanyiwa vitendo vya ukatili mno; kuliko wanyama. Hata vitabu vilivyoandikwa na watu hawa wa Magharibi (Wazungu) vinashuhudia ukweli huu. Hebu tuangalie Historia fupi ya Biashara ya watumwa ilivyofanywa na mataifa ya Kimagharibi na Kanisa.
|
Links | Matoleo Yaliyopita | Sign our Guestbook |