Suluhu kati ya mume na mke

WANAADAMU wanapoishi pamoja, kutokana na udhaifu wa kibinaadamu kukwaana na kugombana ni jambo la kawaida. Hivyo mume na mke ambao wako karibu sana, hawana budi kuvumiliana kwa kiasi kikubwa.

Mmoja akimwona mwenzie amekasirika hana budi kutulizana na kujifanya kama mjinga. Kila mmoja hana budi kujitahidi kwa jitihada zake zote kumtendea wema mwenzake na kumpa haki zake. Vile vile kila mmoja hana budi kuwa tayari kusamehe haki ndogo ndogo alizonyimwa na mwenziwe. Mwenendo huu wa kuvumiliana na kusameheana hudumisha amani na upendo katika nyumba. Hatuna budi kukumbuka kuwa kuvumiliana na kusameheana, hakuleti tu furaha na amani katika nyumba na katika jamii kwa ujumla bali pia ni matendo ya kiucha-Mungu yenye malipo makubwa mbele ya Mwenyezi Mungu (s.w.) kama tunavyojifunza katika aya zifuatazo:

"... Na wasamehe na waachilie mbali (yaliyopita). Je, nyinyi hampendi Mwenyezi Mungu akusameheni? Na Mwenyezi Mungu ni Mwingi wa msamaha, Mwingi wa rehema (basi nanyi sifikeni na sifa hizi)". (24:22).

Na malipo ya ubaya ni ubaya ulio sawa na ubaya huo; lakini anayesamehe na kusuluhisha ugomvi, ujira wake uko kwa Mwenyezi Mungu; bila shaka Yeye hawapendi madhalimu. (42:40).

Aya hizi zinatufahamisha kuwa kusamehe ni sababu ya mtu kusamehewa makosa yake na Mola wake na pia ni sababu ya kupata malipo makubwa mbele ya Mwenyezi Mungu (s.w.). Hivyo ikitokea mume na mke wakahitilafiana na kugombana, hawana budi kujisuluhisha wenyewe kwa njia hii ya kusubiri na kusameheana kama Mwenyezi Mungu (s.w.) anavyotushauri katika Qur'an:

Na kama mke akiona kwa mume wake kugombana-gombana na kutengana-tengana, basi si vibaya kwao wakitengeneza baina yao suluhu (njema wakastahimiliana bila kuachana) maana sulhu ni kitu bora. Na nafsi zimewekewa ubakhili (hakuna mtu anayetaka kuiachia mwingine haki yake). Na kama mkifanya mema (kuwafanyia wake zenu) na mkimcha Mwenyezi Mungu (msiwapunguzie haki zao, bila shaka Mwenyezi Mungu atakupeni) kwani Mwenyezi Mungu anazo habari za yote mnayoyatenda. (4:128).

Ikitokea mume na mke wenyewe wameshindwa kusuluhisha mpaka ugomvi ukajitokeza nje, Waislamu walio karibu nao kwa urafiki, ujirani, udugu, n.k. waingilie kati na kuwapatanisha ndugu zao kabla sumu ya shetani haijaenea katika nyumba. Msuluhishaji atumie busara kubwa na ajitahidi kwa kadiri ya uwezo wake katika kufanya kazi hiyo akijua kuwa hiyo ni kazi nyeti na yenye malipo makubwa sana mbele ya Mwenyezi Mungu (s.w.) kama tunavyosoma katika Qur'an:

Hakuna kheri katika mengi wanayoshauriana kwa siri. Isipokuwa (mashauri ya) wale wanaoamrisha kutoa sadaqa au kufanya mema au kupatanisha baina ya watu. Na atakayefanya hivi kwa kutaka radhi ya Mwenyezi Mungu, basi tutampa ujira mkubwa. (4:114).

Msuluhishi huyu akishindwa, kabla mume hajakimbilia kutoa talaka au mke hajakimbilia kudai talaka, ni vyema Waislamu hawa wakashitakie ugomvi wao kwa Kadhi. Kadhi atajitahidi kuwapa mawaidha mazuri na kumkumbusha kila mmoja haki zake na wajibu wake kwa mwingine, kisha baada ya kumsikiliza kila mmoja wao kuhusiana na ugomvi wao, hatatoa uamuzi pale pale bali ataomba muda wa kupekua zaidi kesi hiyo. Kadhi atachagua ndugu waadilifu kutoka kila upande watakao msaidia kupeleleza kiini cha ugomvi na ni nani aliye mkosea mwenziwe. Kisha Kadhi atamuita mume na mke na kuwapatanisha akisaidiana na jamaa wa kwa mume na wa kwa mke. Kadhi atamsihi mkosa asirejee tena makosa yake na amtake mwenziwe msamaha na vile vile aombe msamaha kwa Mwenyezi Mungu (s.w.). Pia aliye kosewa ataombwa msamehe mwenzake ili naye Mwenyezi Mungu amsamehe makosa yake na kupata ujira mkubwa kutoka kwake. Wawili hawa wakiwa na nia ya suluhu, baada hatua hizi, Mwenyezi Mungu (s.w.) ameahidi kuwapatanisha kama tunavyojifunza katika aya ifuatayo:

Na kama mkijua kuwa kuna ugomvi baina ya mke na mume basi pelekeni mwamuzi mmoja katika jamaa za mwanamume na mmoja katika jamaa za mwanamke. Kama wakitaka mapatano Mwenyezi Mungu atawapatanisha. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mjuzi wa habari za siri na habari za dhahiri. (4:35).

Ni nani mbora wa kutekeleza ahadi yake kuliko Mwenyezi Mungu? Hivyo, mume na mke wasikimbilie talaka bali wajitahidi kutafuta sulhu baina yao kwa nia njema na kwa jitihada zao zote. Ndipo waachane endapo suluhu itashindikana kabisa. Na kutokana na ahadi hii, haitashindikana endapo watakuwa wacha Mungu.

Pia kabla ya kufikia hatua ya talaka, mume na mke wanaruhusiwa kutengana kwa muda wa miezi minne. Suluhu ikishindikana katika muda huo itabidi waachane kama tunavyojifunza katika Qur'an:

Kwa wale wanaoapa kwamba watajitenga na wake zao, (muda wao) ni kungojewa miezi minne. Na kama wakirejea, basi Mwenyezi Mungu ni mwingi wa kusamehe, mwingi wa kurehemu. Na wakiazimia kuacha (basi) Mwenyezi Mungu ni mwenye kusikia, mwenye kujua. (2:226-227)

--
JuuRUDI


Bonyeza hapa
kushriki mjadala au kutoa maoni juu ya habari hizi na masuala mengineyo ya Kiislamu kwenye Baraza ya Wasomaji

   Kutoa maoni yako kuhusu ukarasa huu: Bonyeza hapa
Au
Andika barua  kwa: webmaster@islamtz.org


An-nuur Home | Ukurasa wa Mwanzo | Islam Tanzania
Links | Matoleo Yaliyopita | Sign our Guestbook